Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na
Uvuvi, Profesa Elisante Ole Gabriel (katikati) akisisitiza jambo wakati
akiongea na Timu ya Wataalamu kutoka Manispaa ya Ilala (hawapo pichani)
waliokuja kumtembelea ofisini kwake jijini Dodoma Juni 26, 2020. Kulia ni Afisa
Mipango wa Manispaa ya Ilala, Ando Mwankuga. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa
Idara ya Uzalishaji, Mifugo na Masoko, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Abdallah
Temba.
Afisa Mipango wa Manispaa ya Ilala, Ando Mwankuga akieleza lengo la ziara yao kwa
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Profesa Elisante Ole Gabriel (kulia)
walimpomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma mapema Juni 26, 2020.
Kaimu Meneja wa Machinjio ya Dodoma,
Dkt. Conrad Ndomba (kulia) akiongea na Afisa Mipango wa Manispaa ya Ilala, Ando
Mwankuga (kushoto) alipotembelea machinjio ya Dodoma pamoja na timu yake
kujifunza namna machinjio hiyo inavyoendeshwa.
Na Mbaraka Kambona,
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na
Uvuvi, Profesa Elisante Ole Gabriel amezishauri Halmashauri zote nchini ambazo
zinafanya shughuli za ufugaji kujenga Machinjio za kimkakati ili kupanua fursa
ya soko la nyama na kuongeza mapato ya Halmashauri hizo.
Profesa Ole Gabriel alitoa rai hiyo
ofisini kwake jijini Dodoma Juni 26, 2020 alipokutana na Timu ya Wataalamu
kutoka Manispaa ya Ilala waliokuja kutembelea Machinjio ya Dodoma ili kujifunza
namna ambavyo machinjio hayo yanavyoendeshwa.
Akiongea na Wataalamu hao, Prof. Ole
Gabriel alisema itapendeza kama kila halmashauri ikawa na machinjio ya kisasa
kwani yatasaidia kuongeza mapato ya halmashauri hizo na kuachana na kukimbizana
kila siku na waendeshaji wa machinjio yaliyopo sasa ambayo hayana viwango
ambavyo vinatakiwa.
“Niwaombe Makatibu Tawala wa Mikoa
waliangalie hili, waone uwezekano wa kujenga machinjio ya kisasa yatakayosaidia
kuboresha mazingira ya biashara yatakayochagiza kuongezeka kwa mapato ya
Halmashauri,”alisema
Aliongeza kuwa sio lazima Halmashauri
zijenge Machinjio wao wenyewe, wanaweza kuingia ubia na sekta binafsi na
wakajenga machinjio ya kisasa wakawa wanauza nyama katika soko la ndani na nje
ya nchi, kodi ya Serikali ikawa inalipwa na wateja wakaendelea kupata huduma
nzuri.
Prof. Ole Gabriel aliendelea kusema
kuwa biashara ya nyama sio ndogo huku akifafanua kuwa kwa sasa wastani wa kilo milioni 2.6 za nyama zinaliwa
nchini kila siku na hivyo aliwahimiza maafisa biashara kuelimisha jamii kuhusu
zao la nyama ili watu wale nyama kwa wingi.
“Kwa mujibu wa Shirika la Chakula na
Kilimo Duniani (FAO) mahitaji ya kidunia kwa mtu mmoja anatakiwa kula kilo 50
kwa mwaka, lakini sisi Watanzania bado wastani wetu wa kula nyama kwa mtu bado
upo chini sana, kwa sasa tumefikia kilo 15 kwa mwaka, bado kiasi ni kidogo
sana,”alieleza
“Maafisa biashara tumieni taaluma
zenu kuelimisha umma kuhusu zao la nyama
ili watu wale nyama, watu wakila nyama kwa wingi itachagiza biashara ya
machinjio na ndipo hasa uwekezaji pia utakwenda vizuri,”alisisitiza
Aidha, aliipongeza Halmashauri ya
Bahi kwa jitihada wanazoendelea nazo za kujenga machinjio ya kisasa jambo
ambalo litaboresha biashara ya machinjio na kuongeza pato la Halmashauri hiyo.
Akielezea kuhusu machinjio ya Dodoma,
Prof. Ole Gabriel alisema kabla machinjio hayo hayajachukuliwa na Serikali
ng’ombe waliokuwa wanachinjwa kwa siku ni kati ya 40 mpaka 50 lakini toka
machinjio hiyo irudishwe serikalini namba ya ng’ombe wanaochinjwa imepanda kufikia 150.
“Mikakati tuliyonayo kuhusu machinjio
ya Dodoma ni kuendelea kuiboresha kufikia kuwa machinjio ya mfano kwa Afrika
Mashariki, Ukanda wa Nchi za SADC na hata ikiwezekana Afrika,”alisema
Aidha, Prof. Ole Gabriel aliwahakikishia
wataalamu hao kuwa Wizara ipo tayari kushirikiana na Manispaa ya Ilala
kuhakikisha mipango yao inafanikiwa na machinjio hiyo iweze kufanya kazi zake
kama walivyokusudia.
Naye Afisa Masoko wa Manispaa ya
Ilala, ambaye pia ndiye alikuwa kiongozi wa timu hiyo ya Wataalamu, Ando Mwankuga
alisema machinjio ya Ilala ni mradi wa kimkakati katika kuboresha mazingira ya
biashara ya machinjio ambayo itawawezesha kuwa na nyama za viwango
zitakazouzika hata nje ya nchi.
“Lengo la mradi ni kuongeza mapato ya
Manispaa, tunaamini mradi huu mkubwa ambao utakuwa unachinja ng’ombe 1500 na
mbuzi 1000 kila siku ukikamilika na
kuanza kazi Disemba, 2020 tutapunguza utegemezi kwa Serikali,” alisema.
No comments:
Post a Comment