HOTUBA YA MAONI
YA KAMATI YA KUDUMU YA FEDHA, BIASHARA NA KILIMO KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI YA WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO
KWA
MWAKA WA FEDHA 2020/2021
Mheshimiwa Spika,
Awali ya yote
namshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kuendelea kutujaalia uhai na uzima na
kutuwezesha kukutana ndani ya Baraza lako Tukufu kwa ajili ya shughuli zetu za
upitishaji wa Bajeti. Nashukuru pia kwa kunipatia fursa hii ya kuwasilisha
maoni ya Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo kuhusu makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwaka 2020/2021.
Mheshimiwa
Spika,
Nachukua fursa hii kumpongeza
Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapindhuzi Dkt. Ali Mohamed
Shein kwa uongozi wake imara ambao umepelekea nchi yetu kudumu katika hali ya
amani na utulivu hadi leo hii. Nawapongeza pia wananchi wote wa Zanzibar kwa
kufuata maelekezo ya Wizara ya Afya na miongozo ya viongozi wetu na hatimaye
kuyadhibiti maradhi hatari ya Covid - 19 kwa jamii. Namuomba Mola Mtukufu azidi
kutunawirisha na kutuondolea janga hili ambalo limeikumba dunia nzima. Azma
kubwa tuwe na afya imara ili tuweze kujenga uchumi wa nchi yetu kwa manufaa ya watu
wote.
Mheshimiwa
Spika,
Naomba sasa niwatambue kwa kuwataja
majina Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo ambao walitoa
mchango na ushauri mkubwa katika utekelezaji wa kazi za Kamati kwa Wizara hii,
Wajumbe wenyewe ni:-
1.
|
Mheshimiwa
Dkt. Mwinyihaji Makame
|
-
|
Mwenyekiti;
|
2.
|
Mheshimiwa
Hamida Abdalla Issa
|
-
|
Makamo
Mwenyekiti;
|
3.
|
Mheshimiwa
Ahmada Yahya Abdulwakil
|
-
|
Mjumbe;
|
4.
|
Mheshimiwa
Moh’d Mgaza Jecha
|
-
|
Mjumbe;
|
5.
|
Mheshimiwa
Mussa Ali Mussa
|
-
|
Mjumbe;
|
6.
|
Mheshimiwa
Nadir Abdullatif Yussuf
|
-
|
Mjumbe;
na
|
7.
|
Mheshimiwa
Wanu Hafidh Ameir
|
-
|
Mjumbe.
|
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yetu pia inashirikiana vyema na makatibu wetu wawili ambao kwa kiasi kikubwa
wamekuwa wakitusaidia kutekeleza majukumu yetu. Makatibu hao ni:
1.
|
Ndugu
Asma Ali Kassim
|
-
|
Katibu
|
2.
|
Ndugu
Said Khamis Ramadhan
|
-
|
Katibu
|
Mheshimiwa Spika,
Kamati ya Fedha,
Biashara na Kilimo ilikutana na Wizara ya Fedha na Mipango na kujadili
mapendekezo ya mapato, matumizi na Miradi ya Maendeleo ya Fungu FOI la Wizara
ya Fedha na Mipango, fungu F02 la Mfuko Mkuu wa Serikali na fungu F03 la Tume
ya Mipango. Kiujumla, Kamati yetu imeyakubali na kuyaridhia makadirio ya
mafungu hayo.
Mheshimiwa
Spika,
Jitihada
za Wizara kutafuta mapato, kuyatunza vyema na hatimaye kuyatumia ipasavyo ni
suala la kupigiwa mfano. Tunawapongeza wafanyakazi wote waliopo kwenye
ukusanyaji wa mapato kwa kazi yao nzuri. Kamati yetu inaipongeza Wizara kwa
sera nzuri za fedha na kodi ambazo zina mwelekeo wa kuisaidia sekta binafsi
kuimarika.
Mheshimiwa
Spika,
Tunaipongeza
Wizara ya Fedha na Mipango kwa uandaaaji wa bajeti hii. Naomba ifahamike kwamba
leo tunazungumzia bajeti ya Wizara na si bajeti ya Taifa. Wizara hii ndio
dhamana wa upangaji wa mipango ya maendeleo ya nchi yetu kwa kushirikiana na
sekta mbalimbali. Tunaipongeza Wizara kwa kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi. Hata
hivyo, tunaishauri Wizara kuratibu na kusimamia vyema shughuli za miradi
inayosimamiwa na Wizara zaidi ya moja kama suala la mwani, mashamba ya mpira
mafuta na uwekezaji kwa ujumla.
Mheshimiwa
Spika,
Aidha,
tunaishukuru Wizara ya Fedha na Mipango ambayo ndiyo dhamana wa uwekezaji kwa
kuandaa mpango mzuri kwa miradi mikubwa ya makaazi ikiwemo mradi wa Penny
Royal, mradi wa ujenzi wa nyumba ziliopo Nyamanzi (Fumba Town Development)
pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba za Bakhresa uliopo Fumba. Tunaiomba
Serikali yetu sikivu iweke masharti nafuu kwa wanunuzi wa nyumba hizo ili
kuwavutia wanunuzi kutoka ndani na nje ya nchi, pia kuimarisha uwekezaji
uliokusudiwa.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati iliarifiwa kuwa jumla ya
shilingi Trilioni Moja, Bilioni Mia Tano
Arubaini na Tisa, Milioni Mia Tatu na Arubaini, Laki Nane na Ishirini na Nne
Elfu zinatarajiwa kukusanywa na Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwaka
2020/2021. Kiwango hiki cha mapato ni kikubwa ikilinganishwa na shilingi Trilioni Moja, Bilioni Mia Tatu Thamanini
na Tatu, Milioni Arubaini na Tisa, Laki Saba na Thalathini na Tatu Elfu zilizokusanywa
mwaka 2019/2020. Ongezeko hilo limetokana na makusanyo ya ada ya ukodishwaji
ardhi, mapato ya Bodi ya Uhandisi, Bodi ya Wakandarasi na Bodi ya Uhaulishaji
Ardhi kuingizwa Wizara ya Fedha na Mipango kutoka Wizara inayohusika na Ardhi.
Mheshimiwa
Spika,
Mabadiliko haya yamefanywa baada ya
kubainika kuwa muundo wa Bodi hizo hauko kimamlaka na hivyo kiutaratibu hazina
mamlaka ya kutumia fedha hizo. Aidha, Serikali imebaini matumizi yasiyoridhisha
ya sehemu ya fedha hizo na kuamua kuziingiza kwenye mfuko mkuu ili kuhifadhiwa
vizuri na kufanyiwa matumizi sahihi yaliyopangwa.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo
imebaini kwamba kuna upotevu mkubwa wa mapato unaotokana na kutotumika kwa
mashine za kiektroniki (EFD Machine) hususan katika vituo vya ununuzi wa mafuta
ya vyombo vya usafiri. Kadhalika, kamati yetu inatambua kwamba wananchi wetu
wengi hawana uelewa au utamaduni wa kudai risiti baada ya kupatiwa huduma. Wauzaji nao huwa wagumu kutoa risiti kwa
makusudi ili kukwepa kulipa kodi. Kwa mantiki hiyo, Kamati yetu inaitaka Wizara
ya Fedha na Mipango kuharakisha ukamilishaji wa mfumo na taratibu za matumizi
ya mashine za kielektroniki pamoja na kutoa elimu kwa wananchi na
wafanyabiashara kwa ujumla kuhusu umuhimu wake kwa uchumi wetu.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati hii imegundua kuna mambo mengi mazuri
ya maendeleo na yametekelezwa na Wizara za Serikali katika hali ya kuridhisha. Hata hivyo, Kamati inasisitiza haja ya kuwepo
utaratibu mzuri wa ufuatiliaji wa karibu zaidi katika uandaaji wa miradi ya
maendeleo na utekelezaji wake. Kuna matokeo kadhaa ya migongano kati ya Wizara
zetu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta zao kutokana na
kukosekana kwa uratibu wa karibu wa kazi zinazofanyika
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu imeelezwa kwamba azma ya kuendeleza
na kukamilisha ujenzi wa Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume
(Terminal III) ipo kama ilivyopangwa pamoja na kuibuka kwa janga hili la homa
kali ya mapafu (Covid - 19). Kuwepo kwa hali hiyo kumechangia kuongezeka kwa
muda wa makabidhiano hadi kufikia mwezi Januari 2021. Tunaipongeza tena
Serikali yetu ya Mapinduzi Zanzibar kwa uamuzi wa busara wa kuazimia kumaliza
ujenzi wa terminal III kwa fedha zetu wenyewe.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu inaipongeza Wizara ya Fedha
na Mipango na Serikali kwa ujumla kwa kulisimamia ipasavyo deni letu la Taifa
kuwa katika hali ya uhimilivu kwani ukilinganisha mwezi Machi, 2019 na Mwezi
Machi 2020, deni hilo limepungua kwa asilimia 2.6. Hali hiyo imetokana na
kuongezeka kwa asilimia 13.3 ya deni la ndani ambalo Serikali imekopa kupitia
Taasisi ziliopo nchini. Kamati yetu inaafiki utaratibu huo kwa vile taratibu za
kupatikana na kulipa kwake huwa hauna vikwazo vingi na hata riba yake riba yake
ni rafiki na mazingira halisi tuliyonayo.
Mheshimiwa
Spika,
Moja kati ya vipaumbele ambavyo Wizara ya
Fedha na Mipango imepanga kuvitekeleza katika bajeti ya mwaka 2020/2021 ni
uimarishaji wa shughuli za kitengo cha uchumi wa buluu (Blue Economy). Kamati
yetu imeridhishwa na hatua hiyo ya Wizara kwa kuibua kipaumbele hicho kwani
nchi yetu bado haijazitumia na kunufaika ipasavyo na rasilimali zinazotokana na
Uvuvi wa Bahari Kuu, usafiri na usafirishaji Baharini, utalii wa Baharini
pamoja na rasilimali za mazao ya baharini hususan mwani ambapo kimaumbile kila
kona ya nchi yetu imezungukwa na Bahari. Kwa mantiki hiyo, kama sekta ya Uchumi
wa Buluu itafanyiwa kazi kikamilifu kama ilivyopendekezwa na Wizara itaweza
kutuongezea mapato maradufu na kuimarisha uchumi pamoja na maisha ya wananchi
wetu.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yetu imepata malalamiko kutoka
kwa wawekezaji kadhaa nchini kwamba baadhi ya fursa za uwekezaji walizopatiwa
wengine kabla yao, zimeanza kusita kutolewa na taasisi husika ikiwemo msamaha
wa kodi wa asilimia 20 kwa uingizaji wa rasilimali za awali (capital costs).
Kamati yetu inashauri lizingatiwe kwa makini suala hilo ili tuweze kuwaengaenga
na kuwavutia wawekezaji waweze kuja zaidi nchini kwetu.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa niaba ya Kamati ya Fedha, Biashara
na Kilimo, namtakia mafanikio mema Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango katika
utekelezaji wa bajeti yake ya mwaka 2020/2021 kwa Wizara hii na nawaomba
Waheshimiwa Wajumbe waichangie, waulize, wahoji, wakosoe na hatimae waipitishe
bajeti hii ili kumpa fursa Mheshimiwa Waziri kutekeleza kwa ufanisi yale yote
aliyojipangia kwa mwaka ujao wa fedha.
Mheshimiwa
Spika,
Kabla sijamaliza hotuba yangu, nitakuwa
mwizi wa shukurani kama sitompongeza kwa mara nyengine tena Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein kwa fikra na muono
wake wa mbali wa kuendeleza kivitendo azma ya Muasisi wa Mapinduzi yetu
Marehemu Mzee Abeid Amani Karume kwa kufanya ujenzi mpya wa Mji wa kisasa
katika eneo la Michenzani ambao ulianza mapema katika miaka ya 70.
Mheshimiwa
Spika,
Sote ni mashahidi kwamba eneo la
Michenzani hivi sasa limebadilika na tunategemea mabadiliko makubwa mara tu
baada ya kumalizika ujenzi wa miradi ya maduka ya kisasa (shopping mall),
maegesho ya magari pamoja na mradi wa maduka wa kisonge. Kutokana na muone wake
Mheshimiwa Rais ambao unatekelezwa kivitendo na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii
(ZSSF), nimatumaini yetu makubwa tuombe uhai kuiona Michenzani mpya na ya
kisasa. Maendeleo ya mfano ya aina hiyo yatatoa dira na sura mpya kwa mji wetu.
Mheshimiwa
Spika,
Mwisho lakini sio mwisho kabisa, kwa
niaba ya Kamati yangu ya Kudumu ya Fedha, Biashara na Kilimo pamoja na Makatibu
wetu tunachukua fursa hii adhimu kuomba radhi kama kutakuwa na kusoro zozote za
kiutendaji au vyenginevyo zimejitokeza kwa Waheshimiwa na watendaji wote ambao
kwa mujibu wa Kanuni za Baraza la Wawakilishi (Toleo la 2016) Taasisi zao zinasimamiwa
na Kamati yetu zilizomo katikai Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Biashara
na Viwanda pamoja na Wizara ya kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi. Tunawaeleza
kwamba hatukuwa na nia ya kuwakwaza isipokuwa michango na ushauri tuliyoitoa
ililenga katika kuisimamia Serikali ili iweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo
kwa lengo la kuwatumikia wananchi wetu kwa maendeleo na ustawi wa nchi yetu.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa
kumalizia Hotuba yangu naomba kuchukua fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Dimani kwa kuendelea
kuniamini nikiwa Mwakilishi waliyonichagua niingie ndani ya Baraza hili tukufu
kuwawakilisha. Maagizo, maswali, hoja za kupatiwa ufafanuzi pamoja na maelekezo
waliyokuwa wakinipatia, nimejitahidi kuyawasilisha kadiri ya uwezo wangu na
mafanikio mengi tumeyapata katika sekta nyingi hususan elimu, afya, maji,
umeme, maendeleo katika uvuvi na miundombinu ya barabara. Tunamshukuru sana
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na Serikali kwa
ujumla kwa ushirikiano waliotupa katika ustawi na maendeleo ya Wananchi wa
jimbo la Dimani. Tumeahidiwa na tumeanza kuyaona mengi mazuri na makubwa
yameanza kuonekana.
Mheshimiwa
Spika,
Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja
na naomba kuwasilisha.
Ahsante sana,
Mhe. Dkt. Mwinyihaji Makame,
Mwenyekiti,
Kamati ya Kudumu ya Fedha, Biashara na Kilimo,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment