Habari za Punde

VIONGOZI NA WALIMU WAKUU WA VYUO VYA QURAN WAMETAKIWA KUFUATA MAELEKEZO YA WATAALAMU WA AFYA

Katibu wa Mufti  Zanzibar Shekh Khalid Ali Mfaume akitoa maelekezo kwa Walimu Wakuu wa vyuo vya Quran na Viongozi wa Taasisi za kidini wa Wilaya ya Mjini, Ofisini kwake Mazizini, baada ya vyuo vya Quran na Madrasa kufunguliwa .
Mkuu wa Fatwa wa Ofisi ya Mufti Zanzibar Shekh Nouman Jongo akitoa nasaha kwa Walimu Wakuu wa vyuo vya Quran  na Viongozi wa Taasisi za kidini wa Wilaya ya Mjini huko katika  Ukumbi wa Ofisi ya Mufti Mazizini.
 Kiongozi wa Jumuiya ya kuhifadhisha Quran Zanzibar Maalim Suleiman Omar Baramia akipokea Mashine ya Printa  kutoka kwa Katibu wa Mufti Zanzibar Shekh Khalid Ali Mfaume ili isaidie  kazi zao, huko katika Ukumbi wa Ofisi ya Mufti Mazizini Unguja  
Baadhi ya Walimu  Wakuu wa Vyuo vya Quran na Viongozi wa Taasisi za kidini wa Wilaya ya Mjini Unguja wakifuatilia  nasaha zilizokuwa zikitolewa na Maafisa Waandamizi wa Ofisi ya Mufti Zanzibar, Ofisini kwao Mazizini Unguja .
  
 PICHA ZOTE NA YUSSUF SIMAI MAELEZO ZANZIBAR .

Na Khadija Khamis –Maelezo Zanzibar

Katibu wa Mufti  Zanzibar Shekh Khalid Ali Mfaume  amewataka Viongozi na Walimu Wakuu wa Vyuo vya Quran kufuata maelekezo ya Wataalamu wa Afya ili kuepukana na maambukizi ya maradhi ya Corona baada ya kufunguliwa Vyuo vya Quran  .

Aliyasema hayo Ofisini kwake Mazizini wakati akizungumza na Walimu Wakuu wa vyuo vya Quran na Viongozi wa Taasisi za kidini wa Wilaya ya Mjini

Amesema si vyema Walimu  na Viongozi wa vyuo vya Quran kupuuza  maelekezo  ya wataalamu wa afya kwani Corona bado ipo ingawa maambukizi yamepungua kwa kiasi kikubwa .

Alifahamisha kuwa madrasa nyingi za Zanzibar hazina nafasi ya kutosha kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi katika  madarasa ya kusomea hali inayoweza kuchangia kutokea maambukizi ya maradhi ya Corona .

Amewataka  Viongozi wa Vyuo vya Quran  kuweka vitakasa mikono au maji na sabuni  ili wanafunzi wanapoingia na kutoka waweze kunawa pamoja na kuandaa utaratibu mzuri wa kukaa wakati wa masomo yao .

Alieleza kuwa Ofisi ya Mufti ililazimika kuchelewa kufungua Vyuo vya Qurani  ili kuangalia mwenendo mzima wa maradhi ya Corona ambayo yanaambukiza kwa haraka hasa panapo kuwa na mkusanyiko wa watu wengi .

Katibu wa Mufti aliwashauri Viongozi wa Vyuo kuwa na subra  linapotokezea tatizo ni vyema  Waislamu kukaa pamoja na kulitafutia ufumbuzi kwa pamoja .

Mkuu wa Fatwa kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar Shekh Nouman Jongo aliwataka viongozi wa dini kufuata maadili ya kazi zao kwani ni sehemu ya Wazazi na Walezi  wa Watoto.

‘Inasikitisha na inatia aibu kwa  Mwalimu wa Madrasa kufanya vitendo vya udhalilishaji kwa wanafunzi wake,”alisema  Shekh Nouman Jongo.

Amesema vitendo hivyo vinaondosha heshima ya Walimu na  Viongozi wa Dini ya Kiislamu na kuwajengea hofu Wazazi wanaopeleka Watoto wao Vyuoni.

Aliwashauri Walimu na Viongozi hao kuwa kigezo cha vitendo vyema ili kujenga imani katika jamii .

Katika Mkutano huo Ofisi ya Mufti imetoa Printa sabini kwa Madrasa mbali mbali pamoja na Misahafu inayotarajiwa kusambazwa Zanzibar nzima .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.