Habari za Punde

Mgombea Amewataka Wanachama wa CCM Kuwachagua Viongozi Bora Katika Chaguzi za Chama Zinazoanza Kesho Kwa Nafasi ya Ubunge ,Uwakilishi na Udiwani -Dkt. Mwinyi

Mgombea Urais wa Zanzibar CCM Mhe.Dkt. Hussein Mwinyi akisisitiza jambo wakati wa mkutano wake wa mapokezi na kutambulisha katika viwanja vya Tibirinzi Chakechake Pemba.

Mgombea wa Nafasi hiyo ameahidi kusimamia maslahi ya Zanzibar katika Muungano wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na kusimaamia maslahi ya Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na Jumuiya za Kimataifa kwa ajili ya kuleta maendeleo.

Mgombea huyo alisisitiza haja ya kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi wa mwaka huu na kueleza kuwa ushindi wa mwaka uwe ushindi mkubwa na usiwe ushindi mwembamba ambao utaleta malalamiko na kueleza kwamba kutokana na mapokezi hayo hana wasi wasi kuwa ushindi utakuwa wa kishindo.

Alisema kuwa ushindi huo utapelekea kuunda Serikali itakayokuwa na maslahi kwa wananchi wote huku akiwahakikishia kuwa Serikali atakayoiunda itawatumikia wananchi wote.

“Yajayo yanafurahisha naahidi kwamba tutaboresha maisha ya Wazanzibari....hisani hulipwa kwa hisani na hivyo na mimi naahidi hisani ya kuwatumikia wananchi ”,alisema Dk. Hussein Mwinyi.

Aidha, alipongeza risala na kusema kuwa salamu amezipokea huku akitoa shukurani na pongezi kwa mapokezi aliyoyapata kisiwani humo.

Alisisitiza haja ya kuwachagua viongozi bora katika chaguzi za chama hicho zinazoanza kesho zikiwemo nafasi za Ubunge, Uwakilishi na Udiwani  ili iwe rahisi kuyatekeleza yale yanayoahidiwa na Chama hicho.

Dk. Hussein Mwinyi aliwathibitishia wananchi kwamba yeye hajamtuma mtu hata mmoja ili agombee katika chama hicho kwa azma ya kuja kumteuwa kuwa Waziri na kusisitiza kwamba kila mmoja apambane na hali yake.


Katika hatua nyingine, Mgombe huyo wa urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, alisema kama atapata ridhaa ya kuiongoza Zanzibar, atafanyakazi kwa maslahi ya watu wote na kamwe hatowavumilia wala rushwa, wazembe na wasiowajibika.

Alisema kama wapo watendaji wa aina hiyo na hawamjui yeye utendaji wake, basi watamjua muda mfupi tu baada ya kuwa rais wa Zanzibar, baada ya uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.

“Nitafanya kazi kwa maslahi ya watu wote, nitahakikisha watu wote wanafanya kazi ipasavyo, kwa dhamira ya kuwatumikia Wazanzibari wote na sio vyenginevyo tena bila ya ubaguzi”, alisema.

Akizungumzia suala la amani na utulivu wa nchi, Dk. Mwinyi alisema kuwa atahakikisha amani iliyopo Zanzibar itaendelea kudumu hivyo, aliwataka wananchi kudumisha umoja huku akiamini kuwa ndio silaha pekee ya kuwaletea maendeleo.

“Umoja wetu tutauenzi, tutaudumisha na hata katika masuala ya ajira nitahakikisha kwamba hakutakuwa na ubaguzi…..,”alisema.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Mabodi alieleza hatua zilizochukuliwa na chama hicho kuwapata wagombea Urais na hatimae kumpata kinara wa kupeperusha bendera kwa tiketi ya CCM huku akiwapongeza wanaCCM na wananchi wa Pemba kwa mapokezi makubwa.

Nao wanaCCM, waliokuwa wagombea nafasi ya Urais kwa tiketi ya CCM na kuingia tano bora walitoa maneno yao ya shukurani huku wakimuahidi Dk. Hussein Mwinyi kuwa watakuwa nae bega kwa bega na kuwataka wanaCCM na wananchi kuendelea kumuunga mkono pamoja na kukiunga mkono chama hicho.

Katika salamu za WanaCCM wa Mikoa miwili ya Pemba kwa mgombea Urais wa Zanzibar Dk. Hussein Mwinyi walieleza kuwa chama hicho kimepata nahodha mweliedi, mahiri, mzoefu, mchapa kazi na asiyechoka wala kuogopa anaeelewa mazingira ya pepo zote za bahari asiyechoka wala kukata tamaa.

Waliongeza kuwa wanaamini kuwa mgombea huyo atawavusha salama kwa malezi aliyolelewa yeye ni mtoto mwema na atawapeleka wanakotaka kwenye maendeleo endelevu ya nchi.

“Karibu Pemba kwa WanaCCM wenzako tunakukubali, tunakupenda, tunakuthamini, tunakutaka, tumekuchagua na tunakuahidi tutakupa kura za kutosha ili uiongoze nchi yetu, Mhe. Mgombea ondoa hofu Pemba ya jana sio ya leo” walieleza wana CCM hao.

Aidha, walitumia fursa hiyo kumpongeza Mwenyekiti wa CCM Taifa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli na Makamo Mwenyekiti wa chama hicho kwa upande wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein kwa kuongoza vyema mchakato wa kumpata mgombea Urais wa Tanzania na Rais wa Zanzibar.

Nao waliokuwa wanachama wa vyama vya upinzani waliojiunga na CCM, walieleza azma yao ya kumuunga mkono Dk. Mwinyi pamoja na kuiunga mkono CCM ili ishinde uchaguzi ujao kwa kishindo.

Mapema ndege ya Shirika la ndege la “Pression Air” ilituwa katika kiwanja cha ndege cha Pemba, mnamo majira ya saa 4:11 asubuhi ambayo ilimchukua mgombea huyo ambaye alipokelewa kwa vifijo na nderemo kutoka kwa Wanachama na wapenzi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) pamoja na wananchi mbali mbali waliokuwa na shauku kubwa ya kumpokea Mgombea wao wa Urais wa Zanzibar kupitia Chama hicho Dk. Hussein Ali Mwinyi.

Mamia ya wanaCCM walifurika katika kiwanja hicho kwa ajili ya kumpokea Mgombea huyo akitokea Unguja , huku rangi na kijani kibichi na njano kavu ikitawala ambayo ni sare ya Chama hicho kiwanjani hapo.

Bendi ya Chipukizi pamoja na ngoma nyengine za kienyeji zilitowa burudani ya muruwa katika Kiwanja hicho, ikiwa ni ishara ya furaha ya mapokezi ya mgombea Urais wa  Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dk. Hussein Mwinyi.

Pamoja na mapokezi hayo, katika kiwanja cha Ndege cha Karume Pemba wananchi wakiwemo wanachama , wapenzi wa Chama hicho walipata fursa ya kujipanga kando kando ya bara bara kwa ajili ya kumpokea mgombea huyo baada ya kufika Kisiwani Pemba kwa utambulisho.

Wananchi na WanaCCM hao walijipanga barabarani kutoka kiwanja cha ndege hadi Kiwanja cha kufurahishia watoto Tibirinzi nje kidogo ya mji wa Chake Chake Pemba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.