Na Mwandishi Wetu,
Dodoma
Katika jitihada za
kuhakikisha kuwa thamani ya ngozi inaongezeka, Wizara ya Mifugo na Uvuvi mpaka sasa imetoa mafunzo kwa wachunaji wa ngozi
za wanyama takriban 735 nchini.
Hayo yalisemwa na Mkurugenzi
Msaidizi wa Mazao ya Mifugo, Usalama wa Chakula na Lishe, Gabriel Bura katika
kikao cha Wadau wa Mfuko wa Maendeleo ya Mifugo (LDF) cha kutathimini athari za
ugonjwa wa Korona katika tasnia ya ngozi kilichofanyika jijini Dodoma Julai 14,
2020.
Akitoa ufafanuzi kuhusu
hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Wizara katika kuongeza thamani ya zao hilo
la ngozi, Bura alisema kuwa mafunzo hayo ya wachunaji ngozi yametolewa katika
Mikoa ya Kilimanjaro, Manyara, Arusha, Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Morogoro na
Kagera, huku akiongeza kuwa tayari mchakato wa kutoa leseni kwenye mikoa hiyo
umeshaanza.
“Pia tumeanza kugawa
visu vinavyotakiwa kitaalam kwa ajili ya kazi ya uchunaji katika mikoa ya
Kilimanjaro, Arusha na Manyara na mchakato wa kuhakikisha vinafika katika kanda
zote tulizotoa mafunzo unaendelea,”alisema Bura
Aliongeza kuwa hatua inayosubiriwa hivi sasa ni Waziri
wa Mifugo na Uvuvi kusaini nyaraka za uteuzi wa wakaguzi wa ngozi
waliopatikana kutoka kwenye Halmashauri 113
ambao tayari wameshapitishwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali na mara
baada ya taratibu kukamilika wataalam hao watakuwa na jukumu la kuhakikisha
wanasimamia ubora wa ngozi kama walivyoainishwa kwenye sheria namba 18 ya
masuala ya Ngozi.
Awali, akiongea wakati
wa kufungua kikao hicho, Mkurugenzi wa Masoko na Uzalishaji kutoka Wizara ya
Mifugo na Uvuvi, Dkt. Felix Nandonde alibainisha kuwa kufuatia ugonjwa wa
Korona, hivi sasa ngozi inayozalishwa hapa nchini haiendi nje ya nchi na hata
kama inaenda sio kwa kiwango kile cha mwanzo.
“katika kikao hiki
mbali na kujadili matumizi ya fedha pia kitumike kujadili mbinu za kuikwamua
tasnia hii ya ngozi kutoka kwenye hali iliyopo kwa sababu mpaka sasa nchi yetu
inaagiza zaidi ya pea milioni 52 za viatu huku uwezo wetu wa kuzalisha viatu
ukiwa ni milioni 1.2 tu kwa mwaka,”
Alisisitiza Dkt. Nandonde.
Naye Mkurugenzi wa
Taasisi ya Teknolojia Dar-es-salaam (DIT)
Tawi la Mwanza, Dkt. Albert Mmari alisema kuwa taasisi yake ilishaanza
kuchukua hatua kadhaa za kuongeza thamani kwenye tasnia ya ngozi ikiwemo
kuongeza mashine za mafunzo ya kutengenezea viatu ambapo mpaka sasa zipo 50
ukilinganisha na 25 zilizokuwepo hapo awali.
“Kupitia kikao hiki
ninapenda kuwataarifu kuwa taasisi yetu kupitia benki ya dunia imepata zaidi ya
shilingi bilioni 37 ambazo zitatumika kwenye mradi wa miaka 5 ya kuboresha
miundombinu ya chuo ikiwemo kununua
mashine za kisasa za kufundishia, studio za kubuni mitindo mipya ya viatu na
bidhaa nyingine zitokanazo na ngozi, kujenga madarasa ambapo mara baada ya kukamilika
kwa madarasa hayo yatakuwa na uwezo wa kubeba wanafunzi zaidi ya 1000”
Alifafanua Dkt. Mmari.
Wadau waliohudhuria
kikao hicho walitoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda na Biashara,
Ofisi ya Rais-TAMISEMI na Taasisi ya
Teknolojia Dar-es-salaam(DIT) tawi la
Mwanza.
No comments:
Post a Comment