Kaimu Mkurugenzi wa Uvuvi (WMUV), Ezra Mutagwaba (kushoto) akiongea katika Mkutano wa Wadau kuhusu Mjadala wa Viwango vya Mazao ya Dagaa na Mwani uliofanyika jijini Dar es Salaam leo Agosti 24, 2020. Katikati ni Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah na Kulia ni Mratibu wa Mradi wa SWIOFish, Daniel Nkondola.
Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), Dkt. Rashid Tamatamah(katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa Uvuvi muda mfupi baada ya kufungua Mkutano wa Wadau kuhusu mjadala wa viwango vya mazao ya Dagaa na Mwani uliofanyika jijini Dar es Salaam leo Agosti 24, 2020. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Uvuvi(WMUV), Ezra Mutagwaba. Kushoto ni Mratibu wa Mradi wa SWIOFish, Daniel Nkondola.
Na Mbaraka Kambona,
Serikali imesema ipo katika mchakato wa
kutengeneza viwango vya kitaifa vya ubora na usalama wa mazao ya Mwani na Dagaa
ili kuyapa mazao hayo fursa pana ya masoko ya uhakika ndani na nje ya nchi.
Hayo yalisemwa na
Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Rashid Tamatamah alipokuwa
akifungua mkutano wa Wadau kuhusu mjadala wa viwango vya mazao ya Dagaa na
Mwani uliofanyika jijini Dar es Salaam Agosti 24, 2020.
Dkt. Tamatamah alisema
kuwa kutengenezwa na kuanzishwa kwa viwango vya kitaifa vya ubora na usalama wa
mazao hayo ya uvuvi kutaimarisha na kukuza soko la kitaifa na kimataifa la
bidhaa zinazotokana na mazao hayo ya uvuvi.
“Mazao ya Dagaa na
Mwani kwa muda mrefu yamekuwa hayana viwango vya ubora jambo ambalo limekuwa
likifanya bidhaa hizo kutokutambulika katika soko la kimataifa ndio maana sasa
serikali imeamua kutengeneza viwango vya ubora vya mazao ya uvuvi hasa Daagaa
na Mwani ili yaweze kupata masoko yenye uhakika ndani na nje ya nchi,”alisema
Dkt. Tamatamah
Alisema kuwa uvuvi wa
dagaa pamoja na ukulima wa mwani ni muhimu kwa uchumi wa jamii inayoishi Pwani
na taifa kwa ujumla huku akisema kuwa kilimo cha mwani peke yake kinawahusisha
takribani wakulima elfu tatu (3000) wengi wao wakiwa ni wanawake.
“Kwa mwaka 2019/2020
kiasi cha tani 1449 za Mwani zilizalishwa na kati ya hizo, asilimia 10 zilitumika hapa
nchini katika kutengeneza bidhaa mbalimbali zikiwemo sabuni na aslimia 90
zilisafirishwa kwenda nje ya nchi zikiwemo nchi za China, Marekani, Canada,
Uingereza, Denmark na Ufaransa,”alifafanua Dkt. Tamatamah
“Kwa upande wa
Zanzibar, uzalishaji wa Mwani umefikia takriban tani 35000 na ndio bidhaa ya
pili inayosafirishwa kwa wingi kwenda nje ya nchi,”aliongeza
Dkt. Tamatamah
aliendelea kueleza kuwa kutokana na umuhimu huo ni dhahiri kwamba kuna haja ya
kuwepo kwa viwango vya ubora na usalama ili wafanyabiashara waweze kuyafikia
masoko mbalimbali duniani.
“ Kupitia mradi wa
SWIOFish ulio chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na Shirika la
Viwango Tanzania (TBS) wameweza kuandaa viwango viwili ambavyo ni TBS/AFDC 23
kwa ajili ya unga wa Dagaa na TBS/ AFDC (5714)
kwa ajili ya Mwani mkavu,”alibainisha Dkt. Tamatamah
Naye Mkulima wa Mwani,
Wilayani Bagamoyo, Mzee Machao Ally Jingalao alisema katika mkutano huo kuwa
hatua hiyo ya Serikali ya kutengeneza viwango vya ubora kwa ajili ya mazao hayo
ya uvuvi ni hatua nzuri ya kuelekea uchumi wa viwanda.
“Naiomba serikali
iongeze nguvu katika kuimarisha biashara hii ya mazao ya uvuvi kwani
ikisimamiwa vizuri itasaidia sana kuiongezea mapato nchi na kuinua uchumi wa
mtu mmoja mmoja,”alisema Jingalao
Meneja wa Kampuni ya
Uwekezaji katika zao la Mwani, Mariculture, Roger Valle Morre aliiomba Serikali
kulinda wawekezaji katika zao la Mwani dhidi ya watu wanaojiingiza katika
biashara hiyo bila kuwa na vibali.
No comments:
Post a Comment