Habari za Punde

Siku ya kimataifa ya Vijana duniani yaadhimishwa kisiwani Pemba


RAIYE MKUBWA  - WVUSM – PEMBA.

Kama inavyoeleweka kwamba kila ifikapo tarehe 12/08 ya kila mwaka ni siku ya kimataifa ya Vijana, siku ambayo mataifa mbali mbali ulimwenguni huadhimisha kwa lengo la kutambua na kutathmini juhudi na michango inayotolewa na vijana katika maendeleo ya jamii, taifa na Dunia kwa ujumla.

Umoja wa Vijana wa CCM wakishirikiana na vijana wa baraza la vijana wilaya ya chake chake wameadhimisha siku ya wiki ya vijana duniani kwa kujitolea kufanya usafi katika hospitali ya Rufaa ya Changuo iliyopo Vitongoji wilaya ya Chake chake Mkoa wa kusini Pemba.

Akizungumza na vijana hao Mgeni Rasmi katika maadhimisho hayo Ndg. Kassim Ali Omar amewataka Vijana kuitumia fursa ya wiki ya vijana kwa kuitilia maanani kaulimbiu ambayo inalenga kudumisha amani na utulivu hususan katika kipindi hiki cha matayarisho ya uchaguzi mkuu wa taifa.

Afisa kassim, ametoa wito kwa vijana kuwa na moyo wa kujiendeleza kielimu na kushiriki kikamilifu katika kutafuta mafunzo ya vitu mbali mbali ili kufanya mambo kwa uweledi wa hali ya juu.

Aidha, amewataka Vijana kusoma elimu ya nadharia na vitendo  ili kufanya ujasiriamali hivyo  kuweza kujiajiri wenyewe kutokana na ujuzi wataoupata kwalengo la  kukuza mfuko wa mapato yao pamoja na maendeleo ya  taifa kwa ujumla.

‘’Jambo la msingi tukitia maanani siku hii tujitahidi kujiendeleza kielimu  kusoma elimu ya nadharia na vitendo ambayo ndani yake inaingiza masuala ya ujasiriamali na kuwapelekea vijana kujiajiri wenyewe’’. Alisema

Pia amewapongeza sana vijana kwa kujielewa na kujitokeza kwa wingi katika utiaji nia na uchukuaji fomu za kugombania uongozi wa nafasi mbali mbali kwani kumeonesha muamko mkubwa uliopatikana kwa Vijana ukilinganisha na miaka mengine ya uchaguzi na kuwaomba vijana baada ya uchaguzi wayapokee matokeo kwa njia ya amani

Afisa huyo, amewataka vijana waitumie nafasi hii kuwashawishi vijana wengine waweze kufanya matendo mazuri ili kuepukana na vishawishi kama utumiaji wa madawa ya kulevywa na kuvuta bangi waepukane nayo kwani yanavunja heshma katika jamii

‘’Vijana tuna nafasi kubwa katika jamii katika suala la kushawishi na kuhamasisha wengine waweze kufuata matendo mema, kwani kuna mambo mengi ya madawa tusaidie wenzetu waepukanenayo kwani hayo’yanavunja heshma na hadhi ya jamii’ alisema

Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Chakechake ndg. Ashloo Masoud Khamis amempongeza Mhe. Raisi wa Zanzibar na Mwenyekiti Wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohammed Sheni Pamoja na Dkt John Magufuli kwa Kuwathamini vijana na kuwapa nafasi katika uongozi na kuwashirikisha katika mambo mbali mbali ndani ya serikali.

 Vile vile, Ashloo amewaasa vijana kufanya mambo mazuri katika siku yao kwa kufanya kazi nzuri hata baada ya maadhimisho haya ili kuionesha jamii inayoiangalia ni kitu gani wanafanya.


‘’Nianze kuwaasa vijana mufanye kazi nzuri kwa hili tulilolikusudia kwani jamii inatuangalia na tunajuilikana nini tunafanya lakini pia tuwahongere Raisi wa Serikali zote mbili kwa kwa kuwapenda Vijana na kuwapa kipaombele’’ alieleza
Aidha, katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM wilaya ya Chake Chake Ndg Thamra Bakari Yusuf, amewaomba Vijana kuwa mstari wa mbele katika kupambana na mambo maovu yanayofanywa na vijana wengine ili kuikomboa jamii na mambo machafu, na kuwaelimisha kwamba Zanzibar yetu ni Moja na inahitaji amani na utulivu na sio machafuko.

Akitoa neno la shukrani Daktari dhamana wa Hospitali ya Changuo, Dkt. Sharifu Khatibu amewapongez Vijana waliotumia Muda wao wa siku ya Vijana kwa kuichagua Hospitali ya Changuo kuifanyia Usafi ingawa kuna shughuli nyingi za kufanya katika jamii lakini wakaamua kuwagusa wagonjwa katika Hospitali hii.

‘………….. niwashukuru sana kwa kutumia muda wenu kuja kufanya usafi katika hospitali hii na kuacha maeneo mengine kama mashuleni na kuona umuhimu wa kuwagusa wagojwa….’’ Alieleza
Afisa Vijana wilaya ya Chake chake Bi Stara Khamis Salim amewaomba Vijana kujua kwamba hii ni siku yao adhimu hivyo kuitumia kwa kuwa pamoja na kudumisha amani na utulivu kama walivyoamua kuungana kwa pamoja vijana wote ndani ya wilaya yao kufanya kitu ambacho ni cha kuonekana wameitumikia vipi siku ya vijana duniani.

Kwa upande wao Vijana wameipokea vizuri siku ya vijana na kutoa wito kwa vijana wengine kwamba wawe na moyo wa kujitolea ili kuleta maendeleo katika jamii yao.

Matron wa Vijana wilaya ya Chake chake Ndg. Zuhura Salim Mahmoud ameeleza kuwa vijana wamehamasika na siku hii kwani wamepata kujitoa kwa wingi na kutimiza hamu yao waliokuwa wakiitamani kwa muda mrefu hivyo wameweza kutekeleza moja kati ya malengo yao.

Pia amewaomba vijana wengine waweze kujiunga kwenye vikundi vyao vya michezo na sanaa ili waweze kuhamasika na kujichangamsha pia kusogeza mbele maendeleo ya chama kwani wanapojitolea kinachoonekana ni Vijana na Chama cha Mapinduzi.

‘Vijana wanaweza kuhamasika kupitia makundi yetu ya sanaa na ya kimaendeleo kama haya ya kujitolea ndio nafasi yetu ya kuonekana vijana….’’

Hata hivyo, Hamadi Khamis Ali Katibu wa Vijana tawi la vitongoji Ametoa wito kwa Vijana wengine ambao hawakushiriki katika zoezi hili kuwa na moyo wa kujitolea na kushiriki katika matukio ya kijamii kwani vijana ndio nguvu ya taifa, na kuwaomba vijana wenzake wadumishe amani na utulivu.

Juma Jongo Juma ambaye Ni mjumbe wa baraza la vijana tawi la vitongoji amewataka vijana wengine kujiunga na Umoja huo kwani watapata faida tofautitofauti katika zoezi hilo, kama vile kujichangamsha mwili hivo kuboresha afya zao, kuboresha usafi mazingira ya Hospital  na pia wameweza kujitangaza ndani na nje ya nchi kwani hii ni siku ya kimataifa.

‘……wenyewe tumepata kujichangamsha kiafya, kuboresha usafi kwenye hospitali zetu pia kutambulikana vijana kuwepo ndani ya nchi…….’’

Kwa mwaka huu wa 2020 kauli mbiu ya siku ya kimataifa ya vijana ni ‘youth engagement for global action’ ujumbe ambao unalengo la kuimarisha na ushirikishwaji wa vijana wenye tija katika ngazi ya kijamii, kitaifa na kimataifa.

Kwa upande wa Zanzibar maadhimisho haya yanafanyika wakati taifa likiwa katika kipindi cha matayarisho ya uchaguzi Mkuu wa Zanzibar, ambapo vijana ni sehemu kubwa ya wananchi wanaotarajiwa kushiriki katika uchaguzi huo.

Hivyo, kutokana na kauli mbiu ya 2020 na hali ya Taifa kukabiliwa na kipindi muhimu cha uchaguzi Mkuu, Maadhimisho ya siku ya kimataifa ya Vijana kwa Zanzibar yamebeba kauli mbiu isemayo ‘ KIJANA! SHIRIKI UCHAGUZI, DUMISHA AMANI’’ kwa ajili ya kuhamasisha vijana kushiriki kikamilifu katika hatua zote za uchaguzi kwa njia ya amani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.