Habari za Punde

Dr. Mwinyi Awapongeza Wanafunzi wa Kidatu cha Sita Zanzibar.

Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM Dr. Hussein Ali Hassan Mwinyi akipatia zawadi ya ngao Mwanafunzi Abdulrahman Abdulla wa Skuli ya Biashara Zanzibar baada ya kupata Daraja la Kwanza katika ufaulu wa Mitihani ya Kidato cha Sita Mwaka 2020 akiwa pia Mshindi wa Kwanza kwa jumla Zanzibar {Zanzibar one} hapo Hoteli ya Verde Mtoni.
Baadhi ya Wanafunzi waliomaliza masomo ya Kidatu cha Sita na kufaulu Madaraja ya Kwanza, Pili na Tatu Mwaka 2020 wakiwa katika sherehe ya kupongezwa hapo Hoteli ya Verde pembezoni mwa Jiji la Zanzibar.
Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Mh. Ayoub Mohamed Mahomoud akitoa Mada ya Msomi wa Kimapinduzi na Maendeleo ya Taifa kwa wasomi waliomaliza Kidato cha Sita hapo Verde.
Mratibu wa Elimu Ajira na Mafunzo Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar Nd. Khamis Salum Abdi akitoa maelezo kwenye sherehe za kuwapongeza Wanafunzi waliomaliza Mitihani ya Kidato cha Sita na kufaulu madaraja mbali mbali.
Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM Mhe. Dr. Hussein Mwinyi akiwa katika picha ya pamoja na Wanafunzi watatu bora wa Daraja la Kwanza Mwaka huu waliomaliza Mitihani ya Kidato cha Sita 2020.Kulia ya Dr. Hussein ni Mwanafunzi Muslih Hamad wa Skuli ya Sekondari ya Lumumba, Kushoto ya Dr. Hussein ni Mwanafunzi Abdulrahman Abdullah wa Skuli ya Biashara na Mwanafunzi Rashid Said wa Skuli ya Jang’ombe.
Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM Dr. Hussein Mwinyi Kati kati akiwa pamoja na Wanafunzi bora waliofaului vyema mitihani ya kidato cha Sita pamoja na Viongozi wa CCM na Jumua zake mara baada ya kumaliza hafla ya kuwapongeza.
Picha na – OMPR – ZNZ.
Na.Othman Khamis                                                                                                           
Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Mapinduzi Dr. Hussein Ali Mwinyi alisema miundombinu imara katika Sekta ya Elimu ndio njia pekee inayoweza kuzalisha Wasomi Wazalendo wanaokuwa nguzo imara katika kuimarisha Uchumi wa Taifa lolote.
Alisema miundombinu hiyo ambayo huenda sambamba na kuwa na Mitaala na Mazingira bora, Takwimu, Maslahi ya Walimu pamoja na gharama za kuhudmia Elimu ni mambo ya msingi yanayotosheleza haja ya kuwa na wasomi wengi ambao ndio nguzo sahihi ya tegemeo la Taifa katika Maendeleo.
Dr. Hussein Ali Mwinyi alitoa kauli hiyo wakati wa sherehe za kuwapongeza Wanafunzi wa Kidato cha Sita waliofaulu vyema Mitihani yao ya Mwaka 2020 ufaulu utakaowawezesha kuendelea na masomo yao katika ngazi mbali ya Elimu ya Juu hafla iliyofanyika katika Hoteli ya Verde Mtoni pembezoni mwa Jiji la Zanzibar.
Alisema Vijana ndio tegemeo kubwa la  Taifa hivyo ni lazima mazingira yao ya kupata Elimu kwa mujibu wa mategemeo ya fani tofauti yaendelezwe kwa nguvu zote ili kukidhi matihaji husika yanayojitokeza katika kuendesha Nchi.
Mgombe huyo wa Urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Mapinduzi aliwapongeza Vijana hao kutokana na Ufaulu wao bora wa Mitihani ya Kidato cha Sita na kuwashauri wachague fani nzuri kipindi hichi ili pale wanapomaliza masomo yao waingie katika soko la Ajira mara moja.
Dr.  Hussein Mwinyi aliwaahidi wasomi na Vijana wote wa Zanzibar kwamba endapo atapewa ridhaa ya kuwatumikia Wanbanchi wa Zanzibar katika nafasi ya Urais ataongeza mkazo Zaidi ya ule atakaoukuta katika kuimarisha Elimu ya Maandalizi, Msingi, Kati na Sekondari ili kuwanyooshea njia ya kuyakabili vyema masomo yao ya vyuo Vikuu hapo baadae.
Akitoa Taarifa Mratibu wa Elimu Ajira na Mafunzo Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar Nd. Khamis Salum Abdi alisema Kitengo hicho kimekuwa na utaratibu wa kuwapongeza Vijana wanaomaliza Masomo ya Kidato cha Sita na kufaulu vyema kwa takriban Mwaka wa Nne tokea Mwaka 2017.
Nd. Khamis alisema wanafunzi Mia Moja waliopata Daraja la Kwanza, 503 Daraja la Pili na 769 Daraja la Tatu tayari wameshajisajili kwenye Kitengo hicho ikionyesha wazi kuongezeka kwa kiwango cha Ufaulu Mwaka huu ikilinganishwa na Miaka ya nyuma.
Alisema mfumo huo wa kujisajili kwa Wanafunzi hao mbali ya kuwaandaa kuimarisha uwezo wao wa Kitaalum katika kupata Wataalamu wa uhakika Serikalini na hata Sekta Binafsi lakini pia kwa njia nyengine hupatiwa mfunzo ya Uzalendo yanayosaidia kuendelea kuipenda Nchi yao.
Mratibu huyo wa Elimu Ajira na Mafunzo wa Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui kwa niaba ya wanataaluma wenzake wamempongeza Dr. Hussein Mwinyi kwa umahiri na uzalendo wake uliomuwezesha kuaminiwa na hatimae kupewa nafasi ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kupitia Marais waliopita wa Muungano.
Katika sherehe hiyo pamoja na mambo mengine Wasomi hao walipata semina ndogo iliyobeba dhana Uzalendo, Maisha ya Chuo Kikuu pamoja na Msomi wa Kimapinduzi na Maendeleo ya Taifa zilizotolewa na Wahadhiri Mh. Angelina Malembeka, Dr. Haroun kutoka Chuo Kikuu cha Taifa {Suza} na Mkuu wa Mkoa Kusini Mh. Ayoub Mohamed Mahmoud.
Akitoa Shukrani kwa niaba ya Wanafuynzi wenzake Mwanafunzi Abdulrahman Abdulla wa Chuo cha Biashara Zanzibar aliyefanikiwa kupata Daraja la Kwanza akiwa Mwanafunzi Bora kwa Mwaka huu Zanzibar {Zanzibar one} alisema mfumo wa Elimu uliopo Nchini ambao unapaswa kuimarishwa Zaidi umemuwezesha Kila Mtoto wa Zanzibar kupataTaaluma  kulingana na uwezo wake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.