Habari za Punde

Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Shein CCM Imewaletea Kiongozi Mchapakazi na Mwenye Uwezo Kuwa Rais wa Zanzibar Ambaye ni Dk. Husseim Ali Hassan Mwinyi.

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar (CCM) ambae pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akiwahutubia Wananchi na Wanachama wa CCM wa Wilaya ya Wete Pemba wakati wa mkutano wa kampeni ya Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CCM Mhe.Dk. Hussein Ali Hassan Mwinyi kumuombea Kura kwa Wananchi wa Pemba na kuwaombea kura Wabunge, Wawakilishi na Madiwani wa CCM katika mkutano huo uliofanyika uwanja wa mpira Gando Wilaya ya Wete Pemba leo 27-9-2020.


MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimewaletea kiongozi mchapakazi  na mwenye uwezo kuwa kuwa Rais wa  Zanzibar ambaye ni Dk Hussein Ali Hassan Mwinyi.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika mkutano wa Kampeni za Chama Cha Mapinduzi (CCM) huko Gando, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba, ambao ulihudhuriwa na maelfu ya wanaCCM.

Alisema sifa za Dk. Mwinyi za nidhamu, uhodari wa kazi, kuwajali watu wote na ubobevu wa uongozi sifa hizo hanazo mgombea mwengine yeyote kwa nafasi yoyote kutoka vyama upinzani.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa, Dk. Mwinyi ni kiongozi anaejali shida za watu na ambaye ameweza kushika nafasi mbali mbali katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

‘’Kazi iliyofanywa na mikutano yote ya CCM na kisha kupatikana kwa mgombea huyo Dk. Hussien Mwinyi haikukosea, maana uchapakazi wake unaonekana  kila pale anapokabidhiwa madaraka,’’alieleza.

Hata hivyo, Rais Dk. Shein ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar alisema kuwa yeye anayajua vyema majukumu ya urais kutokana na ugumu wake, na jinsi anavyomfahamu Dk. Mwinyi, basi anauweza kuifanya kazi hiyo bila ya wasi wasi.

“Urais sio asali kama kila mtu airambe, Urais ni kazi na Dk. Mwinyi kazi hiyo anaiweza”,alisisitiza Dk. Shein.

Aidha, alieleza kuwa, Dk. Mwinyi ndio mgombea pekee ambae anafaa kwa asilimia 100 kuwa rais wa Zanzibar, hasa kwa busara zake na utii wa kazi.

‘’Dk. Mwinyi anafaa kwa asilimia 100 kuwa rais, maana mimi nauwelewa sana na sijaona kiongozi mwengine anaeuweza baada ya mgombea aliyetuliwa na CCM,’’alifafanua.

Hivyo, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi na WanaCCM kumpigia kura Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Mgombea wake Mwenza, Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani wote wa CCM.

Alifahamisha kuwa, dhamira ya CCM kila siku ni kuona wananchi wake wanaishi kwa amani na utulivu, hivyo ili hilo litekelezeke ni kuwapigia kura wagombea wa chama hicho cha CCM.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa Dk. Hussein Mwinyi ndie kiongozio pekee anayegombea nafasi ya Urais wa Zanzibar kuwa Rais wa Zanzibar anaeweza kuyalinda, kuyatetea na kuyadumisha Mapinduzi ya Januari 12, 1964 pamoja na kuutunza Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

“Siku ya tarehe 28, Oktoba mwaka huu, siku hiyo ya kupiga kura ikifika, muhakikishe hamfanyi makosa, na muwapigie kura rais John Pombe Magufuli, Dk. Hussein Mwinyi, wabunge, wawakilishi na madiwani wetu wote,’’alisisitiza.

Nae Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema iwapo wananchi wa Zanzibar watampa ridhaa ya kushika nafasi hiyo, atahakikisha, anasimamia uwajibikaji na watakoshindwa atawawajibisha, ili mafanikio ya kweli yapatikane.

Dk. Mwinyi alisema, hayo ndio kipaumbele chake cha kwanza mara atapomaliza kuapishwa, kwani mambo hayo ni miongoni mwa yanadhoofisha kwa kiasi kikubwa maendeleo ya jamii.

Mgombea huyo wa urais, aliyasema hayo Jimbo la Gando wilaya Wete mkoa wa kaskazini Pemba, alipokuwa akizugumza na mamia ya wanaccm na wananchi wengine, kwenye mkutano wa hadhara wa kampeni wa chama hicho.

Aliongeza kuwa, serikali atakayoiongoza hatopenda hata kidogo kuona ndani yake, mna watendaji wasiopenda kuwajibika, kwani wanakuwa kikwazo kufikia maendeleo yaliokusudiwa.

Alisema kuwa jambo hilo ni adui mkubwa wakufikia maendeleo ya  Zanzibar, na kuendelea kudumaa kwa baadhi ya sekta, jambo ambalo halikubaliki na atalisimamia kwa dhati.

“Mkinichagua kuwa rais wa Zanzibar, pamoja na mambo kadhaa ambayo ntawafanyia, lakini suala la uwajibikaji ndio kipaumbele cha kwanza, na akitokezea mtendaji kushindwa kuwajibika, ntamuwajibisha,’’alisisitiza.

Aidha, Mgombea huyo wa urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM Dk. Hussein Ali Mwinyi, amewaahidi wananchi wa Zanzibar kama akipata ridhaa, atahakikisha anaimarisha miundombinu ya barabara, ili iwe ya kisasa zaidi.

Alisema, bara bara ambazo ataanza nazo kwa kisiwani Pemba, ni ile ya Chake Chake - Wete yenye urefu wa kilomita 21, Finya- Kicha yenye urefu wa kilomita 8.8 na zile ndani ya mji wa Wete zenye urefu wa kilomita 9.

Alisema kuwa, ili Zanzibar ipige hatua kubwa kwenye maendeleo ya sekta ya utalii, viwanda, uvuvi inategemea sana uwepo wa barabara za kisasa, katika maeneo yote ya Unguja na Pemba.

Alisema, ingawa tayari Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein anaemaliza muda wake, ameitekeleza kwa kiwango kikubwa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020 ambapo nay eye ameahidi kuitekeleza vyema ile ya 2020-2025.

“Kila mmoja ni shahidi kuwa, Inali ya CCM ya mwaka 2015/2020 Dk. Shein, ameitekeleza kwa asilimia 100, karibu kila sekta na mimi mkinichagua, nitazidi kuziimarisha na kuendeleza,’’alifafanua.

Pia, Mgombea huyo aliwaahidi wananchi kuwa atawafanyia, ni kupiga vita suala la udhalilishaji pamoja na dawa za kulevya, ambapo alisema matatizo hayo amekuwa akilielezwa kila anapopita katika kapeni zake za urais nazozifanya wakati akiwatembelea wananchi mbali mbali Unguja na Pemba.

Alieleza kuwa, tatizo hilo linamnyima usingizi na ndio maana mara akichaguliwa. atahakikisha anafanya kila mbinu kuona udhalilishaji na dawa za kulevya, zinakuwa historia Zanzibar.

Aidha, mgombea huyo wa urais alisema, kutokana na mengi ambayo aliyafanya rais anayemaliza muda wake, kazi yake itakuwa ndogo mara akiingia madarakani ambapo alieleza kuwa tayari Dk. Shein ameliimarisha zao la karafuu na kusababisha kuvunwa kwa tani 3,321 mwaka 2015 na kufikia tani 8,277 ambazo ni nyingi mno.

Aidha, alisema, eneo jengine ambalo limefanikiwa kwa kiasi kikubwa ni sekta ya elimu , kwa kujengwa skuli za ghorofa za Kizimbani, Limbani na ile Chasasa pamoja na chuo cha amali kilichopo Daya wilaya ya Wete.

Kuhusu kuliimarisha zao la mwani, Dk. Mwinyi alisema, tayari Serikali ya Awamu ya Saba, imeshaanza ujenzi wa kiwanda ya kusarifia mwani, eneo la Chamanangwe sambamba na kuwakabidhi vihori 80  wakulima wa mwani wa Wilaya ya Wete.

‘’Ilani ya CCM ya mwaka 2015/2020, lazima nikiri kuwa ilipata msimamizi Dk. Shein, maana hata sekta ya utalii imeimarika kwa kuongeza watalii  kufikia laki tano kutoka watalii 37,900 mwaka 2015,’’alisisitiza.

Katika hatua nyingine, mgombea huyo wa urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, amewataka wananchi wa Zanzibar kuhakikisha kura zao hawazipotezi, kwa kuvipa vyama ambayo havina muelekeo.

Alisema CCM ndio chama kinachojali maisha ya watu wote wakiwemo wanyonge, wakulima na wakwezi hivyo, dhamira hiyo haiwezi kuendelezwa na kiongozi yeyote, isipokuwa anaetoka CCM.

‘’Tupeni ridhaa sisi wagombea wote wa CCM, ili tuendelee dhamira na ari ya kweli ya kuwatumikia, pasi na kujali maeneo mnayotoka wala rangi, na hii ndio shabaha ya waasisi wa taifa hili,’’alieleza Dk. Mwinyi.

Mapema Naibu Katibu mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi, alisema, ushindi wa CCM hauna shaka, kutokana na kuitekeleza vyema Ilani ya  Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020.

‘’Leo kutoka mjini Wete hadi kijiji cha Gando, unatumia dakika zisizozidi 20, maana barabara imejengwa tena kwa kiwango cha lami, hayo ndio mambo ya CCM,’’alisema Dk. Mabodi.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba Mberwa Hamad Mberwa alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa maendelea makubwa yaliyopelekwa na katika Mkoa huo na Serikali anayoiongoza Dk. Shein.

Nao wagombea Ubunge, Uwakilishi na Udiwani wa Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba walitambulishwa na Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar ambapo walitumia fursa ahiyo kuomba kura na kuwataka wananchi na wanaCCM wote kuwachagua ili wazidi kupeleka maendeleo katika maeneo yao.

Viongozi mbali mbali wa CCM walihudhuria akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Waziri Kiongozi Mstaafu Shamsi Vuai Nahodha pamoja na viongozi wengine wa CCM.

Mkutano huo wa Kampeni ulikwenda sambamba na burudani kadhaa zilizotolewa na wasanii mbali mbali wakiwemo wale wa kizazi kipya pamoja na wagongwe kama vile Bi Fatma Issa.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.