HOTUBA YA MHESHIMIWA
DK. HUSSEIN ALI MWINYI, RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI KATIKA UZINDUZI WA
BARAZA LA KUMI LA WAWAKILISHITAREHE: 11 NOVEMBA, 2020
Mheshimiwa
Zubeir Ali Maulid;
Spika wa Baraza
la Wawakilishi la Zanzibar,
Mheshimiwa Hemed
Suleiman Abdulla;
Makamo wa Pili
wa Rais wa Zanzibar,
Mheshimiwa Omar
Othman Makungu;
Jaji Mkuu wa
Zanzibar,
Rais Mstaafu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi na Mama Siti
Mwinyi,
Mheshimiwa Rais
Mstaafu wa Zanzibar, Dk. Amani Abeid
Amani Karume na Mama Shadya Karume,
Mheshimiwa Rais
Mstaafu wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein na Mama Mwanamwema Shein,
Mheshimiwa
Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mstaafu
Balozi Seif Ali
Iddi na Mama Asha Suleiman Iddi,
Waheshimiwa
Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa
Mabalozi Wadogo mliopo, Zanzibar,
Wawakilishi wa Mashirika mbali mbali ya Kimataifa mliopo,
Waheshimiwa
Viongozi mbali mbali wa Serikali na Vyama vya Siasa,
Ndugu Wageni
Waalikwa,
Ndugu
Wanahabari,
Mabibi na
Mabwana,
Assalam Aleikum.
UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika,
Naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa
rehma kwa kutujaalia uhai na afya njema, na kutuwezesha kukutana katika siku
hii ambayo ina nafasi yake katika historia ya nchi yetu.
Leo tumekutana hapa kuzindua rasmi Baraza la Kumi la
Wawakilishi la Zanzibar ambalo linaambatana na kuanza kwa Awamu ya Nane ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mheshimiwa Spika,
Kabla
sijaendelea na hotuba yangu, nachukua fursa hii kutoa salamu za pole kwa
uongozi na wanachama wa Chama cha ACT Wazalendo, Familia pamoja na Ndugu wa
Marehemu Abubakar Khamis Bakar, aliyekuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi
Mteule wa Jimbo la Pandani.
Tutamkumbuka
Marehemu Abubakar kwa mchango mkubwa alioutoa kwa maendeleo ya Zanzibar katika
nyadhifa zake mbali mbali za uongozi alizowahi kushika likiwemo suala la
maridhiano ya kisiasa yenye lengo la kuleta Umoja wa Kitaifa hapa Zanzibar.
Tunamuomba
Mwenyezi Mungu amsamehe makosa yake na ailaze roho yake mahali Pema Peponi,
Amina. Aidha, tunamuomba Mwenyezi Mungu awape wafiwa wote subira katika kipindi
hiki cha msiba wa mwenzetu
SALAMU ZA
PONGEZI
Mheshimiwa
Spika,
Naomba uniruhusu kwanza nitoe
pongezi zangu nyingi kwako kwa kuchaguliwa kwa kuwa Spika wa Baraza la Wawakilishi.
Kuchaguliwa kwako kwa kura zote ni kielelezo cha Imani kubwa waliyonayo
Waheshimiwa Wajumbe. Umefanya kazi nzuri ya kuliongoza Baraza la 9 na ndio
sababu umeaminiwa kuliongoza Baraza hili la 10. Wahenga wamesema, Chanda chema huvikwa pete!
Ahadi yangu kwako ni kukupa kila aina ya ushirikiano utakaohitaji katika kutekeleza majukumu yako. Mafanikio ya Serikali ya Awamu ya 8 ninayoiongoza yanategemea sana ufanisi wa Baraza la Wawakilishi. Chombo hiki ndio chombo cha uwakilishi wa wananchi. Ndio chombo kilichopewa dhamana ya kuisimamia Serikali. Mimi naamini kuwa Baraza la Wawakilishi imara huzaa Serikali imara.
Mheshimiwa Spika,
Pamoja na salamu za pongezi kwako, niruhusu pia nimpongeze Mheshimiwa Mgeni Hassan Juma kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika. Nakutakieni kila la kheri katika kutekeleza majukumu yenu na katika kuitimiza dhima kubwa mliyopewa.
Kwa hakika, kuchaguliwa kwenu kwa kura zote kuongoza mhimili huu wa dola kunaashiria imani waliyonayo Waheshimiwa wajumbe wa Baraza hili kwenu kutokana na hekima, busara, uadilifu, taaluma na uzoefu mlionao. Hongereni sana. Sisi katika Serikali tuko tayari kushirikiana nanyi katika kuijenga nchi yetu.
Mheshimiwa Spika,
Niwapongeze pia Wawakilishi wote
kwa kuchaguliwa na wananchi kuwawakilisha katika Baraza hili tukufu. Mimi na
ninyi tumeshirikiana katika uchaguzi na kufanya kampeni. Tumewasikia wananchi
wetu na matarajio yao kwetu. Kote nilikopita mimi, na bila ya shaka ninyi,
nimekutana na kiu kubwa ya wananchi wetu ya kutaka kuyafanya maisha yao kuwa
bora zaidi. Wametuchagua kwa sababu tumeahidi kutimiza matarajio hayo. Aidha, Heshima
yetu itatokana na sisi kutimiza matarajio yao. Heshima yetu itatokana na sisi
kutimiza ahadi zetu, maana si tu kwamba ahadi ni deni, bali kutimiza ahadi ni
kulinda heshima. Niwatakie kila la kheri katika kutimiza majukumu yenu.
Niwahakikishie dhamira yangu na ya Serikali nitakayoiunda ni kushirikiana nanyi
katika kufanikisha na kutimiza matarajio ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Spika,
Katika Baraza hili la 10, mbali
na ninyi Wawakilishi wa kuchaguliwa, kwa mamlaka niliyopewa na Katiba ya
Zanzibar ya 1984 toleo la 2020, nimefanya uteuzi pamoja na wengine wa
Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla kuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi na
Makamu wa Pili wa Rais na Mheshimiwa Dkt. Mwinyi Talib Haji kuwa Mwanasheria
Mkuu wa Serikali.
Ninayo furaha kumtambulisha
kwenu Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla kuwa Makamu wangu wa Pili na kiongozi wa
Shughuli za Serikali katika Baraza la Wawakilishi. Ni kiongozi kijana, mwenye
ari na nguvu nyingi za kuwatumikia Wazanzibari. Ni kiongozi msikivu, mwenye
huruma na mchapa kazi hodari. Nakuombeni sana mumpe ushirikiano wenu.
Pamoja naye, ninayo furaha
kumtambulisha kwenu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dkt. Mwinyi Talib Haji. Ni kiongozi mnyenyekevu, muungwana na ni mtu makini sana. Ni msomi
mzuri aliyebobea katika masuala ya sheria. Tumempa jukumu hili atusaidie ndani
ya Serikali na katika Baraza lako Tukufu katika kutekeleza majukumu yake ya
utungaji sheria. Nakuombeni naye mumpe ushirikiano wenu wote.
Mheshimiwa Spika,
Kadhalika, nakipongeza chama
changu, Chama Cha Mapinduzi kwa kupata ushindi mkubwa wa asilimia 76.2 kwa
nafasi ya Urais wa Zanzibar, asilimia 92 ya majimbo kwa nafasi za ujumbe wa
Baraza la Wawakilishi na asilimia 93.6 kwa nafasi za Madiwani. Huu ni ushindi
mkubwa na wa kihistoria ambao haujapata kutokea katika chaguzi zilizopita
Zanzibar katika mfumo wa vyama vingi.
Kwa hakika, kura nyingi
tulizopigiwa na wananchi ni ishara ya matumaini makubwa waliyonayo kwa uongozi
mpya. Ushindi huu mkubwa tulioupata ni ishara ya imani kubwa waliyonayo
wananchi kwa chama chetu na kwangu mimi
binafsi. Hivyo ni wajibu wetu sasa
kukidhi matarajio ya wengi; ambalo ndilo jukumu kubwa lilio mbele yetu.
Mheshimiwa Spika,
Natoa
shukrani kwa viongozi wa vyama vyote vya siasa vilivyoshiriki katika uchaguzi, kuyapokea matokeo na kuheshimu uamuzi wa wananchi
katika uchaguzi huo. Napenda nisisitize kuwa naheshimu maridhiano na matakwa ya
kikatiba ya kushirikiana na vyama vyengine vya siasa katika kuendesha Serikali
kuwatumikia wananchi wa Zanzibar. Navihakikishia tena vyama hivyo kwamba niko
tayari kuyatekeleza maridhiano kama Katiba ya Zanzibar inavyoelekeza.
DHIMA YA SERIKALI YA AWAMU YA 8
Mheshimiwa Spika,
Nimekuja Barazani leo hii
kutimiza takwa la Katiba yetu linalonitaka kulizindua rasmi Baraza la
Wawakilishi. Nami ninayo furaha na fahari kubwa kutekeleza takwa hilo.
Hivyo napenda kuitumia fursa
hii kuzungumza nanyi mambo muhimu yahusuyo ustawi wa nchi yetu, watu wetu na
dhima ya Serikali ya Awamu ya 8. Lengo langu ni tuweze kufahamiana juu ya
tulipo, tunapotaka kwenda na namna ambavyo sisi katika Serikali tumejipanga
kutafsiri na kutekeleza Ilani ya CCM ya 2020-2025, ambayo Chama Cha Mapinduzi
kinachounda Serikali kimetuelekeza tuitekeleze. Nafanya hivyo ili wenzetu
katika Baraza mtufahamu na kuona namna bora ya kutusaidia kufanikisha azma
hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Ninaposimama mbele yenu leo,
ninafarijika na mambo matatu makubwa. Kwanza, mimi ni Rais wa Awamu ya 8 ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Kabla
yangu, kumekuwapo na Marais 7. Wote hawa wamefanya kazi kubwa sana ya kuitoa
Zanzibar ilipokuwa kuifikisha ilipo leo ikiwa na mafanikio makubwa. Kutangulia
kwao na kazi nzuri waliyoifanya, kunanifanya mimi kuanzia mahala pazuri zaidi
kuliko pale walipopokea wao. Kipekee, nashukuru sana kuipokea nchi kutoka kwa
Rais wa Awamu ya 7 na Mzee wangu Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein. Amefanya
kazi kubwa sana yenye kustahili pongezi zetu nyingi. Jukumu lililo mbele yangu
ni kumalizia pale ambapo hakukamilisha, kuendeleza mazuri aliyoyaacha na
kufanya mengine mapya ya kuipeleka nchi yetu mbele.
Pili, Nimepata
bahati na heshima kubwa ya kuwaongoza wananchi wa Zanzibar ambao Asilimia
93 kati yao, wamezaliwa baada ya
Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya 1964 na Muungano wetu wa mwaka 1964.
Najisikia fahari kuwa Rais wa kwanza kuiongoza Zanzibar ambaye amezaliwa baada
ya matukio hayo mawili muhimu
katika historia yetu.
Hii kwangu ina maana kubwa
sana. Nayo ni kuyatafsiri upya Mapinduzi yetu Matukufu na Muungano wetu katika
kizazi kipya. Tafsiri hiyo si nyengine bali ni kuijenga Zanzibar Mpya kwa
kufanya Mapinduzi Mapya, ambayo ni Mapinduzi ya Kiuchumi. Ikumbukwe pia kuwa
lengo la Mapinduzi halikuwa tu kuondosha Usultani, bali kuleta uhuru na ustawi
kwa wananchi wa Zanzibar. Hilo la kwanza la uhuru tumefanikiwa. Hili la pili la
ustawi bado tunayo safari ndefu. Ni matamanio yangu kuyadumisha Mapinduzi
Matukufu ya Zanzibar kwa kuyatafsiri katika muktadha wa mahitaji ya sasa ambayo
ni ukombozi wa kiuchumi. Hiyo ndio itakuwa tafsiri yangu na ya Serikali nitakayoiunda
ya ile kauli mbiu yetu tukufu “Mapinduzi … Daima”.
Tatu, kote
nilikopita wakati wa kuomba ridhaa ya wananchi wa Zanzibar, nimekutana na ari,
shauku na utayari wa hali ya juu ya wake kwa waume, vijana kwa wazee, wakulima
kwa wavuvi, wafanyabiashara kwa wafanyakazi na makundi yote, ya kuyapokea
Mapinduzi mapya ya kiuchumi na kujenga Zanzibar mpya. Wananchi wetu wamechoshwa
na siasa za uhasama, kuhubiri chuki na visasi ambazo hazibadilishi hali ya
maisha yao kuwa bora zaidi. Wanataka matunda ya Mapinduzi na si
simulizi za Mapinduzi na Muungano.
Wanachotaka ni kustawi na kufaidika na matunda ya mapinduzi kwa usawa, bila
upendeleo wala ubaguzi. Mimi nakubaliana nao na ninasimama nao! Nami
nimewaahidi, “Yajayo ni neema tupu”.
Kwa mnasaba huu, nimedhamiria
kuwaunganisha wananchi wote kuwa wamoja, bila ya kujali rangi, asili, jinsia,
imani za kidini au itikadi za kisiasa, jambo ambalo tayari nimeanza
kulitekeleza katika uteuzi wa viongozi ninaoendelea kuufanya. Ifahamike kwamba
uteuzi wa viongozi na watendaji katika Serikali yangu utazingatia uwezo wa mtu
kitaaluma, uwajibikaji na uaminifu.
MAPINDUZI YA UCHUMI
Mheshimiwa Spika,
Katika
kuijenga Zanzibar mpya, moja ya ahadi yangu kubwa niliyoitoa kwa wananchi na
ambayo imeelekezwa na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ni kujenga uchumi wa kisasa wa
Bluu (Blue Economy). Uchumi wa Buluu, ama uchumi wa bahari unafungamanisha kwa
pamoja sekta za uvuvi, ufugaji samaki,
ujenzi wa viwanda vya kusindika samaki, ukulima wa mwani, uchimbaji wa mafuta
na gesi, matumizi bora ya rasilimali mbali mbali za bahari pamoja na shughuli
za utalii wa fukwe na michezo ya baharini.
Zanzibar
hatukujaaliwa ardhi kubwa. Nchi yetu ni visiwa. Idadi ya watu wetu imeongezeka
mara tano katika kipindi cha
miaka 56. Mwaka 1964 Wazanzibari tulikua
laki 3 tu, leo tuko takribani milioni
1.6. Wakati huo huo Visiwa vyetu havipanuki wala kuongezeka. Ndio
kusema, ardhi yetu inazidi kuwa finyu mwaka hadi mwaka. Ahueni tuliyonayo ni
kuwa na eneo kubwa la bahari. Hivyo sisi Wazanzibari hatuna budi tuigeuze
bahari hii kuwa ndio shamba letu. Huko ndiko fursa na ajira za Zanzibar mpya
zilipo. Huu ndio msingi wa dhana nzima ya Uchumi wa Bluu.
UVUVI
Mheshimiwa Spika,
Uvuvi ni eneo ambalo hatujalitumia vyakutosha
na linaweza kutuletea manufaa mengi. Serikali itaweka mkazo juu ya kuendeleza
uvuvi wa bahari kuu kwa kununua vyombo vitavyoweza kutumika kwa aina hiyo ya
uvuvi. Nitazitekeleza ahadi nilizozitoa wakati nilipokutana na wawakilishi wa
wavuvi ikiwemo ahadi ya kuwawezesha wavuvi kwa kuwapatia vyombo vya kisasa na
mikopo kwa ajili kuendeleza shughuli zao. Hili litakwenda sambamba na kuboresha
masoko yaliyopo na kujenga masoko mapya ikiwa ni pamoja na viwanda vya
usindikaji wa Samaki kwa ajili ya kuuza ndani na nje ya nchi.
Vile vile, katika maeneo mbali mbali ya
Unguja na Pemba hasa yale yenye bahari zenye mikoko na yenye mazingira mazuri,
tumedhamiria kuimarisha shughuli za ufugaji wa samaki, kama nilivyoahidi,
katika kampeni. Serikali itazalisha na kusambaza kwa wananchi vifaranga vya
samaki milioni 10 kila mwaka kwa
watakaojishughulisha na ufugaji samaki.
Kwa upande wa zao la mwani, tutaongeza uzalishaji kwa kuwawezesha wakulima wa zao hilo. Kama nilivyoahidi wakati wa Kampeni, tutawapatia vifaa na mikopo nafuu wakulima wa mwani, tutajenga viwanda vya kusarifu mwani, tutawatafutia masoko mapya ili zao hilo liwe na bei kubwa zaidi itakayosaidia kuinua hali ya maisha na kipato chao, hasa kina mama. Nawataka wajumbe wa Baraza hili la Kumi, muwe mstari wa mbele kuisimamia Serikali na kuishauri juu ya namna bora ya kutekeleza azma yetu hiyo.
UTALII
Mheshimiwa Spika,
Serikali ya Awamu ya Nane itaendelea
kushirikiana na Sekta Binafsi katika kukuza na kuimarisha Sekta ya Utalii
ambayo hivi sasa ndiyo muhimili mkuu wa uchumi wetu. Tutashirikiana kuitangaza
Zanzibar katika masoko ya asili na masoko mapya; kuendelea na ujenzi wa hoteli
za daraja la juu na miundombinu muhimu; kulinda na kuhifadhi vivutio vya utalii
vilivyopo pamoja na kuanzisha vivutio vyengine vipya. Ninapata matumaini
makubwa kuona kwamba licha ya kuwepo kwa changamoto kadhaa zilizosababishwa na
maradhi ya COVID 19, bado kuna mashirika mengi ya ndege na yale
yanayoshughulika na biashara ya utalii yanayotaka kufanya safari za kuja
Zanzibar kwa ajili ya kuleta wageni. Tumepata taarifa ya ongezeko la wageni katika siku za karibuni.
Mheshimiwa Spika,
Kuendelea
kuimarika kwa sekta ya utalii hivi sasa, kunanipa matumaini kwamba tutaweza
kuyafikia malengo yaliyowekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya kuongeza idadi ya
wageni wanaoitembelea Zanzibar kutoka 538,264
mwaka 2019 hadi kufikia wageni 850,000
mwaka 2025. Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza hili tukufu tuna kazi kubwa ya
kushajiisha na kuendeleza Mpango wa Utalii kwa Wote yani “Tourism for All”, ulioanzishwa na
Awamu iliyopita ili manufaa ya sekta hii yamguse kila mwananchi kama
ilivyokusudiwa. Nimeahidi na nitaitekeleza ahadi ya kuongeza
utalii katika kisiwa cha Pemba. Nina azma ya kukifanya kisiwa cha Pemba, eneo
maalum la uwekezaji yaani Strategic Investment Area kwa kutoa vivutio mahsusi
kwa wawekezaji ili maendeleo ya Unguja yaende sambamba na maendeleo ya Pemba.
Serikali ninayoiongoza itahakikisha kwamba juhudi zetu za kukuza
utalii zinakwenda sambamba na utekelezaji wa mipango yetu ya kuelimisha jamii
umuhimu wa kuulinda na kuutangaza utamaduni wetu, kuyathamini mambo ya
kale pamoja na kuendeleza historia na
urithi wa Zanzibar, ukiwemo Mji Mkongwe
ambao umepata umaarufu mkubwa hivi sasa
duniani kote.
MAFUTA
NA GESI
Mheshimiwa Spika,
Sekta ya Mafuta na Gesi ni miongoni mwa
maeneo makuu ya Uchumi wa Buluu. Serikali ya Awamu ya Nane itaendeleza juhudi
za kushughulikia Sekta hii. Tarehe 23 Oktoba, 2020, Mheshimiwa Rais Mstaafu wa
Awamu ya Saba, Dk. Ali Mohamed Shein alitoa taarifa maalum kwa waandishi wa habari, kuhusu matokeo ya Awali ya tafiti
zilizofanywa katika utafutaji na
uendelezaji wa rasilimali
hizo. Ufupisho wa taarifa
iliyotolewa ni kwamba tafiti zilizofanywa zimeonesha uwezekano mkubwa wa kuwepo
miamba yenye kuhifadhi rasilimali za mafuta na gesi asilia. Utafiti umeonesha
kuwepo kwa maumbile ya miamba (structures) yenye uwezo wa kuhifadhi rasilimali
ya gesi asilia yenye ujazo wa futi trilioni 3.8.
Matokeo haya ya utafiti yanathibitisha ile
kauli mbiu yetu kwamba “yajayo ni neema
tupu”. Tumeshafikia makubaliano ya kindugu baina ya Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kulitoa suala la
mafuta na gesi katika mambo ya Muungano; na hivi sasa sheria mbali mbali
zimeshatungwa za kusimamia Sekta hiyo. Kwa hivyo, Zanzibar itanufaika moja kwa
moja na mapato yote yanayotokana na rasilimali hizo wakati wowote kazi ya
uchimbaji itakapoanza.
Kwa hivyo, Serikali ya Awamu ya 8 itaziimarisha na kuzijengea uwezo wa
kitaaluma na nguvukazi Kampuni ya Mafuta Zanzibar (ZPDC) na Mamlaka ya Usimamizi wa Mafuta na Gesi (ZPRA) ili ziweze
kuiongoza sekta hii muhimu. Vile vile,
tutaendelea kushirikiana na kampuni mbali mbali zenye dhamira njema ya kuwekeza
katika nchi yetu kwenye sekta hiyo.
BANDARI
Mheshimiwa
Spika,
Serikali ya Awamu
ya Nane ina malengo ya kujenga bandari kubwa katika maeneo ya Mangapwani.
Bandari hiyo ya kisasa itakuwa kubwa yenye sehemu kadhaa za kutolea huduma
zikiwemo sehemu za kuhudumia meli zitakazobeba mafuta na gesi, chelezo kwa
ajili ya matengenezo ya meli, eneo la kuhudumia meli zinazobeba mizigo na
makontena, bandari ya uvuvi na bandari ya meli za kitalii.
Mheshimiwa Spika,
Uchumi wa Bluu haukamiliki bila kuweko kwa Bandari za
kisasa zenye ufanisi wa hali ya juu. Kwa upande wa bandari, yamekuwepo malalamiko
ya wafanyabiashara kuhusu kucheleweshewa mizigo yao bandarini na msongomano wa
makontena katika bandari ya Malindi, vitendo vya rushwa na kukosa uwajibikaji
kwa baadhi ya watumishi wa bandari.
Kwa kutambua umuhimu wa Bandari kwa Zanzibar, sikukawia
kuanza na jambo hili mara tu baada ya kuapishwa kwangu. Tarehe 3 Novemba, 2020
niliamua kutembelea Bandari ya Malindi, ili kuweza kufahamu kwa kina malalamiko
ya wafanyabiashara na wananchi kuhusiana na utendaji kazi na utoaji wa huduma
usioridhisha unaofanywa na wafanyakazi katika Bandari yetu hiyo.
Bandari
ni lango kuu la biashara duniani. Kwa hivyo kukosekana kwa ufanisi unaopelekea
usumbufu kwa wafanyabishara katika Bandari yetu kuu ya Malindi kunazorotesha
kasi ya ukuaji wa uchumi wetu; kwa sababu wafanyabiashara hao hulazimika
kutumia bandari nyengine; hasa za Mombasa na Dar es Salaam.
Katika
uzinduzi wa Baraza hili la Kumi la Wawakilishi, nataka niwajulishe viongozi na wafanyakazi wote katika
bandari zetu kuu za Unguja na Pemba
pamoja na Viwanja vya ndege kwamba nitakuwa nikifuatilia kwa karibu utendaji wa
taasisi hizo. Ieleweke bayana, kwamba sijaridhishwa na
uendeshaji wa shughuli za bandari
na viwanja vyetu vya ndege, katika maeneo yote, hasa utoaji wa huduma, uendeshaji, ukusanyaji
na udhibiti wa mapato, kiwango cha faida kinachopelekwa Serikalini
kila mwaka pamoja na mipango ya matumizi ya fedha za maendeleo. Nitahakikisha
kwamba wafanyakazi wa bandarini na
viwanja vya ndege ni wale wanaopenda kazi
kuwatumikia watu,
na sio wale wenye malengo binafsi ya kujinufaisha.
Napenda kuliarifu
Baraza lako Tukufu kuwa tayari tumeshaanza kuzifanyia kazi changamoto hizo
ikiwemo kujaza nafasi ya Mtendaji Mkuu katika mamlaka ya Bandari. Hili ni eneo
ambalo nitalisimamia kwa nguvu zangu zote maana ni eneo lenye fursa ya kutupa
mapato mengi ya kuendeleza Zanzibar yetu. Vile vile, tumedhamiria kuiimarisha
bandari za Wete na Shumba Mjini. Kadhalika, tutaiimarisha bandari ya Mkoani ili
iweze kuhudumia meli kubwa kutoka nje moja kwa moja kwa lengo la kunyanyua
uchumi na biashara kwa kisiwa cha Pemba.
BIASHARA
NA VIWANDA
Mheshimiwa
Spika,
Serikali
ya Awamu ya 8 itaendeleza
dhamira njema ya kukuza Sekta za Biashara na Viwanda hapa Zanzibar, ili
kuwaletea wananchi wake maendeleo zaidi ya kiuchumi. Katika kipindi changu cha uongozi nitahakikisha kwamba
Sekta Binafsi inashiriki kikamilifu katika utekelezaji wa mipango na mikakati
iliyopo ya ujenzi wa viwanda vidogo vidogo, vya kati na vikubwa vyenye kuzalisha bidhaa bora,
zenye viwango na vyenye kuhimili
ushindani wa soko. Nitahakikisha
tunatekeleza ahadi niliyotoa katika Wilaya mbali mbali za Unguja na
Pemba ya kujenga viwanda mbali mbali, vikiwemo viwanda vya kusarifu mwani, kusindika samaki na mazao
mengine, ili kuyaongezea thamani. Serikali itahakikisha inavilinda viwanda
hivyo dhidi ya ushindani usio wa haki wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje ya nchi
ambazo hazilipiwi kodi stahiki.
Serikali inatambua kwamba hii ndio njia ya uhakika ya
kutengeneza ajira, kutoa soko kwa malighafi za ndani na kuongeza pato la
Serikali linalotokana na kodi stahiki zitakazolipwa na viwanda hivyo.
MAKUSANYO YA KODI
Mheshimiwa Spika,
Ili tuweze kutekeleza kwa ufanisi ujenzi wa uchumi mpya,
ni lazima tuongeze uwezo wetu wa kukusanya kodi. Serikali ya Awamu ya
8 itaongeza nguvu katika upanuzi wa wigo wa kodi na kuongeza ufanisi katika
ukusanyaji wa mapato. Tutahakikisha kwamba kila mtu anayestahili kulipa kodi
analipa kodi stahiki. Aidha, tutahakikisha kwamba kila senti inayoongezeka
katika mapato ya Serikali inaelekezwa katika kutoa huduma bora zaidi kwa
wananchi. Tutaziba mianya ya upotevu wa fedha za Serikali ambayo inaipunguzia
Serikali uwezo wake wa kuwahudumia wananchi.
SEKTA
BINAFSI
Mheshimiwa
Spika.
Naamini kwamba ili kuweza kutekeleza kwa
ufanisi dhamira yetu ya kufanya mageuzi ya kiuchumi, lazima pawe na ushirikiano
mzuri na wa kuaminiana baina ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi. Wakati wa
Kampeni za Uchaguzi nilikutana na viongozi waliowakilisha Sekta Binafsi kwa
lengo la kujadiliana, kubuni na kutafuta njia bora za kuimarisha uhusiano na
ushirikiano katika kuijenga nchi yetu.
Serikali
ya Awamu ya 8, itaweka mazingira mazuri ya uwekezaji na uendeshaji wa biashara
ili sekta binafsi iwe na mchango mkubwa zaidi katika kukuza ajira na katika
Pato la Taifa. Ushirikiano na umoja wetu ndio utakaotuwezesha kutekeleza miradi yenye tija ikiwemo uendelezaji wa
viwanda, utaliii na uchumi wa buluu. Ili
kufanikisha azma hii, serikali itaweka mifumo rafiki kwa sekta binafsi kuweza
kufanya kazi zao kwa ufanisi. Kadhalika, Serikali itaweka mazingira rafiki kwa
Wanadiaspora kuja kuwekeza nyumbani kwa lengo la kuleta mapinduzi makubwa ya
kiuchumi tunayokusudia kuyafanya. Nataka niwahakikishie wadau wa Sekta Binafsi
kwamba Serikali yangu haitakua kikwazo kwa Sekta Binafsi bali tutakuwa wadau
wezeshi. Kwa mnasaba huu, sitokubaliana na visingizio vya aina yoyote na uzembe
wa watendaji vyenye kukwamisha azma yangu hii.
VIWANJA VYA
NDEGE
Mheshimiwa
Spika,
Mapinduzi makubwa ya uchumi tunayoyatarajia, yanahitaji
kuwa na viwanja vya ndege vya kisasa vyenye ubora wa kimataifa. Tutaendeleza
jitihada zilizofanywa za kuimarisha Kiwanja cha Ndege cha Abeid Amaan Karume
hasa baada ya ujenzi wa jengo la Terminal Three. Hatua hiyo
sio tu imeuongezea hadhi na haiba uwanja huo, bali pia itawezesha kuzihudumia
ndege kubwa zaidi pamoja na idadi kubwa ya abiria, mizigo na watalii wanaoitembelea Zanzibar. Aidha,
tunathamini jitihada zilizofanywa katika kuimarisha miundombinu ya uwanja wa
ndege wa Pemba, ikiwemo kuongezwa majengo ya kutolea huduma pamoja na kuwekwa
taa za kuongozea ndege. Tutaendelea na juhudi za kuimarisha viwanja hivyo pamoja na huduma zinazotolewa,
ili viwe na mchango zaidi katika kuongeza ukusanyaji wa mapato na kukuza soko
la ajira.
BARABARA
Mheshimiwa Spika,
Ujenzi wa barabara bora za kisasa ni muhimu katika
kufikia mapinduzi ya uchumi mkubwa wa kisasa tunaoutarajia kuujenga. Katika
kipindi cha miaka mitano ijayo, nimeahidi kuendeleza kazi za ujenzi wa barabara
kwa kiwango cha lami yenye urefu wa zaidi ya kilomita 197.6. Unguja na Pemba.
Miongoni mwa barabara zitakazojengwa kwa Unguja ni
Tunguu-Jumbi (km9.3), Jozani-Charawe-Ukongoroni-Bwejuu (km23.3), Fumba-Kisauni
(km 12), Kizimbani-Kiboje (km 7.2) na Kichwele-Pangeni (km 4.8). Nyengine ni
barabara ya Umbuji- Uroa (km 6.9), Mkwajuni-Kijini (km 9.4) na
Tunguu-Makunduchi (km48). Vile vile, kwa kuzingatia usumbufu wanaoupata
wananchi wanaoishi vijiji vya Uzi na Ng’ambwa, Serikali itashughulikia ujenzi
wa barabara na daraja kutoka Unguja ukuu hadi kisiwa cha Uzi.
Kwa upande wa Pemba, tutazijenga kwa kiwango cha lami
barabara ya Chake chake – Wete (km 22.1), Mkoani-Chake chake kupitia Chanjaani
(km 29) na barabara ya Finya – Kicha (km 8.8). Vile vile, tutazitengeneza
barabara za ndani za Unguja na Pemba ili zipitike kwa urahisi wakati wote.
NISHATI YA
UMEME
Mheshimiwa
Spika,
Uchumi mkubwa wa kisasa tunaoukusudia, unahitaji
kupatikana kwa nishati ya umeme wa kutosha wenye uhakika. Dhamira yetu ya
kuhamasisha uwekezaji katika Sekta ya Viwanda inahitaji kuwa na umeme wa kiwango
kikubwa. Kwa upande wa Unguja, mahitaji ya umeme hivi sasa yameshafikia
megawati 80, ambapo laini mpya ya umeme tuliyo nayo ina uwezo wa kuchukua
megawati 100; na ile ya zamani ina uwezo wa kuchukua megawati 40.
Kwa mantiki hii, baada ya kipindi kifupi kijacho, kiwango
cha umeme tulichonacho kitakua ni changamoto katika kufikia dhamira yetu ya
kujenga uchumi mpya wa kisasa. Hali hii, inatulazimisha kuanza kuendeleza suala
la kutafuta vyanzo vipya vya umeme, ikiwemo nishati mbadala ili nchi yetu iwe na
umeme wa uhakika.
HUDUMA
ZA FEDHA
Mheshmiwa
Spika,
Sambamba na miongozo ya Ilani ya Uchaguzi,
Serikali ya Awamu ya 8, itaweka mkazo mkubwa katika kuimarisha Sekta ya Huduma
za Fedha kwa kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na uendeshaji wa shughuli za
benki, mashirika ya bima na taasisi nyengine za fedha. Dhamira yetu ni kuona
kwamba huduma za fedha zinazotolewa na taasisi binafsi na Serikali zinakidhi
wiwango na mahitaji halisi ya wawekezaji, watalii, wageni wanaotumbelea pamoja
na wananchi kwa jumla. Serikali itasimamia utendaji wa mashirika yake kwa lengo
la kuhakikisha kwamba taasisi hizo zinatoa huduma bora zenye kuaminika kwa
wateja wote.
TEKNOLOJIA
Mheshmiwa
Spika,
Matumizi bora ya teknolojia ni msingi muhimu
katika juhudi zetu za kuendeleza viwanda, biashara, utalii, huduma za fedha na
shughuli mbali mbali za kijamii. Kwa msingi huo, Serikali ya Awamu ya 8 ina
lengo la kuendesha shughuli zake katika mifumo ya kisasa ya kidigitali. Tutaweka
mifumo ya kidijitali katika ukusanyaji wa kodi za Serikali, manunuzi ya umma na
uendeshaji wa Serikali kwa ujumla. Aidha, Serikali itaimarisha
mitaala ya masomo ya sayansi katika skuli, vituo na taasisi za ufundi
pamoja na vyuo vikuu ili kuwaandaa
vizuri vijana wetu na hatimae kuweza
kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia katika sekta zote.
KILIMO
Mheshimiwa
Spika,
Serikali
ya Awamu ya 8 itaendeleza mipango na mikakati iliyoanzishwa na Serikali ya Saba
katika kuendeleza Sekta ya Kilimo ili kuhakikisha kwamba nchi yetu
inajitosheleza kwa mahitaji ya chakula. Tutaendeleza mpango mkuu wa umwagiliaji
maji Zanzibar (Zanzibar Irrigation Master Plan) ambao umebainisha kuwa zipo
hekta 8,521 zinazofaa kujengwa miundombinu ya umwagiliaji maji. Hivi sasa,
jumla ya hekta 2,527 tayari zinaendelea kujengwa miundombinu ya umwagiliaji
maji kutoka hekta 700 za mwaka 2010. Ujenzi huo unaendelezwa katika mabonde ya
Cheju, Kilombero, Chaani, Kibokwa, Kinyasini kwa Unguja na Mlemele na
Mkwararani kwa upande wa Pemba. Halikadhalika, Serikali itahakikisha
inaendeleza huduma za ugani kwa kuajiri wataalamu wa kutosha na kutoa vifaa
vinavyohitajika.
Kadhalika,
tutaendelea kuhimiza kilimo cha kisasa katika uzalishaji wa mazao mengine ya
chakula kwa kuwawezesha vijana kuendeleza kilimo kwa ujenzi wa vitalu nyumba
(green houses) na matumizi ya mbegu bora za kilimo. Vile vile, tutaweka mkazo
katika kununua pembejeo za kilimo, dawa za kuulia magugu pamoja na kuwapatia
wakulima huduma bora za matrekta. Watu wengi
duniani hivi sasa wanapendelea kula vyakula vinavyotokana na kilimo hai yaani
“Organic Farming” kutokana na ladha ya asili ya vyakula hivyo pamoja na
uwezekano wa kuwa vinapunguza athari za kemikali. Ni jambo muhimu kwa Taasisi
itakayohusika na Kilimo kulifanyia utafiti suala la kukiendeleza kilimo hai
nchini mwetu na upatikanaji wa masoko ya mazao yanayopatikana kutokana na
kilimo hicho.
Mheshimiwa Spika,
Kwa
kutambua umuhimu wa zao la karafuu na uhusiano wake katika historia na
maendeleo ya kiuchumi ya Zanzibar, Serikali ya Awamu ya Nane itaendeleza juhudi
zilizopo za kuliimarisha zao hilo kwa kutoa mikopo na kuwatafutia masoko
wakulima. Kadhalika, kutokana na tatizo kubwa la uhaba wa nazi unaopelekea
kupanda bei ya zao hilo kila uchao, Serikali itaimarisha upandaji wa miche ya
minazi ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo. Serikali itasimamia na kuendeleza
programu ya kufufua zao la minazi
iliyoanzishwa mwaka 2019; lengo likiwa ni kuotesha miche ya minazi
1,200,000 (Unguja minazi 720,000 na Pemba minazi 480,000); ambapo asilimia 17
itakuwa ni minazi ya madafu naasilimia 83 itakuwa ni minazi yetu ya asili (East African tall).
UFUGAJI
Mheshimiwa
Spika,
Serikali
ya Awamu ya 8, itaweka mkazo katika kuendeleza shughuli za ufugaji wa njia za
kisasa, ili sekta hiyo iwe na tija zaidi kwa wakulima na kuongeza mchango wake
katika upatikanaji wa chakula na kuimarisha Pato la Taifa.
Tutahakikisha panakuwa na matumizi mazuri ya
pembejeo za mifugo, dawa za chanjo na kutoa elimu juu ya matumizi ya mbegu bora
za mifugo. Serikali itabuni na kutekeleza mikakati madhubuti ya kukomesha wizi wa
mifugo na mazao. Katika kuitekeleza
mikakati hiyo, tuzingatie sheria za nchi yetu na Waheshimiwa Wawakilishi muwashirikishe
wananchi majimboni mwenu katika kupambana na wizi wa mifugo na mazao ya kilimo
ambao hivi sasa umekithiri katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba.
Ninaamini kwamba kwa juhudi za pamoja
tunaweza kukomesha vitendo hivi viovu vinavyorejesha nyuma maendeleo ya
wakulima na wafugaji. Katika kuiendeleza sekta ya mifugo, serikali itakaribisha
wawekezaji wakubwa wa ufugaji hasa wa ng’ombe na mbuzi wa maziwa ambao wataweza
kuwasaidia wafugaji wetu wa dogo wadogo kuzalisha bidhaa nyingine zinazotokana
na mifugo.
MAZINGIRA
NA TABIANCHI
Mheshimiwa Spika,
Utekelezaji
wa mipango yetu ya maendeleo utazingatia sana kuwepo kwa mipango mizuri ya
uhifadhi wa mazingira na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Tutahakikisha
kwamba tuna matumizi mazuri ya rasilimali zisizorejesheka, utunzaji wa
maliasili na misitu, fukwe pamoja na bahari.
Kadhalika,
tutaweka mkazo katika kuhakikisha kwamba Manispaa, Mabaraza ya Miji na
Halmashauri zetu zinasimamia vyema jukumu lao la usafi wa miji. Nataka niweke
wazi kwamba kiwango cha usafi katika miji yetu hakiridhishi. Naamini kwamba
Waheshimiwa Wajumbe mtaungana na mimi nikisema kwamba hakuna sababu ya kuifanya
miji yetu isiwe safi na salama. Kwa hivyo, Serikali itahakikisha kwamba miji
yetu inakuwa safi wakati wote kwa ajili ya kulinda afya za wananchi na kuvutia
wageni wanaokuja kututembelea.
HUDUMA
ZA JAMII
Mheshimiwa Spika,
Serikali
ya Awam ya 8, itaweka kipaumbele katika kuziimarisha huduma za elimu, afya na
maji safi na salama kwa kuzigatia umuhimu wake kwa ustawi wa maendeleo ya jamii.
ELIMU
Mheshimiwa
Spika,
Kwa kutambua umuhimu wa sekta ya elimu kama
ni nyenzo muhimu ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii, Serikali itachukua hatua
za kuimarisha ubora wa elimu ambayo ni haki ya msingi kwa kila mwananchi.
Katika kukabiliana na changamoto zinazoikabili sekta ya elimu hivi sasa,
Serikali itaelekeza juhudi katika kuimarisha miundombinu ya elimu, ikiwemo, ujenzi
wa skuli za kisasa na kuzikarabati skuli za zamani, kuzipatia skuli vifaa vya
kufundishia na kusomea pamoja na madawati, kupitia upya mitaala ya elimu na
kupunguza tatizo la walimu hasa wa masomo ya Sayansi.
Kadhalika, tutaimarisha kiwango cha ufaulu
kwa wanafunzi katika mitihani ya Taifa, kuendeleza masomo ya ufundi katika vyuo
vya amali na vituo mbali mbali. Ili kufikia dhamira hiyo, Serikali itaongeza
bajeti ya sekta ya elimu ili iweze kugharamia vyema huduma za elimu katika
ngazi zote kwa kuendeleza sera ya elimu pamoja na kuongeza fursa za mikopo ya
wanafunzi wanaojiunga na masomo ya elimu ya juu.
Pamoja
na hatua hizo, tutayaimarisha maslahi ya walimu ili kuwapa motisha ya
kufundisha na tutaendeleza sera ya elimu bure kwa lengo la kuwaondolea wazazi
mzigo wa kuchangia elimu ya watoto wao.
Mheshimiwa
Spika,
Nikiwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha
Zanzibar (SUZA), nitahakikisha kwamba tunakiendeleza Chuo hiki kwa kuanzisha
programu mpya kutegemea mahitaji halisi ya nchi yetu, sambamba na kujenga majengo
mapya pamoja na kukipatia vifaa vya kisasa vya kufundishia vinavyohitajika ili
kuweza kutoa elimu bora kwa wanafunzi wanaojiunga na chuo hicho. Tutaweka mkazo
katika kufanya tafiti kwenye maeneo muhimu kwa kuzingatia ajenda za maendeleo
ya kiuchumi na kijamii za nchi yetu.
Tutahakikisha kwamba SUZA inaendelea kuwa na
uhusiano mwema na vyuo na taasisi za elimu ya juu zilizopo Zanzibar na sehemu
mbali mbali za dunia. Tutaendelea kuweka mkazo maalum katika kufundisha Kiswahili
ili kutekeleza dhamira yetu ya kuifanya Zanzibar kuwa chimbuko la Kiswahili
sanifu na fasaha. Tutahakikisha kwamba wahitimu wa chuo chetu hiki katika fani
zote tunazofundisha wanabobea kitaaluma na wanajengeka kiushindani katika soko
la ajira popote wanapokwenda.
AFYA
Mheshimiwa
Spika,
Kwa
upande wa Sekta ya Afya, Serikali itandelea na ujenzi wa Hospitali ya Rufaa
huko Binguni Wilaya ya Kati ambayo itakuwa na huduma zote za kibingwa. Mpango
wake upo na lazima tuusimamie utekelezaji wake kwa nguvu zetu zote. Hatua hiyo,
itatuwezesha kupunguza na hatimae kuondoa kabisa tatizo la kupeleka wagonjwa
nje ya nchi.
Sambamba
na juhudi hizo, tutaendelea kuimarisha miundombinu ya afya, ununuzi wa dawa na
vifaa tiba, kuongeza idadi ya madaktari bingwa wa fani mbali mbali na wataalamu
wengine wa afya. Tutaongeza bajeti ya kununulia dawa na vifaa vyengine vya
huduma za afya. Vile vile, tutaongeza nyumba za madaktari na kujenga vituo vya
afya ili kuondoa usumbufu wanaoupata baadhi ya wananchi kufuata huduma za afya
katika maeneo ya mbali.
Aidha, tutaimarisha Hospitali ya Rufaa ya
Mnazi Mmoja na hospitali za wilaya za Makunduchi na Kivunge. Tutazijengea uwezo
Hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani, Hospitali ya Chake Chake na Wete pamoja na
kuipandisha hadhi hospitali ya Micheweni. Lengo letu ni kuona kwamba huduma
zote za kibingwa zinapatikana katika Kisiwa cha Pemba. Katika kufikia dhamira
zetu hizo, tutawashajiisha wawekezaji kuwekeza katika sekta ya afya. Vile vile,
tutaangalia uwezekano wa kuanzisha bima ya afya kwa wenye uwezo na kwa wale
wasio na uwezo Serikali itaendelea kuwapatia huduma za afya bure.
MAJI SAFI NA
SALAMA
Mheshimiwa
Spika,
Upatikanaji wa huduma za maji bado ni changamoto katika
baadhi ya maeneo ya mjini na
vijijini. Hali ya upatikanaji wa maji
hivi sasa imefikia wastani wa asilimia 83 katika mwaka 2020. Kwa kuzingatia kuwa maji ni uhai, Serikali ya
Awamu ya 8 itamalizia kazi iliyobaki ya kuiboresha miundo mbinu ya maji na
kuongeza upatikanaji wake. Kazi hiyo, ni pamoja na kujenga matangi mapya ya
kuhifadhia maji, uchimbaji wa visima vipya vya maji na kuendelea kuifanyia
matengenezo miundombinu ya zamani, ikiwemo kuvitengeneza visima vya zamani na
kuviwekea pampu zenye nguvu zaidi. Vile vile, tutayabadilisha mabomba ya zamani
na kukabiliana na tatizo la uvujaji wa maji.
UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI
Mheshimiwa
Spika,
Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ni
miongoni mwa malengo ya Serikali ya Awamu ya 8 katika kukabiliana na tatizo la
umaskini wa kipato unaosababishwa na ukosefu wa ajira. Tunaelewa
kuwa bado kuna changamoto zinazowakabili wananchi katika kuendesha shughuli za
ujasiriamali, ambazo zinahusiana na ukosefu wa mitaji, vifaa, utaalamu wa
kutosha wa kuendesha biashara na utafutaji wa masoko ya uhakika ya kuuzia
biashara hizo. Katika kukabiliana na changamoto hizo, Serikali itauimarisha
Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kwa kuuongezea uwezo wa kutoa huduma
zilizo bora kwa wananchi wengi zaidi.
Kadhalika,
tutawasajili wajasiriamali wote na kuwapatia vitambulisho. Pia, tutatoa mafunzo
ya namna bora ya kuitumia mitaji na mikopo hiyo katika kupata vifaa na zana za
kisasa na kuendesha shughuli za ujasiriamali kitaalamu zaidi, kulingana na
mahitaji ya masoko ya wakati tulio nao.
Aidha,
tutawajengea wajasiriamali sehemu maalum za kufanyia biashara zao zitakazojengwa
vizuri, ili waondokane na usumbufu wa kuhamahama huku na kule. Pamoja na
jitihada hizi, Serikali itawawekea mfumo na utaratibu bora wa kulipa kodi mara
moja tu kwa mwaka na kuondosha ile kero ya utitiri wa kodi.
Katika
kuhakikisha kwamba mkakati huu unaleta ufanisi tunaoutarajia, tutakuwa
tunafuatilia kwa karibu na kufanya tathmini ya mikopo tunayoitoa kwa vikundi
hivyo, ili kujiridhisha endapo inawafikia walengwa na kwamba hakuna matumizi
mabaya ya fedha hizo yanayofanywa na watumishi wa Serikali wasio waaminifu.
Tusitosheke tu kutoa mikopo na mitaji na baadae kuripoti takwimu za vikundi
vilivyopokea mikopo hiyo, na kuirejesha au kutoirejesha. Ni lazima tujue mikopo
hio imeleta faida gani kwa wananchi.
UTAWALA BORA
Mheshimiwa
Spika,
Maendeleo, amani na utulivu ni dhana zenye maana
zinazotegemeana. Ili kuwe na maendeleo kunahitajika kuwe na amani na utulivu na
kwa upande mwengine, amani na utulivu haiwezi kupatikana ikiwa hakuna
maendeleo; ni kama uhusiano wa kuku na yai. Maendeleo katika nyanja mbali mbali
za maisha ndiyo yanayowaletea wananchi utulivu, na utulivu ndio unaoleta amani.
Wananchi wanaokabiliana na dhiki za maisha hasa katika kupata huduma muhimu za
kuyamudu maisha yao, mwishowe hujenga hasira, hasira ambayo huzaa chuki
miongoni mwao na kusababisha matendo maovu yanayopelekea kuvunjika kwa amani.
Ili uwiano mzuri upatikane baina ya amani, utulivu na
maendeleo ni lazima tuhakikishe kwamba Serikali inaongozwa katika misingi ya
utawala bora.
Mheshimiwa
Spika,
Miongoni mwa mambo yanayodhoofisha misingi ya utawala
bora ni vitendo vya rushwa, uzembe,
kukosa uwajibikaji, kutofuata sheria na kukiukwa kwa maadili. Serikali ya Awamu
ya 8 itakabiliana ipasavyo na vitendo vyote vinavyoathiri utekelezaji wa
misingi ya utawala bora.
Najua wananchi wanachukia sana rushwa na
ufisadi, na wamechoshwa na vitendo hivyo. Mimi pia ninachukia rushwa na
ufisadi. Vitendo vya rushwa na ufisadi vinawanyima haki wananchi na kuitia
hasara serikali. Mimi nimewaahidi wananchi, na nataka niirejee ahadi yangu kwao
mbele ya Baraza lako tukufu, kwamba nitapambana na rushwa na ufisadi bila
kigugumizi wala kuoneana muhali. Ninaomba Waheshimiwa Wawakilishi na Wananchi
wote mniunge mkono wakati wa mapambano haya.
Tutashinda vita hii endapo wananchi pia
watatuunga mkono. Sina shaka kuwa kwa vile wao, kwa wingi wao, wanachukia
rushwa na ufisadi, watakuwa tayari kutoa ushirikiano wao katika mapambano haya.
Ni matumaini yangu pia vyombo husika katika jambo hili vitatekeleza wajibu wao. Nataka niweke wazi kuwa kiongozi yoyote
nitayemteua kwa mamlaka niliyonayo kikatiba, nitamuwajibisha mara moja pindi tu
nikibaini na kujiridhisha kuwa anajihusisha na vitendo vya rushwa na ufisadi.
UTUMISHI
WA UMMA
Mheshimiwa Spika,
Mafanikio
katika utendaji wa Serikali yanategemea jinsi Sekta ya Umma inavyotekeleza wajibu
wake wa kuwatumikia wananchi kwa misingi ya uwajibikaji, usawa na haki.
Utendaji katika Sekta yoyote unategemea kuwepo kwa haki na utekelezaji wa
wajibu. Kwa maana nyengine, haki na wajibu ni watoto pacha. Serikali itaendelea
kuhakikisha kwamba watumishi wa umma wanapata haki zao kwa mujibu wa sheria
pamoja na kuwawekea mazingira mazuri ya kufanyia kazi. Kwa upande mwengine,
wafanyakazi nao wana wajibu wa kutekeleza kwa bidii na nidhamu kubwa majukumu
ya kazi zao kwa mujibu wa sheria za utumishi, kwa maslahi ya jamii na taifa kwa
jumla.
Kwa
hivyo, Serikali ya Awamu ya 8 itasimamia kwa umakini sana nidhamu na
uwajibikaji wa watumishi wa umma. Serikali haitakuwa na muhali kwa mtendaji
yoyote ambae hatowajibika katika utekelezaji wa majukumu yake. Atakayeshindwa
kuwajibika aelewe kuwa atawajibishwa. Uzembe na ukosefu wa nidhamu kazini huzorotesha maendeleo ya kiuchumi na
kijamii, kwa hivyo, tabia hii sitoivumilia. Kadhalika, tunahitaji ubunifu wa
kitaalamu katika kufanya kazi zetu na tuondokane na mtindo wa kufanya kazi kwa
mazoea.
Napenda viongozi wote nitakaowateuwa katika nafasi mbali
mbali walizingatie jambo hili. Ni lazima wawe wabunifu na waweze kuishauri
Serikali juu ya masuala mbali mbali yanayohusu fani na utaalamu wao. Serikali
haitowavumilia viongozi wenye kusubiri kuambiwa kutoka kwangu au Serikalini
nini wafanye katika kutekeleza majukumu yao. Tutaendelea kusimamia utekelezaji
wa sera na sheria ya hifadhi ya jamii kwa manufaa ya wanachama wote;
wafanyakazi na wastaafu. Tutafungua Ofisi za Mfuko wa Hifadhi ya Jamii katika
mikoa ya Zanzibar ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wanachama wake.
IDARA MAALUM
Mheshimiwa
Spika,
Serikali
itaziendeleza Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili
ziendelee kutoa huduma bora za ulinzi na usalama kwa
wananchi na kutekeleza majukumu
yao mengine kwa ufanisi na kwa mujibu wa sheria zinazoongoza Idara zetu hizo.
Tutaendeleza
miradi ya ujenzi wa majengo ya ofisi,
mahanga na nyumba za maofisa, sambamba
na kuyaimarisha mazingira ya kambi mbali mbali za Idara zetu maalumu.
Vile vile, tutaendelea kuwajengea uwezo
maofisa na wapiganaji kwa kuwapatia
vifaa na mafunzo ya kisasa katika vyuo vya ndani na nje ya nchi.
Kadhalika, tutaendelea kuimarisha maslahi yao
kwa kadri hali ya uchumi wetu itakavyoruhusu.
AJIRA
KWA VIJANA
Mheshimiwa Spika,
Mapinduzi makubwa
ya Uchumi tunayokusudia kuyafanya yatatupelekea kuwa na uchumi mpya wa kisasa,
ambao utaongeza fursa nyingi za ajira kwa vijana wetu. Kwa hivyo, ni wajibu wa
vijana wetu kuwa tayari kufanyakazi. Serikali itawajengea uwezo kwa kuwapatia
mafunzo maalumu ya ufundi wa fani mbali mbali katika vyuo vya ufundi na vituo
vya amali. Vile vile, vijana watawezeshwa kwa kupatiwa mitaji ili waweze
kujiajiri wenyewe na kuondokana na tatizo la kutegemea ajira chache kutoka
Serikalini. Serikali itaandaa sera nzuri za ajira na kuwashajiisha wawekezaji
kuweka kipaumbele katika kuajiri vijana wa Zanzibar.
USTAWI
WA WAZEE, WANAWAKE NA WATOTO
Mheshimiwa
Spika,
Wazee ni hazina kubwa kwa nchi yetu, na kwa
kutambua hilo, Serikali itaendelea kuwatunza wazee. Kwa wazee wanaoishi kwenye
nyumba za wazee za Sebleni, Welezo na Limbani, huduma za kuwapatia makaazi
bora, chakula na matibabu zitaendelea. Vile vile, huduma ya pensheni jamii kwa
wazee waliofikia umri wa miaka 70 na zaidi zitatolewa. Hapo baadae, Serikali
itaangalia uwezekano wa kushusha umri na kuongeza kiwango cha pensheni
inayotolewa sasa kwa mwezi.
Kwa
upande wa wanawake na watoto, Serikali imeazimia kuwasaidia wanawake wajane
ambao tayari wameshaunda rasmi jumuia yao. Wanawake hao watasaidiwa kwa
kuwezeshwa kiuchumi na kusimamia haki zao ikiwemo mirathi. Kadhalika, Serikali
itaendeleza juhudi zilizotangulia za kuwapatia wanawake na watoto haki zao zote
za msingi ili waishi vizuri katika jamii. Katika kulinda haki zao, Serikali
itaendeleza mapambano ya vitendo vya udhalilishaji wa watoto na unyanyasaji wa
kijinsia kwa nguvu zetu zote na kuhakikisha kwamba sheria zilizotungwa na
kupitishwa zinazolinda usalama na maslahi ya wanawake na watoto zinatumika ipasavyo,
na haki inatendeka.
WATU
WENYE ULEMAVU
Mheshimiwa Spika,
Kama
ilivyosisitizwa na kuelekezwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Serikali
itaweka kipaumbele maalum katika kuwashirikisha watu wenye ulemavu kwenye
shughuli mbali mbali za kiuchumi pamoja na kuzilinda na kuziimarisha haki zao.
Tutawawezesha kwa kuwapatia mitaji na mafunzo mbali mbali ya ujasiriamali bila
ya kuwabagua kijinsia au aina ya ulemavu walionao.
MAENEO MENGINE MTAMBUKA
Sanaa, Burudani na Michezo
Mheshimiwa
Spika,
Eneo jengine
ambalo tutalishughulikia ni sanaa, burudani na michezo. Mambo haya matatu yana
nafasi ya kipekee katika kuwaunganisha Wazanzibari, kuwatambulisha Wazanzibari
duniani na kukuza uchumi na kutoa ajira. Muziki wa Taarab, muziki wa kizazi
kipya na sanaa ya filamu kupita matamasha ya ZIFF na ‘Sauti ya Busara’
yameitangaza sana Zanzibar na kuwa na mchango wa kipekee. Naahidi kuyalea na
kuyakuza matamasha haya na mengine ili kutangaza hazina ya utamaduni na
ustaarabu wa Zanzibar ikiwa ni sehemu ya kukuza utalii, kipato na ajira.
Kwa upande wa
michezo, tutafanya mengi. Lakini kubwa sana na ambalo linalifadhaisha moyo ni
kupotea kwa msisimko wa Ligi ya Soka ya Zanzibar. Siku za nyuma, timu za
Zanzibar za Small Simba, Malindi,
Mlandege na KMKM zilikuwa
ni timu zenye sifa na kuchachafya timu za Bara na Afrika Mashariki. Tutawekeza
kwenye michezo katika kuibua, kulea na kuendeleza vipaji vya vijana. Hii
itakwenda sambamba na kukaa na wadau wa soka kutafuta jawabu la kuamsha
msisimko wa Ligi yetu ya Zanzibar. Azma yetu ni kuona Timu ya Taifa ya Zanzibar
inakwenda mbali katika kushiriki michuano ya Afrika ili kutumia vizuri fursa ya
uanachama wetu katika Shirikisho la Michezo la Afrika (CAF) ambayo tumeipigania
kwa miaka mingi.
Natambua kua
maendeleo ya michezo yanahitaji udhamini kutoka kwa wadau wa michezo. Naahidi
kujadiliana nao ili waweze kutoa udhamini kwa michezo yetu mbali mbali.
AMANI NA
UTULIVU
Mheshimiwa
Spika,
Mafanikio ya utekelezaji wa mipango na ahadi tulizozitoa,
hayawezi kupatikana bila ya kuendelea kuwepo kwa amani na utulivu nchini.
Jukumu la kulinda na kudumisha amani tuliyo nayo sio la vyombo vya ulinzi na
usalama peke yake. Huo ni wajibu wa kila mmoja wetu. Kuiharibu amani ni jambo
jepesi na la mara moja, ila kuirudisha ni vigumu na tujifunze kwa wengine
walioichezea tunu hii. Kwa hivyo, sote tuwe walinzi wa amani kwa kutambua kuwa
bila ya amani hakuna maendeleo. Serikali ya Mapinduzi ya Awamu ya 8
itashirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha
kuwa amani na usalama wa Watanzania na mali zao pamoja na wageni wote
wanaotutembelea nchini vinadumishwa na kulindwa.
HITIMISHO
Mheshimiwa Spika,
Kabla
sijamaliza hotuba yangu, nawashukuru tena wananchi wa Zanzibar kwa kutupa dhima
hii ya kuongoza nchi na Serikali. Tunatambua uzito wa dhamana tuliyoibeba kwa
wananchi ya kuwatumikia watu wote kwa misingi ya usawa. Nakuahidini kuwa
Serikali nitayoiunda itasimamia kwa weledi na umahiri mkubwa utekelezaji wa
ahadi zote tulizozitoa wakati wa kampeni kwa ufanisi huku tukizingatia kuwa
ahadi ni deni na wananchi wametuchagua kwa matumaini. Ni matarajio yangu kuwa
na nyinyi Waheshimiwa Wawakilishi mtazingatia wajibu wetu huu na Madiwani wetu
nao watazingatia kuwa uongozi tuliopewa ni dhamana ya kuwatumikia watu na sio
kwa maslahi yetu binafsi.
Kwa mara
nyengine, nakupongeza Mheshimiwa Spika, Naibu Spika, na Wajumbe wote wa Baraza
la Wawakilishi la Kumi la Zanzibar kwa heshima kubwa mliyopewa na wananchi ya
kuchaguliwa kuingia katika chombo hiki muhimu cha kutunga sheria ili
muwawakilishe. Matumaini yangu, mtaitumia vyema fursa hii kwa lengo la
kuchangia mipango ya maendeleo na kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbali mbali
zinazowakabili wananchi wetu kwa kusaidiana na Serikali yenu.
Namalizia
hotuba yangu kwa kuvishukuru vyombo vya habari vinavyowatangazia wananchi tukio
hili la uzinduzi wa Baraza. Kadhalika, nawashukuru wananchi wote wanaofuatilia
uzinduzi huu kupitia vyombo vya habari. Tumuombe Mwenyezi Mungu aizidishie nchi
yetu amani, umoja na mshikamamo. Mola atuwezeshe kuitekeleza mipango yetu ya
maendeleo kwa ufanisi. Nakutakieni nyote kila la heri na mafanikio.
Baada ya kusema hayo, na kwa mamlaka niliyo nayo ya
kikatiba kama yalivyoainishwa katika Ibara ya 91 kifungu (1), sasa natamka kuwa
Baraza la Kumi la Wawakilishi la Zanzibar limezinduliwa Rasmi leo tarehe 11
Novemba, 2020.
MUNGU IBARIKI ZANZIBAR,
MUNGU IBARIKI TANZANIA,
MUNGU IBARIKI AFRIKA.
No comments:
Post a Comment