Habari za Punde

Risala ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Hussein Ali Mwinyi ya Mwaka Mpya Kwa Wananchi wa Zanzibar na Tanzania.

 
           Assalamu Aleikum Warahmatullah Wabarakatuh

Kila sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu. Tunamshukuru Yeye kwa kutuwezesha kufika siku hii ya leo ambapo tunauaga mwaka 2020na baada ya masaa machache tutaukaribisha mwaka mpya 2021.

Tuliuanza mwaka 2020 tukiwa pamoja na wenzetu ambao leo hii hatunao tena, kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, wameshatangulia mbele ya haki.  Tumuombe Mola wetu awape malazi mema peponi na sisi tulio hai atujaalie kila la kheri katika maisha yetu hapa duniani na atupe hatma njema. Amin!

Ndugu Wananchi,

Kipindi cha mwaka mmoja ni kirefu katika maisha ya mwanadamu.Ndani ya kila mwaka hutokea mambo mengi makubwa ambayo, baadhi yao, huacha alama  na kumbukumbu za historia katika ngazi ya kimataifa, kitaifa na  hadi ngazi ya familia na mtu mmoja mmoja.  Bila ya shaka, mambo yote  hayayametokea  katika mwaka 2020 ambao leo tunauaga.

Kwa ngazi ya Kimataifa, moja kati ya mambo makubwa yaliyotokea katika mwaka 2020 ni  kuenea na  kusambaa kwa maradhi ya Virusi vya Korona (COVID - 19)  ambayo yalijulikana na  kutangazwa rasmi mwezi wa Disemba, 2019.

Athari za maradhi ya COVID – 19kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii ni kubwa. Yamezusha hofu na taharukiisiyomithilika;bado athari zake zimegubika nyanja zote za maendeleo ya karne hii ya 21. Mataifa mengi duniani, hasa Ulaya na Amerika, yamekuwa yakiweka na kuondoa karantini, ambazo zinaathari kubwa kwa mwenendo wa watu bidhaa na huduma hali ambayo inaendelea kuathiri uchumi wa dunia.Wiki mbili zilizopita taharuki imeongezeka baada ya  kuzuka kwa aina mpya yaVirusi vya Korona nchini Uingereza. Hadi  tarehe 30 Disemba 2020 idadi ya watu walioambukizwa duniani imeshafikia  milioni 81 na idadi ya vifo ni milioni 1.8. Nchi yetu inafuatilia kwa karibu habari hizi ili iwe inachukua hatua zinazofaa.

Athari za maradhi COVID - 19 kwa nchi za  visiwa ni kubwa zaidi  kutokana na utegemezi wa sekta za huduma, hasa utalii, kwa maendeleo ya kiuchumi; hali hiyo kama tunavyoendelea kushuhudia imejitokeza hapa Zanzibar. 

Kwa hivyo tunauaga mwaka huu ikiwa  kasi ya ukuaji wa uchumi wetu imeathirika sana kutokana na maradhi hayo.  Ni vyema tukachukua changamoto zilizojitokeza kutokana na maradhi ya COVID -19 tukazifanyia kazi ili zisiendelee kuathiri kasi  yetu ya utendaji na uwajibikaji.  Kamwe, isiwe kwamba  kuendelea kuwepo kwa maradhi ya COVID 19 katika mataifa mengine kuwa  kisingizio au  kikwazo kwa kila kitu tulichopanga kufanya kwa maendeleo yetu.  

Ndugu Wananchi,

Kwa ngazi ya Kitaifa,  tutaukumbuka mwaka huu 2020 kwa tukio la kuondokewa na  Kiongozi wetu Mpendwa, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Marehemu Benjamin Mkapa ambae alifariki tarehe 24 Julai, 2020 na kuzikwa tarehe 29, Julai,2020 kijijini kwao Lupaso Mkoani Mtwara. Tunamuomba Mwenyezi Mungu ampe malazi mema.

Vile vile, matukio mengine makubwa ya kukumbukwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni  zoezi la Uchaguzi Mkuu ambalo limefanyika kwa hali ya  amani na utulivu na hatimae  kumuwezesha Mheshimiwa Dk. John Pombe Joseph Magufuli kuendelea kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kipindi cha Pili cha Serikali ya Awamu ya Tano anayoiongoza.

Watanzania tunaendelea kuukumbuka  mwaka 2020 kwa maendeleo makubwa ya kiuchumi tuliyoyapata  ndani ya mwaka huu chini ya Uongozi wa Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli.Benki ya Dunia ilitangaza  rasmi kwamba  Tanzania imeingia katika uchumi wa kipato cha kati ngazi ya chini kuanzia Julai mosi, 2020 tarehe ya kwanza ya mwaka mpya wa fedha. Mafanikio hayo, yameiwezesha nchi yetu kujiunga namataifa saba ya Afrika  yaliyoKusini mwa Jangwa la Sahara yenye  hadhi hiyo.Tujipongeze kwa kupiga hatua hiyoukizingatiwa  kwamba kwa mujibu wa Dira ya Maendeleo ya Tanzaniaya 2025, ilitarajiwa kwamba tutafikia kiwango hicho ifikapo mwaka 2025. Bila ya shaka,  hili ni jambo kubwa la kukumbukwa kwa mwaka huu 2020 tunaouaga.

Ndugu  Wananchi,

Kwa upande wa Zanzibar,  yako matukio mengi ya  kihistoria  ambayo yatatufanya tuukumbuke mwaka huu 2020.Tutaukumbuka kwa tukio lililotokea katika Mji Mkongwe wiki iliyopita, tarehe 25 Disemba, 2020 siku ya Krismas  la kuanguka sehemu kubwa ya Jengo la ‘Beit El Ajaib’ na kusababisha vifo vya ndugu zetu wawili  baada ya kufukiwa na kifusi na wengine kadhaa kujeruhiwa.  Vifo hivi vimeleta mshtuko kwa wananchi wa Zanzibar. 

Tunamuomba Mwenyezi Mungu azilaze mahala pema peponi roho za marehemu wote.  Kwa mara nyengine, tunatoa mkono wa pole kwa familia za marehemu. vile  vile, tunamuomba Mwenyezi Mungu awape uzima na nguvu za kuendelea na maisha ya kawaida wale wote walioumia kutokana na ajali hiyo.

Kwa upande  mwengine, tumehuzunika kutokana na kuharibika kwa jengo la Beit El Ajaib, ambalo ni mithili ya uso wa Mji wetu Mkongwe ambao tunaupenda na unapendwa duniani kote kutokana na Historia yake na uzuri wake.

Kwa hivyo, kwa pamoja, azimio letu la mwaka mpya 2021, liwe ni kuungana katika kutafuta njia bora na endelevu za kuulinda na kuuhifadhi Mji Mkongwe, ikiwa ni pamoja na kuyatekeleza mapendekezo yote yaliyotolewa katika mkutano tulioufanya juzi tarehe 28 Disemba, 2020 baina ya Viongozi wa Serikali na Wadau mbali mbali wa Mji Mkongwe kwa lengo la kutafuta njia bora za kuuhifadhi na kuuendeleza.  Tunamuomba Mwenyezi Mkungu atupe wepesi katika kutekeleza mambo hayo mema tuliyoyadhamiria.

Vile vile,  tutaukumbuka mwaka 2020 kwa kufanya Uchaguzi Mkuu na kufanikisha zoezi  hilo muhimu  kwa salama na amani.Katika mwaka huu tumeshuhudia kumalizika muda wa uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Awamu ya Saba iliyokuwa ikiongozwa na Rais Mstaafu Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein na kuanza kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya  Awamu ya Nane ninayoiongoza mimi. Tumeshuhudia tena historia na sifa ya nchi yetu ya kubadilishana madaraka na nafasiza uongozi kwa hali ya amani na utilivu.

Katika kipindi cha uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Awamu ya Saba tumeshuhudia maendeleo makubwa ya kiuchumi yakiwemo kukamilika kwa miradi mingi mikubwa  ya ujenzi wa miundombinu, skuli za ghorofa,  majengo ya Ofisi, makaazi  na maduka ya kisasa pamoja na miradi ya usambazaji wa maji safi na salama.

Kati ya miradi hiyo,imo miradi ya jengo la Abiria la Terminal IIIkatika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa, wa Abeid Amani Karume, Maduka ya Michenzani  (Michenzani Shopping Mall) na barabara mbali mbali za Unguja na Pemba zilizojengwa kwa kiwango cha lami.

Mwaka 2020, vile vile, utakumbukwa kwa kuwa ni mwaka ambao Zanzibar imekamilisha utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2020 na kufikia lengo la kiwango cha nchi zenye kipato cha kati(Low Middle Income Status)  kwa kuzingatia vigezo vya kiuchumi vilivyowekwa  na  Jumuiya za Kimataifa.

Ndugu  Wananchi,

Tunaukamilisha mwaka 2020 ikiwa tumeshatumia miezi miwili ya mwanzo ya Uongozi wa Serikali,  katika kipindi hiki tumeunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa kama Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 inavyoelekeza na viongozi wa kushika nyadhifa mbali mbali wameshateuliwa. Moja kati ya malengo ya kuwekwa mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ni kuimarisha umoja na mshikamano  miongoni mwa wananchi wa Zanzibar.

Nasaha zangu hivi sasa ni kwamba sote tuuanze  mwaka mpya 2021 kufanyakazi kwa ari mpya na kuiunga mkono Serikali kwa yale mambo yaliyopangwa kutekelezwa. Mapinduzi makubwa ya kiuchumi tuliyodhamiria kuyafanya katika uchumi wa buluu, ujenzi wa miundombinu, uwekezaji, utalii, biashara, ujenzi wa viwanda, kilimo, uvuvi, ufugaji, elimu, afya, usambazaji wa maji safi na salama na  uwezeshaji wa wananchi tutayafikia ikiwa kila mmoja atafanya kazi kwa bidii na kutekeleza wajibu wake.

Tuunge mkono juhudi za Serikali katika kupambana na rushwa, wizi, ubadhirufu wa mali ya umma na uzembe katika sehemu zetu za kazi. Tuiunge mkono Serikali katika utekelezaji wa mipango ya kukomesha udhalilishaji wa watoto na unyanyasaji wa kijinsia.

Mwaka 2021 uwe ni mwaka wa kuwa na mipango imara ya  usafi wa miji yetu na uhifadhi wa mazingira. Kwa pamoja, tuhimizane matumizi bora ya ardhi na tushirikiane katika kuitatua migogoro ya ardhi iliyopo na itakayojitokeza.

Ndugu Wananchi,

Ikiwa ni sehemu ya Shamra shamra za Sherehe za maadhimisho ya miaka 57  ya Mapinduzi ya Zanzibar, kesho tarehe 01 Januari, 2021 tutafanya Bonanza la Mazoezi ya viungo. Tutaanza na  matembezi  yatakayoishia katika Viwanja vya Amani kwa hapa mjini Unguja. Nawaalika wananchi  mushiriki katika matembezi hayo, na wale watakaokosa nafasi ya kushiriki wafanye mazoezi katika  Mikoa na Wilaya zao. Sote tushiriki katika shamra shamra za Sherehe za  Mapinduzi kwa namna mbali mbali ili kuzienzi na kuziendeleza  fikra na mawazo ya waasisi wa Mapinduzi na Viongozi mbali mbali walioiongoza nchi yetu katika kipindi hiki cha miaka 57.

Ndugu Wananchi,

Nafahamu kwamba usiku wa kumkia mwaka mpya huwa ni usiku wa  furaha. Nawasihi wananchi tufurahie kuingia kwa mwaka mpya  tukizingatia Sheria  na kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani.

Namalizia risala yangu kwa kutoa salamu za mwaka mpya kwa wananchi wote wa Tanzania. Kadhalika, natoa salamu kwa viongozi wa nchi marafiki, Taasisi za kimataifa na washirika wetu mbali mbali wa maendeleo. Tunamuomba   Mola wetu aujaalie kheri na baraka nyingi mwaka mpya wa 2021. Tunamuomba atuzidishie neema na baraka na adumishe umoja na mshikamano uliopo.

                                                 Mungu Ibariki Zanzibar

Mungu Ibariki Tanzania

Ahsanteni kwa kunisikiliza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.