Na Ramadhani Ali – Maelezo 31.12.2020
Tamasha la saba la Biashara la Zanzibar linatarajiwa kuanza tarehe 4 na kumalizika tarehe 15 Januari 2021 katika Viwanja vya Maisara Mjini Zanzibar.
Akizungumza na Waandishi wa Habari katika viwanja vya Maisra baada ya kukagua maandalizi ya Maonyesho hayo, Kaimu Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda, Mudrik Ramadhani Soraga amesema kuwa zaidi ya wafanyabiashara na wajasiriamali 340 wa ndani na nje ya nchi wamethibitisha kushiriki Tamasha hilo.
Alisema madhumuni makubwa ya Tamasha la Biashara la Zanzibar ni kutoa nafasi kwa wajasiriamali na Wafanyabiashara kutangaza bidhaa na huduma zao ndani na nje ya nchi ili kupata masoko ya uhakika ya bidhaa zao.
Kaimu Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda alibainisha kuwa Tamasha ni njia moja ya kukutana na wanunuzi wa bidhaa ama huduma wanazotoa ana kwa ana, kwani ukuaji wa sekta ya biashara ndio chanzo cha kuongeza ajira na kunyanyua pato la wananchi na Taifa kwa jumla.
Alieleza kuwa Tamasha la Biashara litaweka jukwaa kwa ajili ya kutangaza Uchumi wa Bluu pamoja na kuwa na siku ya maalum ya ubunifu yenye lengo la kuibua vipaji vya wajasiriamali.
Akitaja mafanikio ya yaliyopatikana katika Tamasha la sita, Kaimu Waziri alisema jumla ya wafanyabiashara na wajasiriamali 398 kutoka ndani na je ya Zanzibar walishiriki na inakisiwa kulikuwa na mauzo ya zaidi ya shilingi milioni 954.7 yalifanyika katika kipindi hicho
Waziri Soraga alisema Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan atalifungua rasmi Tamasha la saba la Biashara la Zanzibar tarehe 6 Januari 2021katika viwanja vya Maisara.
No comments:
Post a Comment