Habari za Punde

Watanzania Tujivunie Matunda Ya Muungano - Waziri Ummy

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa  Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu akipata maelezo juu ya Ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kianga kutoka kwa Mkurugenzi wa Uratibu shughuli za Serikali – SMZ Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Bw. Khalid Khalid Hamrani Mkurugenzi, hii leo Zanzibar. Kushoto ni Mjumbe wa Baraza la Uwakilishi (Mwera) Mhe. Mihayo Juma N’hunga na wa pili kulia ni Mbunge wa Jimbo la Mwera Mhe. Zahor Mohamed Haji

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa  Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu akipata maelezo juu ya Ujenzi wa Bwalo la Mitihani kwa wanafunzi (halipo pichani) kutoka kwa Mkurugenzi wa Uratibu shughuli za Serikali – SMZ Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Bw. Khalid Khalid Hamrani Mkurugenzi, hii leo Fujoni Zanzibar.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa  Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu akiongea na wananchi  na wafanya biashara katika soko la Kinyasini ikiwa ni moja miradi ya Muungano inayotekelezwa pande zote. Waziri Ummy ametoa rai kwako kujuvunia matunda ya Muungano.

 Na Lulu Mussa  

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Ummy Mwalimu amesema watanzania wote wanao wajibu wa kujivunia matunda ya Muungano ikiwa ni pamoja na miradi ya Maendeleo inayotekekezwa pande zote mbili za Muungano.

 

Akiwa visiwani Zanzibar katika siku yake ya pili ya ziara ya kikazi, Waziri Ummy ametembelea miradi ya TASAF na MIVARF ikiwa ni pamoja na Kituo cha Afya Kianga, Bwalo la Wanafunzi na Soko la Mbogamboga la Kinyasini.

 

Amesema pamoja na changamoto zilizopo zipo fursa kwa Watanzania kujiletea maendeleo na ustawi wao, kwa kuwa kuwepo kwa fursa hizo kumeleta tashwishi na matarajio makubwa kwa wananchi katika kuendeleza mafanikio yaliyopatikana na kuchochea mafanikio katika maeneo mengine kwa maslahi ya Taifa

 

“Tumejionea wenyewe mpango huu mkubwa wa kunusuru kaya maskini kupitia  Muungano wetu unatekelezwa na pande zote mbili na haya ndio matunda ya Muungano kuhakikisha miradi mikubwa inatekelezwa pande zote mbili” Ummy alisisitiza.

Aimetaja baadhi ya Miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali zeto mbili  yenye kunufaisha wananchi wake iko katika Nyanja za  Elimu; Afya; Masoko; Maji; Mazingira pamoja na Usafiri na Usafirishaji.

“Kama mnavyofahamu tunataka kuulinda, kudumisha na kuuimarisha muungano wetu  kwani ndio umoja wa watanzania, ndio usalama wa watanzania na ndio amani ya watanzania wote” Alisisitiza Mhe. Waziri

Kupitia mradi wa MIVARF takriban masoko 16 yamejengwa Tanzania nzima kati ya hayo masoko 4 yamejengwa Zanzibar, kituo cha afya Kianga chenye kunufaisha takriban Shehia 3 za Kianga, Dole na Mazizini  huku kikihudumia takribani wakazi 19,840, ujenzi wa madarasa katika Skuli za Fujoni na Mahonda ambazo zimeweza kutatua changamoto za elimu.

Waziri Ummy Mwalimu amesema kuwa ni vyema tukatumia ipasavyo fursa zilizopo Tanzania Bara na Zanzibar kwa kuleta maendeleo yatakayoinua hali ya uchumi wa Watanzania, na kutoa rai ya kuulinda, kuuimarisha na kuudumisha Muungano wetu kwani ni dira ya mafanikio yetu.

Kwa upande wake Mjumbe wa Baraza la Uwakilishi (Mwera) Mhe. Mihayo Juma N’hunga ameshukuru Serikali kwa kupata kusogeza huduma zenye kugusa Maisha ya wananchi.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.