Habari za Punde

Hayati, JPM na Mradi Mkubwa wa Nishati, Wa Ndoto ya Baba waTaifa (JKN) kuweka Nchi katika Uhuru wa Kiuchumi. . Bwawa kuzalisha umeme wa MG 2,115 . Mradi utagharimu TZS trilioni 6.5

 Na. Paschal Dotto-MAELEZO

“Kama maendeleo ya kweli yatachukua nafasi ni lazima watu washiriki katika kujenga maendeleo hayo”. Ni kauli ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere  kuhimiza wananchi kushiriki katika ujenzi wa Taifa kwani nchi haijengwi na mtu mmoja, na  waswahili husema ‘kidole kimoja hakivunji chawa’.

Hayati,  Dkt. John Pombe Magufuli alipenda kutumia msemo usemao ‘kawia ufike, tumeamua tufike ni kauli ambayo alikuwa akiitumia  Katika kuchukua dira ya kujenga uchumi wa kati kwa wananchi wake, Hayati Dkt. Magufuli alichukua  dhamira ya kweli ya kuleta mapinduzi ya uchumi katika ngazi zote nchini, na hasa alitaka kuona Tanzania ikiwa na umeme wa kutosha utakaoweza kuendesha miradi mikubwa kama ule wa Reli ya Kisasa (SGR) mradi unaojengwa kutoka lango la uchumi Mashariki wa Tanzania hadi lango la uchumi Kanda ya ziwa.

“Duniani tuna nukuu (quotes) za watu maarufu kama Martn Luther King, Jr. Abraham Lincoln na wengine wengi. Kwa hapa kwetu tuna nukuu za Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, Sasa ni wakati mwafaka kuweka nukuu zake kwenye uzi huu, usihofu iwe mbaya masikioni mwako au iwe nzuri wewe weka tu maana lolote analo litamka Mkuu wa nchi linapaswa kutunzwa”,  Ni kauli ambazo zilitoka kwa uzalendo mkubwa kutoka kwa  Rais wa Awamu ya Tano, Tanzania Hayati, Dkt.John Pombe Magufuli.

Maana  hata Biblia katika kitabu cha Mithali sura ya 13:10, inasema “kiburi huleta mashindano tu, bali hekima hukaa nao wanaoshauriana,” hii ni kauli ambayo inatoa mwelekeo mmoja kwa watu  wote kusikilizana na kujua njia sahihi ya  kuelekea kwa hiyo Watanzania hatuna budi kujenga utamaduni wa kufanya kazi na kutekeleza majukumu kwa kufuata ushauri wa viongozi.

Katika hotuba mbalimbali, Hayati, Dkt. Magufuli alikuwa akisisitiza nia ya kuendeleza ndoto za Mwasisi wa Taifa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage  Nyerere ikiwemo ndoto ya kuhamia Dodoma makao makuu ya nchi na ujenzi wa bwawa kubwa la umeme, Nyerere Hydro Power Project (NHPP) katika mto Rufuji litakalogharimu shilingi  trilioni 6.5.

Katika ukuaji wa nishati nchini ilikuwa ni dhamira ambayo inaendana na Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano “Tanzania ya viwanda”. Moja ya ndoto kubwa ya Baba wa Taifa ilikuwa ni ujenzi wa bwawa hilo litakalo  zalisha Megawati 2,115 ili kuiwezesha Sera hiyo kufikiwa kwa uhakika zaidi na hapo mawazo yake yalikuwa sahihi kama Hayati, Dkt. Magufuli alivyona akajenga mradi mkubwa wa Reli ya kisasa (SGR) kilomita 1,200 inayogharimu shilingi  trilioni 7.

“Kama tumeamua kujenga nchi kwa ajili ya viwanda ni lazima tufanye uwekezaji wa kutosha katika sekta ya nishati hasa kwenye umeme wa maji (Hydroelectric Power) na hii itakuwa njia sahihi kwa ukuaji wa viwanda vyetu, lakini pia itatusaidia kwenye uwekezaji wa miundombinu kama ya reli zinazotumia umeme”,  Hayati, Dkt.  Magufuli.

“Ukitaka kuruka agana na nyonga,” hii ni kauli ambayo inasisitiza maandalizi ya kufanya kitu hususani katika kufanya mapinduzi ya uchumi, katika Miradi hii mikubwa lazima wananchi wote wanapaswa kujiandaa ili kuwa na mwelekeo mmoja katika kutimiza azma hiyo ya kutengeneza nchi kwa vizazi na vizazi.

“Ninafahamu kuwa umeme huu wa Steiglers Gorge (JNHPP) utapata mapingamizi mengi, lakini nawaomba Watanzania tusimame imara katika kuhakikisha mradi huu unafanikiwa, kwa sababu ndiyo yalikuwa mawazo ya Baba wa Taifa aliona mbali katika maendeleo ya nchi yetu,” alisisitiza Hayati, Dkt.  Magufuli.

Nchi nyingi za Afrika sasa zimedhamiria kujenga na kuimarisha sekta ya nishati kupitia vyanzo vya maji, Ethiopia ambao walitusaidia  katika  ushauri wa mradi huu mkubwa wenyewe wana nishati ya kutosha katika masuala ya nishati kwa hiyo ujenzi wa mradi huu utainua sekta ya nishati na kukuza uchumi kwa wananchi kwani bei ya umeme itashuka kwa hiyo Watanzania wanatakiwa kutoa ushirikiano kwa mradi huo wa JNHPP kwani ndio mradi mkubwa wa nishati na  utakuwa na umeme wa uhakika

Mathalani katika hotuba yake,  Hayati, Dkt. Magufuli na wataalamu wa nishati kutoka Ethiopia alisema kuwa taifa hilo lina wataalamu wengi na kuna mabwawa mengi ya Gibe 2 na 3 na lingine kubwa ambalo linajengwa linalotarajia kuzalisha megawati 6,000, hivyo Tanzania haina budi kujenga bwawa la JNHPP lenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115.

Katika harakati hizi nzuri kwa Taifa la Tanzania wazo hili ni muhimu kutekelezwa ili kuleta maendeleo katika maeneo mengi pamoja na kumuenzi Baba waTaifa kwa kuanzisha wazo hili.

“Tumeona twende na mawazo mazuri yaliyowekwa  na Hayati Baba wa Taifa Julius Kambarage Nyerere  tokea miaka ya 1972 na 1975 alipoamua kuunda sheria ya kuanzisha RUBADA kwa lengo la kuhakikisha kuwa Steiglers Gorge (JNHPP), inajengwa kwa manufaa mapana ya nchi yetu”, alifafanua Hayati, Dkt.  Magufuli.

Mradi huo mkubwa utagharimu shilingi za Kitanzania trilioni 6.5, ambazo zitatolewa na Serikali ya Tanzania na lengo la Serikali ni kufikia megawati 5,000 ili kuwezesha wananchi kuwa na nishati ya kutosha kutoka vyanzo mbalimbali, pia Serikali inalenga kufikia  megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025 kama Sera ya nishati ya mwaka 2015 inavyoeleza kuelekea uchumi wa viwanda.

Katika tafiti zilizopo nchini zinaonesha kuwa, Tanzania inaweza kuzalisha megawati 4,700 kutoka katika vyanzo vyake vya maji, mradi huo mkubwa utawezesha wananchi katika eneo husika kupata mahitaji mengine kama alivyoelezea  Hayati, Dkt. Magufuli.

“Tukijenga mradi huu tutategemea kuwa na eneo la ziwa la maji mengi ambalo litatumika kwa uvuvi, wanyama wetu kunywa maji, litakuwa eneo zuri kwa utalii, kilimo cha umwagiliaji, maji ya kunywa kwa wananchi pamoja na umeme megawati 2,115  utakaotolewa na bwawa hilo kwa hiyo ni mradi mzuri wenye fursa nzuri za kiuchumi kwa  Wananchi,” alisisitiza Hayati, Dkt. Magufuli.

Kwa nchi kama Tanzania yenye vyanzo vingi vya nishati, Serikali inawashauri wananchi kutoa ushirikiano wa kutosha ili kuweza kuingia katika mapinduzi hayo akieleza kuhusu vyanzo hivyo  Hayati, Dkt. Magufuli alisema kuwa..

“Kuna maeneo mengi na vyanzo vingi sana  vya nishati Uranium ipo tu, Makaa ya mawe tani 1.9 milioni, gesi ujazo wa  trilioni 57.25 pamoja na upepo kwa maeneo ya Singida kwa hiyo tumeanzia kwanza kwenye ndoto ya Baba wa Taifa ya ujenzi wa wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP), kwa hizo megawati 2,115 na tutaendelea kujenga vituo vingine kwa sababu wataalam wapo.”

Sekta ya nishati ni muhimu kwa maisha ya wananchi wote kwa hiyo inatakiwa kuungwa mkono kwa asilimia 100 na kusiwepo na lugha ya kutofautiana maana ndiyo sekta itakayotufikisha kwenye ndoto yetu ya uchumi wa viwanda kwa sababu  kwenye kuwekeza miradi mikubwa inafaa zaidi kwa manufaa ya milele.

Hivi karibuni, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa alitembelea na kujionea maendeleo ya ujenzi wa mradi huo ambapo aliwaeleza Watanzania kutokuwa na hofu juu ya mradi huo ambao Serikali imewekeza ili kulete uhuru wa kiuchumi kwa Taifa na Serikali kwa ujumla.

“Wataalam Wetu wametuambia kwa kasi ya mradi tuna matumaini kuwa ifikapo Juni mwaka 2022 mradi utakuwa umekamilika, kwa sababu maeneo makubwa na nyeti ya mradi huu yamefikiwa kwa asilimia 47, na Serikali itaendelea kutoa fedha kukamilisha mradi huu. Bwawa hili litatoa Megawati 2,115 ambazo zikijumlishwa na Megawati 1,500 zinazozalishwa na vyanzo mbalimbali hivi sasa zitaifanya Tanzania kuwa na umeme toshelevu”, Mhe. Kassim Majaliwa.

 Alibainisha kuwa lengo kuanzisha mradi huo ni moja ya juhudi za Serikali za kupunguza gharama za umeme kwa wananchi kwa sababu uzalishaji wake ni wa gharama nafuu, uniti moja ya umeme unaozalishwa kwa kutumia maji unagharimu shilingi 36 hadi shilingi 50.

Aidha, Majaliwa alieleza gharama za umeme unaozalishwa kutoka katika kila chanzo cha uzalishaji umeme ikiwemo upepo shilingi 103.5, jua shilingi 103.5, makaa ya mawe shilingi 114, jotoardhini shilingi 118, nyuklia shilingi 65 na gesi shilingi 147 huku umeme wa maji gharama yake ikiwa ni ndogo kuliko zote yaani shilingi 36, hivyo amewaomba wananchi waondoe hofu juu ya utekelezaji mradi huo kwani utakamilika kwa wakati.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani Jumatatau ya Tarehe 12, 2021 alilieleza Bunge kuwa Novemba mwaka huu Bwawa la kuzalisha umeme (JNHPP), litaanza kujazwa maji rasmi na hapo ndiyo ndoto ya Hayati, Dkt. John Magufuli itaanza kutimia kuelekea uhuru wa uchumi alioutaka kwa Watanzania.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.