Habari za Punde

Tanzania Yapokea Nyongeza ya Euro Milioni 4 Kutoka Ubelgiji Kwa Ajili ya Mradi wa Maji Kigoma.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba, akizungumza wakati wa halfa ya utiaji saini mkataba wa marekebisho ya nyongeza ya kiasi cha Euro milioni nne kwa ajili ya kutekeleza wa mradi wa maji mkoani Kigoma, kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Ubelgiji Jijini la Dodoma. Kulia ni Balozi wa Ubelgiji nchini, Mhe.  Peter Van Acker.
Balozi wa Ubelgiji nchini, Mhe.  Peter Van Acker, akizungumza wakati wa  akizungumza wakati wa halfa ya utiaji saini mkataba wa marekebisho ya nyongeza ya kiasi cha Euro milioni nne kwa ajili ya kutekeleza wa mradi wa maji katika  Mkoa wa  Kigoma, kati ya Serikali ya Tanzania na Falme za Ubelgiji Jijini la Dodoma.

Ujumbe kutoka Tanzania ukiongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe kutoka Serikali ya Ubelgiji  ukiongozwa na  Balozi wa Ubelgiji nchini, Mhe.  Peter Van Acker, (wapili kulia) baada ya halfa ya utiaji saini wa mkataba wa marekebisho ya nyongeza ya kiasi cha Euro milioni nne kwa ajili ya kutekeleza wa mradi wa maji katika Mkoa wa Kigoma, jijini Dodoma.

 (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango – Dodoma)

Na, Farida Ramadhani

Serikali ya Tanzania imepokea nyongeza ya kiasi cha Euro milioni nne kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa maji mkoani Kigoma kutoka Serikali  ya Ubelgiji.


Hafla fupi ya utiaji saini wa mkataba wa marekebisho ya nyongeza ya mradi huo ilifanyika jijini Dodoma kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Emmanuel Tutuba kwa upande wa Serikali na Balozi wa Ubelgiji nchini, Bw. Peter Van Acker.


Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba alisema mradi huo ambao ulianzishwa kwa ajili ya Wilaya zote sita za Mkoa wa Kigoma, mwanzoni ulitarajiwa kugharimu Euro milioni nane.


“Sasa hizi Euro milioni nne zitakwenda kuongezea na kufanya jumla ya Euro milioni 12 sawa na takribani Shilingi bilioni 33 za kitanzania ambazo zitatumika kwa ajili ya kuongeza upatikanaji wa maji maeneo ya vijijini na mijini mkoani humo”, alifafanua.


Alisema katika Mkoa wa Kigoma, Serikali ya Ubelgiji pia imefadhili mradi mwingine wa kilimo ambao unaendelea na umegharimu Euro milioni nane sawa na takribani Shilingi bilioni 22, hivyo miradi yote miwili (mradi wa maji na kilimo) inagharimu jumla ya takribani Shilingi bilioni 55.


Aidha aliipongeza Serikali ya Ubelgiji kwa kubuni njia nzuri ya kupunguza gharama za utekelezaji wa mradi wa kilimo kwa kujenga madaraja ya mawe ambayo yanaweza kuunganisha sehemu ya mashamba na sehemu ya makazi na kupunguza gharama za ujenzi wa daraja moja kwa takribani asilimia 80.


Bw. Tutuba aliihakikishia Serikali ya Ubelgiji kuwa fedha hizo zitatumika kikamilifu na utekelezaji wa miradi hiyo utakamilika kwa wakati.


Naye Balozi wa Ubelgiji nchini, Bw. Peter Van Acker alisema Serikali ya nchi yake itaendeleza ushirikiano na Tanzania kwa kuendelea kufadhili miradi mbalimbali ya maendeleo.


Alisema anaamini mradi wa maji mkoani Kigoma utatatua changamoto ya maji mkoani humo na ameahidi kuwajibika katika masuala ya maji kama hotuba ya Mhe. Rais, Samia Suluhu Hassan ilivyosisitiza.


Akipokea kwa shukrani nyongeza hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga, aliishukuru Serikali ya Ubelgiji kwa kuendeleza ushirikiano mzuri na Tanzania na kubainisha utekelezaji wa mradi wa maji mkoani Kigoma utanufaisha watu takribani laki moja na 30.


Aliahidi kusimamia matumizi ya fedha hizo kikamilifu ili kuhakikisha malengo ya utekelezaji wa mradi huo yanatimia kwa wakati.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.