Habari za Punde

Jumla ya ajali 18 zaripotiwa mwezi wa Mei 2021

 Na Mwashungi Tahir    Maelezo   15-6-2021

Imeelezwa kwamba jumla ya ajali 18 zimeripotiwa mwezi Mei ,2021 ambapo Wilaya ya Magharibi ‘A’ imeripotiwa kuwa na ajali nyingi zaidi ambazo ni 4, ikifuatia Mjini na  Micheweni ajali 3  kwa kila Wilaya.

Akiwasilisha takwimu za ajali na makosa ya barabarani Mtakwimu kutoka katika kitengo cha Makosa ya jinai , Madai na Jinsia  Asha Mussa Mahfoudh wakati alipokuwa akiwasilisha kwa   waandishi wa habari huko katika ofisi za mtakwimu ilioko Mazizini .

Amesema Mlinganisho wa idadi ya ajali za barabarani kwa mwezi uliopita zimepungua kwa asilimia 10.0 kutoka ajali 20 kwa mwezi wa April hadi ajali 18mwezi wa Mei 2021.

Pia amesema Mlinganisho  wa ajali za barabarani kwa mwaka zimeripotiwa mwezi wa Mei,2021 zimepungua kwa asilimia 40.0 kutoka ajali 30 mwezi Mei,2020 hadi ajali 18 mwezi wa Mei,2021.

Aidha amesema idadi ya waathirika wa ajali za barabarani jumla 28 wameripotiwa mwezi Mei, 2021ambapo 24 wanaume na 4 wanawake , Wilaya ya Wete imeripotiwa kuwa na waathirika wengi ambao ni 10 asilimia 35.7 ikifuatiwa na Wilaya ya Kati waathirika 6 sawa na asilimia 21.4.

Aidha amesema ajali nyingi kwa mwezi wa Mei,2021 zilitokea muda wa saa 3.01mpaka saa 6.00 usiku ajali 4 ikifuatiwa muda wa saa 3.01 mpaka saa 6.01, mpaka saa 9.00 jioni na 9.01 mpaka saa 12.00 jioni ajali 3 kwa kila masaa.

Pia amesema kwa upande wa makosa ya barabarani jumla ya makosa 1,256 yameripotiwa mwezi wa Mei,2021 ambapo makosa yote 1,256 yamefanywa na wanaume . Wilaya ya Kati ina idadi kubwa ya makosa ya barabarani makosa 347 sawa na asilimia 27.6 kati ya makosa yote yaliyoripotiwa ambapo Wilaya ya Kusini ina idadi ndogo ya makosa ya barabarani yaloripotiwa ambayo ni makosa 21 asilimia 1.7.

Vile vile ameelezea kosa kuu lililoripotiwa kwa mwezi  wa Mei,2021 ni kuzidisha idadi ya abiria na mizigo makosa 325, kutofuata miongozo ya kanuni za usalama barabarani makosa 265 na kuendesha chombo cha moto gari,vespa,pikipiki ,fifti bila ya leseni makosa 213.

Orodha ya makosa haya matatu 3 ya barabarani kati ya yote kumi yaliyoripotiwa yamechangia asilimia 63.9

Nae Koplo Ali Abdullah Juma  kamanda wa kikosi cha usalama barabarani Makao Makuu ya Polisi amesema jitihada zaidi zinahitajika kwa kutoa elimu kwa madereva wanaotumia pikipiki na wanaoendesha baiskeli kuzingatia sheria za barabarani  na kutoa wito kuwa waangalifu wanapotumia barabara ili kuweza kupunguza ajali.

Kwa upande wake Mrakibu Msaidizi wa Polisi Ramadhani Himidi Haji Mkuu wa Kitengo cha Takwimu , Makao Makuu ya Polisi Zanzibar ametoa wito kwa madereva  na watumiaji  barabara kutii sheria bila ya shuruti kama inavyotakiwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.