Na Jovina Bujulu-BAKITA
Kiswahili ni miongoni mwa lugha kumi zinazotumiwa na watu wengi duniani. Chimbuko la lugha hii ni Tanzania na inakadiriwa kutumiwa na watu zaidi ya milioni 200.
Baraza la Kiswahili la Taifa
(BAKITA), ndicho chombo chenye dhamana ya kuendeleza, kusimamia na kuratibu
shughuli za wadau wote wanaokuza Kiswahili nchini Tanzania na pia Baraza hili
ni mdau muhimu wa maendeleo ya Kiswahili kimataifa.
Miongoni mwa majukumu ya
BAKITA ni kuhimiza matumizi fasaha ya Kiswahili na kuzuia upotoshaji wake,
kushirikiana na mashirika ya kitaifa, asasi, au vikundi na watu binafsi katika
kuendeleza lugha hii, kushauri pamoja na kusimamia shughuli za ukuzaji wa Kiswahili
na ubidhaishaji wake.
Tangu kuanzishwa kwa BAKITA
mwaka 1967, Baraza limeendelea kufanya juhudi mbalimbali ambazo zimewezesha
kuipaisha lugha hii kitaifa, kikanda na kimataifa. Aidha, juhudi hizo
zimewezesha Kiswahili kuwa lugha ya mawasiliano mapana ya Jumuiya ya Afrika
Mashariki, kuwa moja ya lugha rasmi na lugha ya kazi katika Jumuiya ya
Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na Umoja wa Afrika (AU).
Fauka
ya hayo, Kiswahili kimekubalika kutumika katika mashirika mbalimbali ya
Kimataifa kama vile Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni
(UNESCO) na pia kinafundishwa katika vyuo mbalimbali duniani ikiwa ni pamoja na
kutangazwa katika idhaa mbalimbali za redio za kimataifa kama vile, Shirika la
Utangazaji la Uingereza (BBC), Idhaa ya Kiswahili ya Ujerumani (DW Swahili) na
redio Sauti ya Amerika (VoA), Redio Japan, Idhaa ya Kiswahili Redio Tehran na
Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa.
Hivi
karibuni BAKITA limepokea vifaa vya kisasa
vya kufundishia ukalimani ambavyo vimenunuliwa na Serikali kwa kiasi cha
shilingi mil. 187.5. Vifaa hivyo vitaliwezesha BAKITA kutoa mafunzo ya msasa na
kuwasajili wakalimani watakaotumiwa vifaa hivyo katika mikutano mbalimbali
kitaifa na kimataifa.
Akizindua
vifaa hivyo, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Bashungwa alisema
kupatikana kwa vifaa hivyo kumetimiza malengo ambayo Serikali ilijiwekea katika
kukuza lugha ya Kiswahili kwani lugha hiyo inawaunganisha Watanzania na watu wa
mataifa mengine kuwa wamoja katika shughuli mbalimbali za kitaifa na kimataifa.
Akizungumza
katika hafla ya uzinduzi wa vifaa hivyo iliofanyika Jijini Dar es Salaam katika
Ofisi za BAKITA Mhe. Bashungwa alisema kuwa Kiswahili hivi sasa kinazidi kuenea
kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kwani kinatumia katika vyombo
mbalimbali vya habari duniani, kufundishwa katika shule, vyuo na taasisi
nyingine za elimu za kimataifa na hata kwa mtu mmoja mmoja katika mataifa mengi
duniani.
“Chimbuko
la Kiswahili ni hapa kwetu Tanzania, tuna wajibu mkubwa wa kukiendeleza zaidi
kwa kuwasaidia wengine wanaokitafuta kwa kuwapatia rasilimali mbalimbali
zitakazo wawezesha kukielewa na kukitumia kwa usanifu na ufasaha zaidi. Moja ya
rasilimali hizo muhimu ni utaalamu huu wa ukalimani,” amesema Bashungwa.
Aidha, Mhe. Bashungwa
alisema kuwa Serikali inasimamia vema azma ya kukuza lugha hii ili iendelee
kuwa kuwa lulu ya mawasiliano duniani, na
alifanya kikao na watendaji wa Baraza la Kiswahili la Taifa Jijini Dar
es Salam ambapo pamoja na mambo mengine aliagiza kuboresha Mkakati wa Taifa wa Kubidhaisha
Kiswahili wa Miaka 10 unaoanzia mwaka 2021-2031 na mara baada ya hapo
uzinduliwe na uanze kutekelezwa.
Katika kufanya maboresho ya
mkakati huo, Waziri Bashungwa aliwaagiza BAKITA kuongeza ufunguzi wa vituo
maalumu vya kufundishia lugha ya Kiswahili na Utamaduni wa Mtanzania katika
nchi mbalimbali duniani.
Naye Kaimu Katibu wa BAKITA,
Consolata Mushi amesema kutokana na kuongezeka kwa mawanda ya matumizi ya lugha
ya Kiswahili, Baraza limeweka mipango mipya ya kukidhi ongezeko hilo ili
kuwezesha nchi na wataalamu wake kunufaika na fursa za Kiswahili zinazojitokeza
duniani.
“Miongoni mwa mikakati hiyo
ni pamoja na kuendeleza kanzidata ya wataalamu wa Kiswahili, kutoa mafunzo ya
kunoa stadi kwa wataalamu mbalimbali hususani wafasiri na wakalimani, waandishi
na wahariri, walimu pamoja na wakalimani”, amesema Mushi.
Mipango mingine ni kuandaa
Mkakati wa Taifa wa Kubidhaisha Kiswahili nchini na nje ya nchi kwa kipindi cha
miaka kumi kuanzia 2021 hadi 2031. Utekelezaji wa Mkakati huu utahusisha wadau
mbalimbali kutoka Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na Sekta binafsi. Lengo ni
kukuza kukuza Kuswahili ili kitumike kama chachu na bidhaa katika kuleta
maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii ndani na nje ya nchi.
Malengo mengine ya mkakati
huo ni kuimarisha matumizi ya teknolojia katika kufundisha Kiswahili kwa njia
ya mtandao, kuimarisha ushirikiano na mashirika, taasisi mbalimbali na nchi
nyingine katika kusambaza na kubidhaisha Kiswahili pamoja na kuanzisha programu
ya kujifunza Kiswahili kwa ajili ya watalii wanaoingia nchini kwa kushirikiana
na mamlaka mbalimbali.
Aidha, Mkakati huo utahusu
kuendeleza kanzidata ya Baraza ya wataalamu wa Kiswahili ambapo kwa sasa idadi
yao ni 1,325. Uingizaji wa wataalamu hao ulifanywa kwa kutumia programu maalumu
ya kikompyuta iliyoundwa na Baraza.
Miongoni wa taarifa nyingine
zinazoingizwa katika programu hiyo ni aina ya lugha nyingine ambazo mhusika
anazimudu vizuri, maeneo ya ubobezi katika taaluma ya Kiswahili, pamoja na
ujuzi mwingine alionao mtaalamu kama vile kutumia programu za kompyuta
zinazoweza kumsaidia katika ufundishaji na utafiti wa Kiswahili.
“Kuwepo kwa mfumo huo,
kutasaidia nchi kutambua idadi ya wataalamu wa Kiswahili waliopo na maeneo yao
ya ubobezi. Hatua hii ni njia muafaka ya kutumia fursa za lugha ya Kiswahili
zilizopo ndani na nje ya nchi”, ameongeza Mushi.
Mbinu nyingine zinazotumiwa
na Baraza katika kubidhaisha Kiswahili ni kutoa mafunzo kwa wataalamu wa
Kiswahili ambapo mpaka sasa takribani wataalamu 1,097 kutoka mikoa 12
wamekwishapatiwa mafunzo hayo ambao walifundishwa mbinu mpya za kufundisha na
kutumia vifaa mbalimbali vya ufundishaji ikiwa ni pamoja na vile vinavyotumia
teknolojia ya kompyuta.
Baraza pia limekuwa
likitumia vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi kukuza na kusambaza
Kiswahili. Hii inatokana na kwamba vyombo hivyo vinawafikia wananchi walio
wengi. BAKITA limekuwa likiendesha vipindi mbalimbali katika redio,
televisheni, magazeti na mitandao ya jamii kuelimisha umma matumizi sahihi,
sanifu na fasaha ya Kiswahili.
Akizungumzia umuhimu wa
Mkakati wa ubidhaishaji wa Kiswahili, Mushi alisema kuwa utasaidia kukua na
kuendelea kwa Kiswahili ndani na nje ya nchi, kutumika kwa Kiswahili sanifu na
fasaha, kuwepo kwa takwimu za wataalamu wa Kiswahili walionolewa vyema katika
tafsiri, ukalimani, ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni, ikiwa ni pamoja na
kuimarika kwa ushirikiano miongoni mwa wadau mbalimbali hususani sekta za umma
na binafsi katika ukuzaji na uendelezaji wa Kiswahili. Utekelezaji wa masuala
hayo utaleta matokeo chanya katika kutanua wigo wa matumizi ya Kiswahili na
ubidhaishaji wake.
MWISHO
No comments:
Post a Comment