Habari za Punde

RAIS SAMIA CHIFU MKUU TANZANIA, APEWA JINA LA HANGAYA

 

Na Eleuteri Mangi, WHUSM, Mwanza                                                                                          

Mwanadamu hupewa jina ili kumtambulisha ili atofautishwe na watu wengine. Jina hilo linaweza kuwa linamtambulisha yeye binafsi  au cheo chake katika taasisi hata nafasi yake katika nchi.

Siku ya Jumatano Agosti 08, 2021 itakumbukwa na Watanzania pamoja na dunia kwa ujumla kwa kuwa Machifu wa Tanzania wamempata Chifu wao Mkuu wa kwanza mwanamke ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akichukua nafasi ya mtanglulizi wake Hayati Dkt. John Pombe Magufuli.

Kwa kukabidhiwa kwake madaraka hayo, kunamfanya apewe jina ambalo ndilo linalomdhihirisha kuwa yeye ni Kiongozi Mkuu wa Kitaifa kuwaongoza Machifu wenzake na Watanzania kwa ujumla.

Ilikuwa majira ya saa sita kuelekea saa saba mchana katika Viwanja vya Red Cross eneo la Kisesa wilaya ya Magu mkoa wa Mwanza ndipo Mhe. Rais Samia alipewa jina la Hangaya wakati alipokuwa anakabidhiwa madaraka ya kuwa Chifu Mkuu nchini.

Jina hilo, Hangaya lina maana ya nyota angavu ya asubuhi inayoonesha matumaini linasadifu nafasi ya Mhe. Rais Samia ambayo Watanzania wana matumaini makubwa kwa uongozi wake kwenye maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

Ili kuwa Chifu kamili, Kiongozi huyo wa Machifu nchini, Chifu Hangaya alifanyiwa ibada ya kimila iliyokuwa na sala maalumu ya kumuombea siha njema, dhima na dhamana ya kuwa kiongozi hodari na mahiri kwa taifa analoliongoza.

Sala hiyo iliongozwa na maneno kuntu ambayo yalishamirisha sherehe hiyo adhimu iliyokuwa imefurika hadhira iliyohudhuria Tamasha la Utamaduni la siku mbili kuanzia Septemba 7 hadi 8, 2021. Tamasha hilo liliandaliwa na Umoja wa Machifu Tanzania (UMT) kwa lengo la kulinda mila na desturi za Mtanzania liliongozwa na kaulimbiu isemayo, “Turithishe Utamaduni Wetu, Tudumishe Utamaduni Wetu, Amani na Umoja ni Tunu Zetu.”

Kwa mujibu wa Makamu Mwenyekiti wa Machifu Tanzania, Chifu Msagata wa Uchifu wa Unyanyembe Tabora  alisema “Sasa una mamlaka ya kuwaita watu kwa vikao vyako kwa sababu una mamlaka, wewe ni kiongozi shupavu, imara, mkakamavu, mweledi, uwaongoze watu wako kwa amani.”

Kiongozi huyo mpya amekabidhiwa vitendea kazi mbele ya jopo la Machifu na Watanzania ikiwa ni alama ya kusimamia himaya yake ya kiutawala yaani Taifa la Tanzania akisaidiwa na Machifu hao katika maeneo yao. Miongoni mwa vitendea kazi hivyo ni pamoja na nguo nyeusi,nguo nyekundu, ngozi ya chui, ushanga ulio na yai la mbuni, kiti cha utawala, ngao na mkuki pamoja na usinga.

Ili kujua maana ya vifaa hivyo, mwandishi wa makala haya alichukua wasaa wa kuonana na Chifu Aron Mikomangwa Nyamilonda wa Uchifu wa Jiji la Mwanza unaojumuisha Halmashuri za Ilemela na Nyamagana ambaye ni mbobezi wa masuala ya utamaduni wa kabila la Wasukuma na kueleza kuwa, nguo nyeusi aliyovikwa Chifu Hangaya ni alama ya mawingu meusi yanayoleta mvua ili wananchi walime na kupata chakula. Chifu anapovaa nguo hiyo, maana yake Watanzania wanapomuona kiongozi wao wanapata matumaini ya kupata mafanikio kupitia kiongozi wao chini ya uongozi wake mahiri.

Aliendelea kusema kuwa, nguo nyekundu aliyovikwa Chifu Hangaya ni alama ya ulinzi, Chifu Hangaya anapaswa kuilinda nchi yake. Kwa nafasi yake Rais ni mlinzi wa kwanza wa nchi yake na watu wake kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kifaa kingine alichokabidhiwa Chifu Hangaya Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni ngozi ya chui ambayo alivikwa ikiwa ni ishara na alama ya upole na ulinzi wakati wote. Chifu Mikomangwa alisema “Muogope sana chui akiwa na watoto wake ukimkanyaga atakumaliza.”

Kwa muktadha wa Rais Mhe. Samia kukabidhiwa madaraka hayo, yeye ndiye Chifu Mkuu na chini yake wapo Machifu na Watanzania kwa ujumla wao ambao wanamuombea awe mpole awe na mwangalifu kwa watu wote wenye nia ovu na Tanzania.

Vile vile katika hafla hiyo Chifu Hangaya Samia alivikwa ushanga wenye yai la mbuni, ndege huyo ni mwangalifu sana katika kulinda mayai na watoto wake. Hivyo, Watanzania ndiyo mayai na vifaranga wa Chifu Hangaya Samia ambaye anawajibu wa kuwalea, kuwatunza na kuwalinda Watanzania.

Hali kadhalika Mhe. Rais amekabidhiwa kiti chenye mguu mmoja ambacho ni alama ya utawala mmoja ambacho hakikaliwi na mtu mwingine zaidi yake. Mikomangwa alisema Hangaya anapokaa katika kiti chake cha kiutawala, hukaa na Watanzania ili kujenga na kuendeleza nchi na watu wake.

Pia, amekabidhiwa ngao na mkuki akiwa kiongozi na Mkuu wa Mchifu nchini ili aweze kulinda nchi yake na watu wake kupitia majeshi ya Ulinzi na Usalama ambapo yeye ni Amiri Jeshi Mkuu.

Mwisho ila siyo kwa umuhimu, alikabidhiwa usinga unaotokana na singa za mikia ya nyumbu ambao tafsiri yake ni watu. Usinga kwa muonekano na uhalisia wake una manyoya mengi, haya yanawakilisha uwingi wa watu alionao Chifu Hangaya ambao ni Watanzania. Amekabidhiwa ili awalinde kwa amani.

Hakika Chifu Hangaya Samia Suluhu Hassan ameanza kazi yake ya Uchifu mara moja ambapo alisema Tanzania ipo kwenye mchakato wa kuandaa Sera mpya ya Utamaduni itakayoendana na mazingira ya sasa ya dunia lakini itakayolinda maadili Mtanzania.

Hivyo, mara baada ya kukabidhiwa madaraka hayo aliagiza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambayo ndiyo yenye dhamana na Utamaduni kupata maoni kutoka kwa Watemi na Machifu.

“Na niagize Wizara, katika maadalizi ya mchakato wa Sera hii, lazima tupate maoni kutoka kwa Watemi na Machifu wetu, maoni yao yaingizwe kweye Sera hii ili tuendeleze utamanuni wetu. Na ni imani yangu kuwa hatua hizi zitasaidia kulinda, kuenzi na kukuza utamaduni wetu” alisisitiza Rais Mhe. Samia.

Ujio wa Machifu wengi katika hafla hiyo ya kukabidhiwa madaraka hayo kwa Chifu wao Mkuu Hangaya Samia Suluhu Hassan ni udhihirisho na imani ya Watanzania wote kusimama imara na kuhakikisha kaulimbiu ya uongozi wake ya “Kazi Iendelee” inakuwa mwanzo mpya wa kuhakikisha utamaduni wa Mtanzania utaendelea kujulikana kote kupitia filamu ya “Royal Tour” inayoandaliwa kuitangaza Tanzania duniani.

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Filamu ya “Royal Tour”, Dkt. Hassan Abbasi alisema kuwa filamu hiyo ni fursa adhimu ambayo itasaidia kutangaza rasilimali za Tanzania huku akinukuu maneno ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye alisema “Baada ya kukamilika kwa filamu hii itakayotangaza utalii, biashara na fursa za uwekezaji nchini kupitia kipindi maarufu cha Royal Tour, dunia itafahamu kuwa madini ya Tanzanite yanachimbwa Tanzania pekee.”

Maneno hayo yalisemwa na Rais Septemba 5, 2021 akiwa mkoani Manyara wakati akizungumza na wananchi wa Mirerani na kuongeza kuwa ni faraja na ushahidi dhahiri kuwa eneo hilo ni mahali pekee yanakochimbwa madini ya Tanzanite duniani.

Sasa ni wakati wa kuutangaza utamaduni wa Mtanzania duniani ili kuakisi maneno ya Mwasisi wa Taifa la Tanzania, Baba wa Taifa Mwl Julius Kambarage Nyerere ambaye aliwahi kusema “Utamaduni ni kiini ama roho ya taifa lolote, taifa lisilo na utamaduni ni sawa na mkusanyiko wa watu usio na roho.”

Kupitia Tamasha la Utamaduni la Kisesa Mwanza, Rais Mhe. Samia ametoa mwanga na hamasa kwa makabila yote nchini kuanzisha matamasha katika maeneo yao ili kutambulisha mila na desturi zilizopo katika maeneo yao na kutangaza fursa za kiutamaduni na utalii hatua itakayosaidia kukuza uchumi katika mikoa yote na kila pembe ya Tanzania.

Matamasha hayo yamekwisha anza kufanyika katika mikoa ya Mwanza, Arusha, Manyara, Dodoma na Mbeya. Sasa ni zamu yenu mikoa mingine kuwa na matamasha yanayowapa fursa ya kutangaza utamaduni wenu na kuwapa fursa Watanzania kufanya utalii wa ndani katika mikoa yenu ili kuweza kujifunza mila, desturi, historia na tamaduni za makabila mbalimbali yaliyopo nchini. “Hakika Kazi Iendelee.”

Mwisho

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.