Habari za Punde

‘Tozo za Miamala ya Simu Kujenga Madarasa na Zahanati’ Rais Samia

 


Na. Georgina Misama – MAELEZO

Septemba 03, 2021

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali imepunguza tozo kwa asilimia 30 baada ya kusikia malalamiko ya Watanzania,  na kuwasisitiza umuhimu wa tozo hizo katika kukamilisha miradi mikubwa iliyoachwa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli na pia kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo vituo 220 vya afya, pamoja na miradi ya elimu, maji na umeme ambayo inakwenda moja kwa moja kwa wananchi. 

Akizungumza na wakazi wa jimbo la Kawe  Jijini Dar es salaam  leo, wakati akiwa njiani kuelekea Bagamoyo katika ziara yake ya kurekodi vivutio vya utalii ili kuitangaza Tanzania, Rais samia alisema kwamba Serikali iliweka tozo ya miamala ya simu ili kukusanya fedha kwa ajili ya maendeleo na kuwahakikishia kukamilika kwa miradi hiyo kama ilivyopangwa kwa faida ya watanzania wote.

“Katika bajeti iliyopita tuliweka tozo kwenye miamala ya simu ambayo imepigiwa kelele kila mahali. Nimesikia malalamiko yenu, nimekaa na wataalam wangu, tumepunguza asilimia 30 lakini hatutozifuta kabisa tozo hizo kwasababu fedha tutakazopata zitatusaidia kutekeleza miradi yetu wenyewe, pasipo kuingiliwa, hakuna wa kutujengea madarasa pasipo sisi wenyewe”, alisema Rais Samia.

Aidha, Rais Samia alisema kwamba fedha zitakaozokusanywa kwa miezi ya Septemba na Oktoba, zitatumika kujenga vyumba vya madarasa zaidi ya 500 Tanzania nzima ili kuwaandalia wanafunzi wanaotarajiwa kuingia sekondari mwakani na pia wale watakaoanza shule ya msingi ikiwemo shule aliyoomba mbunge wa Kawe Mhe. Josephat Gwajima katika mkutano huo.

“Misaada siku hizi ni michache sana, lazima tuminyane wenyewe kwa wenyewe ili tujiletea maendeleo, tuna wimbi kubwa la watoto wanataka madarasa kuingia sekondari na wengine wataanza darasa la kwanza, niwahakikishie tutakwenda kuikamilisha miradi hiyo kama ilivyopangwa”, alisisiza Rais Samia.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kawe Mhe. Josephat Gwajima alitoa shukrani kwa Rais Samia kwa kuwawapatia fedha kiasi cha shilingi  bill.8 ambazo zimetumika kujengea mifereji katika kata ya Mbweni ambayo ilikuwa inakabiliwa na mafuriko, lakini pia kwa kupokea shilingi Bil.14 kwa ajili ya ujenzi wa barabara  za ndani 115 katika  jimbo hilo.

“Tunakushukuru Mhe. Rais kwa mambo makubwa uliyotufanyia, ulituahidi kutupa bill.8 ili zitusaidie kujenga mifereji katika kata ya Mbweni ambayo ilikuwa na changamoto ya mafuriko. Tayari fedha hizo tumeshapokea na kazi ya kujenga mifereji inaendelea, aidha, tunakushukuru kwa kutupatia bill.14 kupitia mkono wa TARURA ili kujenga barabara hizo”, alisema Mhe. Gwajima.

Aliongeza kuwa hivi sasa wapo kwenye kukamilisha mradi wa maji ambapo unatarajiwa kukamilika ifikapo  Oktoba 15 mwaka huu kwenye vijiji vya Nakasangwe na Kisanga vinavyokabiliwa na changamoto hiyo.

Mhe. Gwajima pia alimuomba Rais Samia kuwajengea shule wakazi wa  Wazo ambao hivi sasa wanalazimika kuvuka barabara ili kwenda kwenye shule za Kunduchi na kusababisha kugongwa na magari wakati wakivuka barabara kubwa ya Bagamoyo, ambapo changamoto hiyo ilitatuliwa hapo hapo na Mhe. Rais.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.