Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. Philip Mpango leo tarehe 15 Januri 2022 ametembelea katika mitaa
mbalimbali ya Jiji la Dodoma pamoja na Soko la Majengo kukagua utunzaji wa
Mazingira katika maeneo hayo.
Akiwa katika mitaa hiyo Makamu wa Rais
ameshuhudia uwepo wa takataka katika maeneo mbalimbali ambazo wananchi
wamezikusanya lakini huchukua muda mrefu pasipo kuondolewa.
Wananchi hao wamemueleza Makamu wa Rais adha
wanayoipata ya kuishi na takataka hizo jirani na maeneo yao kwa kipindi cha
wiki mbili pasipo kuondolewa hali inayohatarisha usalama wa afya zao. Aidha
wamesema licha ya kutoa fedha kwa mamlaka zinazokusanya takataka hizo lakini
bado takataka hizo husalia katika maeneo yao ambayo pia hutumika kwa biashara
za vyakula.
Akizungumza na viongozi wa Mkoa wa Dodoma
mara baada ya kutembelea maeneo hayo, Makamu wa Rais ameonesha kutoridhishwa na
hali ya usafi katika mkoa wa Dodoma. Ameagiza kusimamishwa kwa mkataba baina ya
Jiji la Dodoma na kampuni inayokusanya taka hizo (Green Waste) kutokana na kushindwa kutekeleza majukumu
yake kiufanisi.
Amewataka viongozi wa Jiji la Dodoma
kuchukua hatua za haraka katika kuhakikisha jiji hilo linakuwa safi pamoja na
maeneo ya masoko na barabara zote. Aidha Makamu wa Rais amewaagiza wakurugenzi
katika maeneo mengine nchi nzima kuchukua zoezi la usafi kama zoezi endelevu na
linapaswa kuzingatiwa kikamilifu. Amewataka viongozi kuacha kukaa ofisini pekee
bali pia kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo yao ili kufuatilia wale
waliowapa dhamana ya uondoaji wa takataka hizo katika mitaa kama wanakidhi
kuendelea kufanya kazi hiyo.
No comments:
Post a Comment