Na Eleuteri Mangi, WUSM-Moshi
Serikali ya Awamu ya Sita
chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ipo
msatari wa mbele kusimamia, kuendeleza na kuimarisha masuala ya utamaduni
nchini hatua inayosaidia kuendeleza mila na desturi za mtanzania kwa kizazi cha
sasa na vizazi vijavyo.
Hayo yamedhihirishwa na
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Utamadini kutoka Wizara ya Utamaduni, Sanaa na
Michezo Dkt. Emmanuel Temu alipofanya ziara ya kikazi mkoani Kilimanjaro kwa
kutembelea vikundi vinavyojishughulisha na masuala mbalimbali ya kiutamaduni
katika makabila ya wapare, wachaga, wamasai pamoja na wagweno wanavyoendeleza
utamaduni wao kupitia ngoma za asili, vyakula vyao pamoja na lugha zao.
“Huu ni muda mwafaka wa
kuwafundisha vijana wetu utamaduni wetu kwa kuunda vikundi vya ngoma za asili
kama sehemu ya kutunza amali za utamaduni kupitia vyakula, historia za makabila
yetu, mavazi, vifaa vya kiutamaduni pamoja na mila na desturi ambazo ni njema
kwa vijana wetu” amesema Dkt. Temu.
Dkt. Temu ameongeza kuwa
Septemba 8, 2021 Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye tamasha la Utamaduni
lililofanyika eneo la Kisesa mkoani Mwanza alihimiza mikoa yote nchini kuwa na
matamasha ya utamaduni katika maeneo yao ili kuwarithisha watoto na vijana
utamaduni wao.
Hatua hiyo ya kiongozi wa
nchi inaonesha Serikali inatoa msukumo wa wananchi wahamasike kulinda, kutunza,
kuhifadhi, kuthamini na kuendeleza utamaduni wa mtanzania.
Akiwa
wilayani Mwanga mkoani humo Dkt. Temu amekutana na Mkuu wa Wilaya hiyo Bw.
Abdallah Mwaipaya ambaye ameahidi kuendelea kushirikiana na Wizara na
kuwahamasisha wananchi na vikundi mbalimbali vya utamaduni katika wilaya hiyo ili
kuendeleza mila na desturi njema kwa kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
Akinukuu
maneno ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Bw. Mwaipaya alibainisha kuwa Baba wa Taifa aliwahi
kusema “Utamaduni
ni kiini ama roho ya Taifa lolote. Taifa
lisilo na utamaduni ni sawa na mkusanyiko wa
watu wasio na roho.”
Kwa
upande wake Mkuu wa wilaya ya Siha Bw. Thomas Apson amesema ziara hiyo imewatia
moyo na wapo tayari kutoa ushirikiano kila wakati kwa kuwa hilo ni jambo jema
na kila mtu anaguswa kwa namna yake ili kuimarisha, kuboresha na kuendeleza
utamaduni wetu kwa watoto na vijana wajue mila na desturi zao.
Vikundi
ambavyo vimetembelewa katika ziara hiyo ni kikundi cha Lambo Daima kutoka
kijiji cha Lambo, kikundi cha Teule
kutoka kijiji cha Kisanjuni, kikundi cha Furahisha kutoka kijiji cha Mwaniko
ambavyo vyote vipo wilaya ya Mwanga pamoja na kikundi cha Rosi kutoka Marangu
wilaya ya Moshi Vijijini.
Vikundi
vingine ambayo vimetembelewa ni Gonjaza Asili Star kutoka Suji, Lukungu Sanaa
Group kutoka Vudee Nyika kata ya Bangalala pamoja na kikundi cha Wazee Nasuro
kutoka kijiji cha Nasuro kata ya Mwembe vyote kutoka wilayani Same.
Katika
wilaya ya Hai ambapo ujumbe huo umekutana na mghani mashairi Bw. Seifu Mkambala
wakati katika wilaya ya Siha kikundi cha Osiligilai kutoka kijiji cha Ndinyika
Karansi kimepata fursa ya kutembelewa na kuonesha namna wanavyoendeleza
utamaduni wa kabila la Wamaasai katika eneo lao ambapo asilimia kubwa ya
wanakikundi hicho ni vijana jambo linalotia moyo kuwa utamaduni huo
unaendelezwa tofauti na vikundi vingine ambavyo idadi ya washiriki wengi ni
watu wazima pamoja na wazee.
No comments:
Post a Comment