Habari za Punde

Uwepo wa Makongamano na hafla mbali mbali za Kidini kutaweza kurudisha Mila Silka na Tamaduni Nchini.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akitoa nasaha zake kwa Waumini wa Dini ya Kiislamu na wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja katika hafla ya ufunguzi wa Tamasha la Ramadhani lililotayarishwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kaskazni Unguja lililofanyika Kiwanja cha Misuka Mahonda.


Na.Abdulrahim Khamis.OMPR. 18/04/2022

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Alhajj Hemed Suleiman Abdulla ametoa wito huo akifungua Tamasha la Ramadhani lililotayarishwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja lililofanyika katika kiwanja cha Misuka Mahonda.

Amesema Zanzibar inasifika kwa maadili mema kihistoria yaliyotokana na Dini ya Kiislamu maadili ambayo kwa sasa yamepotea hatua inayopelekea kukosa viongozi  bora wenye hapo baadae.

Amesema umefika wakati wazazi na walezi kurudi katika malezi ya Asili ambayo yataweza kuisaidia Serikali katika kuondosha matendo maovu.

Amesema malezi mema kwa watoto yatasaidia kupata Wanazuoni na Maimamu wa baadae ambao watakuja kuisimamia Dini ya Allah (S.W) ambao pia watasaidia kupata Zanzibar yenye viongozi bora wenye maadili mema.

Aidha Alhajj Hemed amesema kuwa ana Imani Kongamano hilo litakuwa na mnasaba wa Maendeleo ya Zanzibar yenye maadili mema kupitia mada mbali mbali na ujumbe utakaotolewa kwa wawasilishaji mbali mbali.

Sambamba na hayo Mhe. Hemed ametumia fursa hiyo kuwataka waumini wa Dini ya Kiislamu kuendeleza Ibada mbali mbali na kujifunza mengi mazuri yanayopatikana katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Mhe. Ayoub Muhamed Mahmoud ameeleza kuwa lengo la kuandaa Tamasha hilo ni kubadiki fikra za wananchi wa Mkoa wa Kaskazini na Zanzibar Unguja kwa ujumla ili Zanzibar irudi katika maadili iliyokuwa ikisifika.

Amesema Serikali ya Mkoa wa Kaskazini Unguja imeanzisha Programu mbali  mbali kila mwezi ambazo lengo ni kuwaelimisha wananchi wa Mkoa huo kufahamu mengi mazuri ya kuwa nayo ambayo yatapelekea kuwa na Zanzibar yenye Maendeleo na kuisaidia Serikali katika kufikia malengo yake iliyojiwekea.

Nae Naibu Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Mahmoud Mussa Wadi amesema ili kurudi katika malezi bora ni wajibu kufuata maelezo yaliyomo katika Qur-an Tukufu na Hadithi za Mtume Muhammad (S.A.W) na kushauri kuundwa kwa Kamati za Maadili katika Shehia.

Tamasha la Ramadhani lililoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja litajumuisha matukio mbali mbali ikiwemo Kongamano, Mashindano ya Kuhifadhi Qur-an, Ugawaji wa Sadaka kwa kaya Maskini pamoja na Iftaari kwa makundi mbali mbali.

Muhadhari wa Dini ya kiislamu Zanzibar Sheikh Othman Maalim akitowa nasaha zake na kuwasulisha Mada kuhusiana na Utalii katika Uislamu wakati wa Kongamano la Ramadhani lililofanyika katika viwanja vya Misuka Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Naibu Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Mahmoud Mussa Wadi akitoa salamu kutoka Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar katika ufunguzi wa Tamasha la Ramadhani lililofanyika katika kiwanja cha Misuka Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Mhe. Ayoub Muhamed Mahmoud akitoa maelezo kuhusiana na Tamasha la Ramadhani lililofanyika Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja
Waumini wa Dini ya Kiislamu wakimsikiliza kwa makini Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla wakati akitoa nasaha zake baada ya ufunguzi wa Tamasha la Ramadhani lililofanyika Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.