Habari za Punde

Waziri Mhe Harusi Atembelea Kituo cha Kurekebisha Tabia Kidimni Wilaya ya Kati Unguja.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe Harusi Said Suleiman akimsikiza kwa makini Meneja msimamizi mafunzo wa Kituo cha Tiba na Marekebisho ya tabia kilichopo Kidimni ndugu Simai M. Amour alipokuwa akimuelezea ratiba ya mzunguko wa maisha ya wanafunzi waliopo kituoni hapo.   


Kituo cha Tiba na Marekebisho ya tabia kilichopo Kidimni kinatarajiwa kuwa ni kitovu cha malezi ya vijana walioathirika na matumizi ya Dawa za Kulevya sehemu ambayo watapatiwa tiba sahihi na stadi za maisha, kujifunza masuala mbali bali yenye manufaa ili waendane na harakati za maendeleo kama mipango ya Serikali ilivyobainisha

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe Harusi Said Suleiman ameyasema hayo wakati alipotembelea kituo hicho akiwa ameongozana na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar Kanali Burhani Z. Nasoro pamoja na viongozi wengine wa mamlaka hio

Mhe Harusi amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inatekeleza mradi huu ikiwa imetumia busara kubwa na kufikiria wananchi wake hasa vijana ambao ndio wajenzi na rasilimali muhimu katika kuendeleza uchumi wa nchi na taifa kwa ujumla

Amesema dawa za kulevya ni adui wa maadili, ndio chanzo cha maasi na huharibu mfumo wa uchumi, hivyo ameiomba jamii kuunganisha nguvu za pamoja kuchukia matumizi ya dawa za kulevya kwa kuwafichuwa waingizaji, wasambazaji na wauzaji

Wajibu wetu wananchi kila mmoja wetu kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kuwafichua wafanyabiashara na wasambazaji wa dawa za kulevya”alisisitiza Bi Harusi

Mhe Harusi akiwa kituoni hapo amekagua na kutembelea mradi wa banda la malisho ya ngombe, mabanda ya kuku, sehemu inayotegemewa kujengwa karakana ya kutengeneza magari, sehemu inayolimwa bustani za mbogamboga, vyumba vya kulala na ofisi

Nae na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Zanzibar Kanali Burhani Z. Nasoro amemuhakikishia   Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe Harusi Said Suleiman kuendelea kuweko kwa ulinzi na usimamizi madhubuti katika kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya ndani na nje ya kituo hicho

Aidha Kanali Burhani amewasisitiza wazazi na wanafamilia kupeleka vijana wao katika Kituo cha Tiba na Marekebisho ya tabia kilichopo Kidimni kwani kuna fursa muhimu za kijana kuweza kujitegemea mara tu atakapotoka hapo na kuwa raia wema wa baadae.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.