Habari za Punde

Chuo cha Ruaha CDTI Chazindua Dawati la Jinsia.

Mkuu wa Wilaya ya Iringa Ndg.Mohamed Hassan Moyo akiongea na wanafunzi na wadau mbalimbali waliofika chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha CDTI wakati wa uzinduzi wa dawati la jinsia.
Mkuu wa chuo cha CDTI Godfrey Mafungu akiongea na wanafunzi na wadau mbalimbali waliofika chuo cha maendeleo ya jamii Ruaha CDTI wakati wa uzinduzi wa dawati la jinsia.


Na Fredy Mgunda,Iringa.                                                                                                                              

Mkuu wa Wilaya ya Iringa Mohamed Hassan Moyo amezindua kitengo cha dawati la jinsia katika chuo cha maendeleo ya Jamii Ruaha CDTI kilichoanzishwa rasmi ili kukomesha vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanafunzi chuoni hapo

 

Akizunguma wakati wa uzinduzi kitengo hicho, mkuu wa wilaya ya Iringa alisema kuwa uwepo wa dawati hilo utachangia maendeleo ya usawa wa kijinsia na kupunguza vitendo vya ukatili ikiwemo rushwa ya ngono inayotajwa kukithiri katika vyuo mbalimbali na kuchafua taswira ya elimu ya kati na ya juu nchini.

 

Moyo alisema kuwa uwepo wa kitengo hicho cha dawati la jinsia katika chuo hicho kutachochoe usawa wa haki kwa wanafunzi wa chuo hicho cha Ruaha.

 

Alisema kuwa Iringa kumeibuka wimbi kubwa kwa wanaume kuanza kufanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia na wanaume wameanza kutoa malalamiko yao kwenye vyombo husika hivyo wanafunzi wa kiume kutoona aibu kulitumia dawati hilo pindi wanapotendewa ukatili

 

“kitengo hicho siyo kwa ajili ya wanafunzi wa kike pekee, huku akiwahimiza wanafunzi wa kiume kutoona aibu kulitumia dawati hilo pindi wanapotendewa ukatili” alisema Moyo.

 

Kiongozi huyo amepongeza hatua ya uanzishwaji wa dawati hilo Chuoni hapo na kutoa mwito kwa taasisi mbalimbali kuunga mkono jitihada zilizoanzishwa katika kupambana na ukatili wa kijinsia chuoni hapo.

 

Moyo alizitaka mamlaka nyingine kama vile jeshi la Polisi,TAKUKURU,ofisi ya mashtaka na taasisi zisiszo za kiserikalina za serikali kuendelea kuunga mkono juhudi zilizofanywa na chuo hicho kwa kutoa ushirikiano unatakiwa.

 

Kwa upande wake mratibu wa dawati la jinsia katika chuo hicho cha maendeleo ya jamii CDTI Asha Nyoni alisema kuwa Unzishwaji wa dawati hilo la jinsia umetokana na uwepo wa taarifa za matukio ya vitendo vya ukatili wa kijinsia katika Taasisi za Elimu ya juu na ya kati.

 

Nyoni alisema kuwa maswala ya ukatili wa kijinsia ni mtambuka hivyo ni kuangalia kwa namna gani ya kuweka mfumo rafiki ya kuona namna gani wanakomesha au kuondoa kabisa vitendo vya ukatilii wa kijinsia.

 

 

Alisema kuwa ukatilii wa kijinsia umekuwa ukitokeza maeneo mengi ya elimu ya juu na kati ndio maana wizara ikaamua kuanzisha dawati la ukatilii wa kijinsia.

 

 

 Awali mkuu wa chuo cha CDTI Godfrey Mafungu ameeleza jitihada zilizoanzishwa na chuo hicho katika kuwawezesha wanafunzi kujitambua na kuepukana na vitendo hatarishi

 

Mafungu alisema kuwa umefika wakati kwa wanafunzi kujitambua kuhusu maswala ya ukatili wa kijinsia kwa ajili ya maendeleo ya elimu wanayoipata chuoni hapo.

 

Alisema kuwa imekuwa vigumu mno kwa vijana wengi kujitambua wawapo chuoni hivyo jambo la kujitambua linatakiwa kupigiwa kelele sana ili vijana waweze kujitambua.

 

Mafungu alisema kuwa ukatili wa kijinsia umekuwa unarudisha nyuma juhudi za kuleta maendeleo kwa wananchi hivyo wanafunzi wa chuo wakiwa na elimu ya ukatilii wa kijinsia basi wataifikisha kwa jamii husika juu ya madhara ya ukatili wa kijinsia.

 

Hatua hii ni utekelezwaji wa maelekezo ya Rais Wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa  wakati akilihutubia Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano ambapo alielekeza Taasisi za Umma na Binafsi kuhakikisha zinaweka utaratibu unaofaa wa kutokomeza Ukatili kwa wanawake, wasichana wavulana na watoto.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.