Habari za Punde

CHANETA KUBEBWA KWA MBELEKO MBILI-GEKUL

 

Na.Adeladius Makwega-WUSM

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Bi Pauline Gekul amesema kuwa Serikali itaendelea kuvibeba vyama vya michezo ikiwamo CHANETA kwa mbeleko mbili, moja ikiwa yake na ya pili ikiwa ya Rais Samia Suluhu Hassan kuhakikisha michezo inaimarika nchini.

Kauli hiyo ya serikali imetolewa na Naibu Waziri Gekul Mei 20, 2022 akiwa njiani akitokea Babati mkoani Manyara kuja Dodoma kuendelea na shughuli zake za kikazi ikiwamo kufanya kikao na CHANETA ambacho ni Chama cha Mpira wa Netiboli nchini.

“Ninaposema mbeleko maana yangu kuwa mtoto anabebwa kwa ubeleko mmoja lakini pale kunapokuwa hakuna budi mama hufanya upendeleo wa kumbeba mtoto wake kwa mbeleko mbili kuhakikisha anafika mbali zaidi.”

Aliongeza kuwa yeye kwa ushirikiana na Waziri wake Mheshimiwa Mohammed Mchengerwa ubeleko wake umefungwa vizuri na vyama vya michezo vinakuwa imara na michezo inazidi kufanikiwa na ndiyo maana wamejiwekea utaratibu wa kukutana na vyama mbalimbali vya michezo kila mara.

“Ubeleko wa Rais Samia Suluhu Hassan katika michezo umekuwa imara zaidi kwa kuongeza bajeti ya michezo kila uchao.”

CHANETA wakiongoza na mwenyekiti wao Dkt. Devota Marwa wapo jijini Dodoma kwa ratiba maalumu ya mazungumzo ya kina na Serikali ambapo kwanza wameanzia na Bungeni ambapo walizungumza na wabunge wakiongozwa na watumishi kadhaa wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Wanatarajia kufanya kikao kizito na Naibu Waziri Gekul, ambapo CHANETA wanasema kuwa wamejindaa vema kuuboresha mchezo huo hapa nchini.

“Tumekamilika, uongozi wetu upo imara, tunahakika katika kikao hicho na serikali tutayaweka wazi mambo yetu kadhaa, tuna imani yatapokelewa kwa mikono miwili na mara zote Serikali imekuwa ikifanya hivyo.”

Katika kikao hicho CHANETA inaongozwa na viongozi wake 11 inayowajumuisha wanahabari wawili maarufu nchini Bi Shy-Rose Bhanji na Bi Betty Mkwasa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.