Habari za Punde

WATUMISHI WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO WAHIMIZWA KUFANYA KAZI KWA BIDII

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Jenifa Omolo, akizungumza wakati wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi kilichofanyika ukumbi wa Kambarage, jijini Dodoma. Kushoto ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Tumwesigwe Kazaura na kulia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi (Tughe) Bi. Scolastika Okudo.

Na. Saidina Msangi, WFM, Dodoma.

Wizara ya Fedha na Mipango imewataka watumishi wake kuendelea kufanya kazi kwa bidii na weledi katika kuhudumia wananchi wakati ambao Wizara inaendelea kushughulikia maslahi yao.

Hayo yalielezwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Jenifa Omolo, wakati akifunga kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo jijini Dodoma.

Alisema kuwa wizara inaendelea na jitihada mbalimbali ili kuhakikisha kuwa watumishi wanafanya kazi katika mazingira bora na salama.

‘Tunaendelea na ujenzi wa Ofisi za wizara Mtumba na pia tunaendela na ukarabati wa Ofisi za Hazina Ndogo mikoani, lengo ni kuona kuwa watumishi wanafanya kazi katika mazingira bora na salama’, alisema Bi. Omolo.

Akizungumzia maslahi ya nyongeza ya mishahara, Bi. Omolo, alisema kuwa Wizara imepokea maoni hayo na kuwa suala hilo tayari Serikali imelipokea na inaendelea kulifanyia kazi.

Aidha, alieleza kuwa Wizara imefanikiwa kupandisha madaraja watumishi 437 pamoja na kutoa mikopo kwa ajili ya vyombo vya usafiri kwa watumishi yenye thamani ya Sh. bilioni 1.8.

Aliongeza kuwa changamoto ya upungufu wa watumishi inafanyiwa kazi ambapo mpaka kufikia Julai mwaka huu watumishi watakuwa wamepelekwa katika Ofisi za Hazina Ndogo mikoani.

Bi. Omolo alifafanua kuwa lengo la kufanya kikao cha Baraza la Wafanyakazi ni kuwapa watumishi nafasi ya kutoa maoni kuhusu namna ya kushughulikia maslahi ya watumishi na pia kuangalia taarifa ya utekelezaji wa Bajeti ya Wizara kwa mwaka uliopita na kuangalia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara kwa mwaka Wwa fedha unaokuja.

Kwa upande wake, Mhasibu Mkuu wa Serikali Bw. Leornard Mkude, amewasisitiza wastaafu wanaolipwa pensheni na Hazina kuepuka matapeli wanaodai kuweza kuwasaidia kupata mafao kwani huduma hiyo ni bure na malipo ya pensheni kwa wastaafu wanaolipwa na Hazina yanalipwa kulingana na ukamilishwaji wa taarifa muhimu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.