Habari za Punde

Dk.Mwinyi Ampongeza Mkuu wa Majeshi Jenerali Mabeyo kwa Kutekeleza Vyema Majukumu Yake.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania Jenerali Venance Salvatory Mabeyo, alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na kuja kumuaga, mazungumzo hayo yaliofanyika katika ukumbi wa Ikulu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amempongeza Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Jenerali Venance Salvatory Mabeyo kwa kutekeleza vyema majukumu yake katika kipindi chake chote cha utumishi ndani ya Jeshi hilo.

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungumzo na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Jenerali Venance Salvatory Mabeyo ambaye amefika Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kumuaga Rais kufuatia kumaliza muda wa utumishi wake ndani ya Jeshi hilo mwishoni mwa mwezi huu.

Katika maelezo yake Rais Dk. Mwinyi alimuelezea Jenerali Mabeyo kwamba ni kiongozi ambaye alifanya kazi zake vyema katika Jeshi hilo na alimpa ushirikiano mkubwa yeye na viongozi wenzake wakati akiwa Waziri wa Ulinzi hatua ambayo ilimuwezesha kutekeleza mambo mengi ndani ya Jeshi hilo.

Alieleza kwamba ushirikiano alioupata kutoka kwa Jenerali Mabeyo wakati akiwa Waziri wa Ulinzi na hata akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi anauthamini na ataendelea kuukumbuka.

Hivyo, Rais Dk. Mwinyi alimtakia kila la kheri Jenerali Mabeyo katika maisha yake ya kustaafu hasa ikikumbukwa kwamba amelitumikia kwa muda mrefu Jeshi hilo na kufanya mambo mengi yatakayoacha alama.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi alimpongeza Jenerali Mabeyo kwa mashirikiano yake aliyoyatoa katika kuhakikisha changamoto mbali mbali zinapatiwa ufumbuzi wakati wa uongozi wake ndani ya Jeshi hilo.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Mwinyi alieleza hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali zote mbili kwa mashirikiano ya Jeshi la Ulinzi Tanzania katika kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa changamoto za ardhi katika maeneo ya Jeshi.

Alitoa shukurani kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutenga Bajeti maalum kwa ajili ya fidia hatua ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa kupatikana kwa ufumbuzi wa kudumu katika changamoto hiyo.

Mapema Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania Jenerali Venance Salvatory Mabeyo alitoa pongezi na shukurani kwa Rais Dk. Mwinyi kwa kutekeleza vyema uongozi wake uliotukuka tokea akiwa Waziri wa Ulinzi hadi hivi sasa akiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

Jenerali Mabeyo alitumia fursa hiyo kwa kumuaga rasmi Rais Dk. Mwinyi kufuatia kumaliza muda wake wa utumishi ndani ya Jeshi hilo utakaokamilika mwishoni mwa mwezi huu.

Katika maelezo yake Mkuu huyo wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania alieleza haja ya kuja kumuaga pamoja na kutoa shukurani kwa Rais Dk. Mwinyi na kueleza kuwa ni kiongozi ambaye amefanya kazi nae kwa muda mrefu na kumsaidia katika kutekeleza vyema majukumu yake ndani ya Jeshi hilo.

“Nakutakia afya njema na maisha marefu Mheshimiwa Rais pamoja na familia yako….nathamini sana ushirikiano ulionipa katika kipindi chako cha uongozi tokea ukiwa Waziri wa Ulinzi hadi leo hii, ahsate sana”, alisema Jenerali Mabeyo.

Mkuu huyo wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania alisema kuwa Jeshi la Ulinzi Tanzania litaendelea kumkumbuka Rais Dk. Mwinyi kwa busara na hekima zake katika kuzishughulikia changamoto mbali mbali ndani ya Jeshi hilo ambalo hatimae limepata mafanikio makubwa.

Alieleza kwamba katika uongozi wake Rais Dk. Mwinyi akiwa Waziri wa Ulinzi aliweza kutatua changamoto kadhaa sambamba na kulifanyia mambo mengi Jeshi hilo hatua ambayo imepelekea viongozi wa Jeshi hilo waendelee kufuata nyayo zake.

Alipongeza hatua zinazoendelea kuchukuliwa katika kutatua changamoto za ardhi na kueleza matarajio yake ya mafanikio yatakayopatikana katika kupata ufumbuzi wa kudumu wa changamoto hiyo.

Sambamba na hayo, alimpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa busara na hekima kubwa anayoendelea kutumia katika kuitafutia ufumbuzi wa kudumu changamoto hiyo ya ardhi hasa kwa kutambua kwamba Jeshi ni sehemu ya wananchi.

Imetayarishwa na Idara ya Mawasiliano,

Ikulu Zanzibar.  RESPONSIBILITY

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.