Na John Mapepele- Birmingham.
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa amezipongeza timu za Tanzania za KABBADI za wanaume na wanawake kwa kufuzu kuingia kwenye mashindano ya Kombe la Dunia.
Mhe. Mchengerwa ametoa pongezi hizo leo Julai 27, 2022 jijini Birmingham nchini Uingereza anakohudhuria mkutano wa mawaziri wa michezo kwa nchi za Jumuiya ya Madola.
Timu hizo za Taifa za wanaume na wanawake za mchezo wa KABBADI zipo nchini Misri kwenye mashindano hayo ya Afrika yaliyoanza Julai 22-28, 2022.
Timu hizo zimefuzu kwenye mashindano ya Dunia baada kushinda katika mashindano ya Afrika ya mchezo huo yanayofanyika nchini Misri.
Mashindano hayo yameshirikisha nchi mwenyeji Misri, Tanzania, Kenya, Nigeria, Mauritania, Somalia, Djibuti na Cameron.
Mashindano ya dunia ya mchezo huo yatakayofanyika Oktoba mwaka huu nchini India.
Kufuatia kufuzu kwa timu hizo za Tanzania kushiriki Kombe la Dunia, Tanzania sasa inaandika historia ya kupeleka timu nne kwenye mashindano ya Kombe la Dunia mwaka huu.
Timu nyingine zilizofuzu kuingia kwenye mashindano ya Kombe la Dunia ni pamoja na Timu ya Soka ya Taifa ya Wanawake chini ya umri wa miaka 17 (Serengeti Girls) na Timu ya Taifa wanaume ya Soka ya ya wenye ulemavu (Tembo Warriors).
No comments:
Post a Comment