Habari za Punde

Dk Mabodi avunja ngome ya Upinzani Pemba

NAIBU Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi,akizungumza na baadhi ya Wananchi wa Kijiji cha Kangagani Jimbo la Kojani katika ziara yake ya kikazi ya kuimarisha Chama Cha Mapinduzi  Pemba.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi,akikabidhi mabati 150 ya kuezekea Ofisi ya CCM Tawi la Mchanga Mdogo yaliyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Kojani Hamad Hassan Chande.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi,akipandisha Bendera ya CCM katika Maskani ya Dk. Tulia Ackson iliyopo kijiji cha Chwale Jimbo la Kojani Pemba.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi, akishiriki ujenzi wa Ofisi ya Tawi la Kiuyu Kigongoni Jimbo la Kojani.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi, akikata utepe katika ufunguzi wa Maskani ya CCM ya Dk.Tulia Ackson katika Kijiji cha Chwale Jimbo la Kojani.


NA IS-HAKA OMAR,PEMBA.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, kimeendelea kuvunja ngome ya ACT-Wazalendo baada ya kupandisha kwa mara ya kwanza bendera ya CCM katika kijiji cha Kiwani Soweto Jimbo la Kojani Pemba.

Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdulla Juma Mabodi, katika ziara ya kuimarisha Chama katika jimbo la Kojani katika kijiji cha Kiwani,alisema hatua ya wananchi wa kijiji hicho kujiunga na CCM na kukubali kupandisha bendera katika masikani ya kijiji hicho ni mafanikio makubwa ya kisiasa kisiwani humo.

Alisema dhamira ya CCM ni  kuvunja ngome za upinzani kisiwani humo  ili kuandaa mazingira rafiki ya kufuta upinzani na kushinda majimbo yote katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Dk.Mabodi, aliwahakikishia Wananchi hao kwamba wajitokeze kwa wingi bila hofu kujiunga na CCM kwa lengo la kunufaika na maendeleo endelevu yanayotokana na Utekelezaji mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020/2025.

Aliweka wazi kwamba Chama Cha Mapinduzi ndiyo taasisi pekee ya kisiasa yenye sera zinazotekelezeka kwa vitendo kwani kimeweka mizizi ya kushughulikia changamoto za wananchi kuanzia ngazi za Mashina hadi Taifa.

Alisema Serikali ya awamu ya nane chini ya Uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi, imetekeleza ahadi zilizotolewa katika kampeni za uchaguzi zilizopita.

Alieleza kwamba kijiji hicho kwa sasa kina huduma muhimu zikiwemo upatikanaji wa maji safi na salama, huduma za afya,elimu, kilimo,uvuvi na barabara.

Alisema taasisi hiyo inaongozwa na Viongozi wazalendo,waadilifu na wachapakazi wanaotekeleza kwa vitendo kila wanachokiahidi kwa wananchi.

Alisema njia pekee ya wananchi wa baadi ya maeneo ya Pemba yenye changamoto sugu ni kujiondoa na kukataa kwa vitendo kuendelea kutumiwa na vyama vya upinzania.

“Vyama vya upinzani vimeongoza majimbo kwa miaka mingi lakini bado wananchi wanalalamika kutopata maendeleo wanayoyataka, sasa CCM kwa sasa imepata nafasi ya kupata baadhi ya Wabunge na Wawakilishi wanachapa kazi na kuwaletea wananchi maendeleo wanayoyataka.

Ahadi yangu kwenu Wananchi wa Kiwani na maeneo mengi njooni CCM ni yetu wala msiogope vitisho,vurugu na vitisho sisi tupo tayari kukulindeni kwani tunaendeshwa na mfumo wa Demokrasia inayotoa uhuru wa kila mwananchi kuheshimiwa maamuzi yake ya kufuata Chama chochote cha kisiasa anachotaka hasa CCM”,. Alifafanua Dk.Mabodi.

Alielezea kufurahishwa na ujasiri na uzalendo wa Vijana na Wazee Masikani hiyo waliojikusanya pamoja na kuanzisha maskani yenye malengo endelevu mazuri ya kimaendeleo ambao wameshiriki kwa kiasi kikubwa kupandisha Bendera na kueneza siasa za CCM katika Jimbo hilo.

Katika maelezo yake Dk.Mabodi, aliutaka uongozi wa CCM ngazi za majimbo kuendeleza madarasa ya itikadi pamoja na kuhamasisha wananchi wengine kujiunga kwa wingi na CCM.

Naibu Dk.Mabodi, alimpongeza Mbunge wa jimbo la Kojani Mhe.Hamad Hassan Chande kwa kazi kubwa ya kuwapelekea maendeleo wananchi wa jimbo hilo kama Ilani ya Uchaguzi ya CCM inavyoelekeza.

Aliuagiza uongozi wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba kuhakikisha unapandisha hadhi Maskani ya CCM ya ‘’Umoja’’ na kuwa Tawi kamili kwa kufuata taratibu za Chama ili wananchi wa eneo hilo wapate Ofisi kubwa watakayofanya shughuli za kisiasa.

Naye Mbunge wa Jimbo la Kojani Hamad Hassan Chande, alisema hivi karibuni atakamilisha mradi mkubwa wa huduma ya maji safi na salama katika kijiji hicho kwa kuchimba kisima kikubwa kitakachomaliza suala la upungufu wa huduma hiyo.

Chande ambaye pia ni Naibu Waziri wa Wizara ya Fedha Tanzania, alisema ametekeleza ahadi alizotoa wakati wa uchaguzi mkuu uliopita kwa kiwango kikubwa katika sekta za afya,kilimo,maji safi na salama,michezo,uvuvi na kutekeleza wajibu wake katika ujenzi wa Ofisi mbali mbali za Chama na Jumuiya zake.

“ Wanachama wenzangu nitaendelea kutekeleza hatua kwa hatua changamoto zinazotokea katika maeneo yenu jambo la msingi ninalokuoombeni muendelee kuniamini kwani nyinyi ndio mlionipa ridhaa ya kukutumikieni”, alisema Mbunge Chande.

Akitoa ushuhuda Rashid Hamad Mjaka ambaye ni mkaazi wa kijiji cha Kiwani, amekili kuwa eneo hilo limekuwa na maendeleo makubwa kutokana na usimamizi mzuri wa sera za CCM inayoongoza Serikali ya awamu ya nane.

Mjaka,alisema wananchi wa eneo hilo wapo tayari kujiunga na CCM kwani kwa sasa wanapata huduma muhimu za kijamii tofauti na miaka iliyopita wakati jimbo hilo likiwa mikononi mwa viongozi wanaotokana vyama vya upinzani.

Alisema kijiji hicho kilikuwa ni miongoni mwa vijiji vilivyokuwa na changamoto nyingi za kijamii,kiuchumi na kimaendeleo ambazo hivi sasa zimetatuliwa.

Akitoa historia ya kijiji hicho alisema viongozi mbali mbali wa Chama Cha Mapinduzi na Serikali wamekuwa kitembelea kijiji hicho lakini hawakuwahi kupandisha bendera ya CCM lakini kwa sasa wananchi wameamua wenyewe kuchagua chama chenye maslahi kwa vizazi vya sasa na vijavyo.


 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.