Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania imepokea fedha kiasi cha Euro Milioni 10 kutoka kwa
Serikali ya Ujerumani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya
maendeleo ikiwa ni pamoja na mradi wa kupunguza migogoro baina ya binadamu na
Wanyamapori ambao una thamani ya Euro milioni 6.
Hayo yamesemwa na Naibu
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Juma S. Mkomi wakati wa hafla
fupi ya Kusaini Makubaliano Baina ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya
Ujerumani kwa ajili ya Utekelezaji wa Miradi hiyo katika ukumbi wa Mikutano wa
Benki Kuu leo jijini Dar es Salaam.
“Fedha hizi tulizopokea
kiasi cha Euro Milioni 6 zinalenga kutekeleza Mradi wa Kupunguza Migogoro baina
ya Binadamu na Wanyamapori katika wilaya mbalimbalii lakini hasa katika wilaya
88 ambazo zipo karibu na maeneo yaliyohifadhiwa” Bw. Mkomi amesisitiza.
Amefafanua kuwa katika
wilaya za Serengeti, Bunda Vijijini, Tunduru, Mwanga, Mvomero, Namtumbo na
Itilima kumekuwa na matukio mengi ya wanyamapori kusababisha madhara kwa
wananchi na mazao ukilinganishwa na wilaya nyingine.
Amesema hali hiyo
imesababisha hasara kubwa kwa wananchi, akitolea kwa mfano katika kipindi cha
miaka mitano (2017 - 2021), wastani wa wananchi 28,137 wamepata madhara
kutokana na wanyamapori ikijumuisha uharibifu wa mazao (ekari 56,972) yenye
thamani ya wastani wa shilingi bilioni 28, jumla ya wananchi 508 kujeruhiwa na
634 kuuawa na wanyamapori.
Ameweka bayana kuwa
mradi huo utakuwa na mchango mkubwa katika kupunguza migongano kati ya binadamu
na wanyamapori nchini na kuihakikishia Serikali ya Ujerumani kwamba fedha hizo
zitatumika kwa lengo lililokusudiwa na si vinginevyo.
Aidha, ameishukuru
Serikali ya Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani kwa misaada inayoendelea kuitoa
hususan katika maeneo yanayohusiana na uhifadhi wa maliasili.
Fedha zilizobakia Euro
milioni 4 zitatumika katika kutekeleza mradi wa kuwezesha upatikanaji wa haki
za wanawake na watoto na mradi wa kuandaa maandiko ya kitaalamu na kufanya
tafiti .
Hafla hiyo imehudhuriwa
na Balozi wa Jamhuri ya Shiikisho la Ujerumani, Mhe. Bi. Regine Hess, Katibu
Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango,Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na
Sheria; Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Wizara ya Maliasili na
Utalii,Viongozi wa GIZ pamoja na Maafisa wa Serikali za Tanzania na Ujerumani.
No comments:
Post a Comment