Habari za Punde

Kuna Umuhimu wa Kufikiria Njia Muafaka na Mbadala za Kuendesha Biashara ya Utalii Nchini

 

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Massoud Othman  akizungunza katika ufunguzi wa Kongamano la Maazimisho ya Siku ya Utalii duniani huko hoteli ya Park Hayati shangani Mjini Zanzibar leo tarehe 27.09.22.
 ( Picha na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Kitengo cha Habari).

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, amesema kuna umuhimu wa kufikiria njia muafaka na mbadala za kuendesha  biashara ya utalii nchini, ili kujikwamua kwa haraka, kutoka pahala  ulipo sasa na kuweza kupiga hatua zaidi.

Mhe. Othman ameyasema hayo huko hoteli ya Park Hayat mjini Zanzibar alipohutubia katika ufunguzi wa Kongamano la kuazimisha siku ya Utalii Duniani inayofanyika kila tarehe 27 Septemba ya kila mwaka.

Amefahamisha kwamba  kufanya hivyo ni kwenda sambamba na maudhui ya kauli mbiu ya mwaka huu ya siku ya Utalii  mwaka huu unaosema na kuhimiza kufikiria upya sekta ya Utalii ambao unakwenda na wakati ikizingatiwa kwamba utalii umepita katika kipindi kigumu cha maradhi ya Korona duniani kote.

 Amesema kwamba taarifa za kiutafiti zinaonesha kwamba uchumi wa Zanzibar  kupitia sekta ya  Utalii unachangia asilimia 29.2 ya Pato la Taifa kwa Zanzibar, ambazo hazifikiwi na sekta nyengine yoyote ya uzalishaji hapa nchini.

Aidha amesema kwamba utalii, ni Sekta mtambuka inayotegemeana au kutegemewa na sekta nyengine zote nchini, zikiwemo za ajira, miundombinu, nishati, uchumi wa buluu, na kilimo, na hata upatikanaji wa huduma za kijamii na kwamba kuna ulazima kwa sekta zote kujumuika pamoja katika kuendeleza utalii ili uimarike zaidi.

Mhe. Othman amesema kwa muda sasa, Zanzibar imekuwa  ikitegemea zaidi utalii wa mahoteli, bahari na fukwe, na kuacha kutumia bidhaa nyingi za kitalii zilizopo Unguja na Pemba.

Hata hivyo, Mhe. Othman amesema umefika wakati kwa  Zanzibar kuacha kujitangaza kama ni kituo cha utalii cha Jua, Mchanga na Bahari  pekee,  bali  itumie pia vivutio vya kiutamaduni, historia, vyakula, dini, na matibabu , ambavyo vinajipambanua na nchi nyengine kwa vile havipatikani popote duniani isipokuwa Zanzibar.

Mhe. Makamu amesema  kongamano hilo litachangia, kwa kiasi kikubwa, kuuamsha ‘ulimwengu wa kitalii’ kwamba Zanzibar iko tayari kuwapokea watalii, muda wowote , sambamba na kutekeleza itifaki ya Kudhibiti Maambukizi ya KORONA  Zanzibar kwa mashirikiano baina ya Sekta binafsi na Serikali.

Hata hivyo Mhe. Othman ametoa wito  kwamba, Kongamano hilo  litumike kuleta hamasa kwa wananchi wa Zanzibar kushiriki katika utalii ili kunufaika nao, badala ya kuendelea kubakia kuwa mashahidi wa utalii.

Aidha, amewashajiisha wawekezaji wa Sekta ya Utalii, kutoa kipaumbele kwa wananchi wa Zanzibar, katika ajira na fursa nyenginezo za kiuchumi na kimaendeleo, kupitia makampuni na mashirika wanayoyasimamia.

Naye waziri wa Utalii na Mambo ya Kale  Mhe. Simai Mohammed Said amesema kwamba  kwa kushirikiana na wadau  mbali mbali  wa utalii wataendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika kukuza sekta ya Utalii Zanzibar ili ulete tija zaidi kwa taifa.

Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar kupitia Kitengo cha Habari leo tarehe 27.09.22.


Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Massoud Othman  akizungunza katika ufunguzi wa Kongamano la Maazimisho ya Siku ya Utalii duniani huko hoteli ya Park Hayati shangani Mjini Zanzibar .

Washiriki wa Kongamano la maazimisho ya Siku ya Utalii duniani hapa Zanzibar linalofanyika katika hoteli ya Park Hayat Shangani Zanzibar wakifuatilia kwa makini hotuba ya Mhe. Othman Masoud Othman ambaye alikuwa mgeni rasmi katika Kongamano hilo

Washiriki wa Kongamano la maazimisho ya Siku ya Utalii duniani hapa Zanzibar linalofanyika katika hoteli ya Park Hayat Shangani Zanzibar wakifuatilia kwa makini hotuba ya Mhe. Othman Masoud Othman ambaye alikuwa mgeni rasmi katika Kongamano hilo


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.