Habari za Punde

Serikali Yakabidhi Hati za Kimila Mkalama Kupitia Mradi wa LDFS.Serikali yang’ara matumizi bora ya ardhi

 

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mkalama mkoani Singida Mhe. James Mkwega akikabidhi hati ya kwa mmoja wa wanakijiji cha Mpambala wilayani kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais. 

Mratibu wa Mradi Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) Bw. Joseph Kihaule (katikati) na Meneja wa Kanda ya Kati wa Tume ya Taifa ya Mipango na Matumizi ya Ardhi Bi. Suzana Mapunda (kulia) wakihakiki hati ya kimila ya mmoja ya wananchi wa Kijiji cha Mpambala wilayani Mkalama mkoani Singida wakati wa hafla ya utoaji wa hati za kimila kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.

Sehemu ya wananchi wa Kijiji cha Mpambala wilayani Mkalama mkoani Singida wakiwa katika hafla ya kukabidhi hati za kimila kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.

Sehemu ya wananchi wa Kijiji cha Mpambala wilayani Mkalama mkoani Singida wakiwa wameshika hati za kimila wakati wa picha ya pamoja mara baada ya kukabidhiwa hati hizo kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.

(PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS)

Imeelezwa kuwa Tanzania ni mojawapo ya nchi mbili kati ya 12 za Afrika zilizofanya vizuri zaidi katika utoaji wa hati za kimila za matumizi bora ya ardhi.

 

Hayo yamebainishwa na Mratibu wa Mradi wa kitaifa Bw. Joseph Kihaule wakati wa hafla ya kukabidhi hati za kimila 550 kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) katika Kijiji cha Mpambala wilayani Mkalama mkoani Singida.

Aliwahimiza wananchi waendelee kupata hati hizo kwani mafanikio makubwa yameonekana katika eneo na kusababisha baadhi ya nchi kuiga utaratibu huo ambao umeonesha mafanikio makubwa.

Aidha, Kihaule alisema pamoja na utoaji wa hati hizo za kimila, msitu wa Munguli uliopo katika Kata ya Mwangeza umelengwa kupatiwa hati miliki ya kimila ili uingizwe kwenye biashara ya hewa ya ukaa ambayo itakuwa chanzo cha mapato.

“Msitu huo utasaidia kunyonya hewa ya ukaa na biashara hiyo kama mnavyofahamu wawekezaji wamekuwa wakifika nchini mwetu kuonesha nia ya kufanya baishara hiyo,” alisema Kihaule.

Aliongeza kuwa yapo mafanikio makubwa katika zoezi la ugawaji wa hati za kimila ambapo tayari zimetolewa hati za kimila za mfano 750 katika wilaya ya Magu mkoani Mwanza, 600 wilayani Nzega mkoani Tabora.

Hata hivyo, hati za kimila 351 zilizobakia kati ya 901 zinatarajiwa kutolewa kwa wananchi wa Kijiji cha Mwangeza kupitia mradi huo na hivyo kupunguza changamoto ya migogoro ya matumizi ya ardhi.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mkalama Mhe. James Mkwega alitoa shukrani kwa Ofisi ya Makamu wa Rais inayoratibiwa mradi huo na kusema umekuja wakati muafaka kwa wananchi wilayani humo.

Alisema kuwa kutokana na changamoto ya ukame inayokabili wilaya hiyo hususana katika kijiji hicho, mradi huo utakuwa na manufaa ambayo yameanza kuonekana ikiwemo kuimarika kwa kilimo cha mpunga na ufugaji nyuki.  

Mhe.Mkwega alisema upatikanaji wa hati za kimila utasaidia kupunguza migogoro ya matumizi ya ardhi katika maeneo ya wanufaika ambao wamekuwa wakitumia muda mrefu kufuatilia mashauri badala ya kuzalisha.

Aidha, mwenyekiti huyo alitoa wito kwa wananchi hao kufuata mpango wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo yao ili kuwa na maendeleo endelevu katika matumizi ya ardhi.

Kwa upande wao wananchi wa kijiji cha Mpambala walionufaika na hati hizo za kimila, Bi. Regina Edward alisema zitasaidia kupunguza migogoro ya ardhi na kufaidika na fursa za mikopo kwa ajili ya maendeleo.

Nae Simon Mluta alishukuru Mradi wa LDFS ambao pia unawachimbia visima na majosho ambayo yatasaidia kuondoa changamoto ya uhaba wa maji kutokana na ukame.

Mradi huo unatekelezwa katika halmashauri tano hapa nchini zikiwemo Magu (Mwanza), Nzega (Tabora), Kondoa (Dodoma), Mkalama (Singida) na Micheweni (Pemba).

 


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.