Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mkalama mkoani Singida Mhe. James Mkwega akikabidhi hati ya kwa mmoja wa wanakijiji cha Mpambala wilayani kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.
Mratibu wa Mradi Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa
Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) Bw. Joseph Kihaule (katikati) na
Meneja wa Kanda ya Kati wa Tume ya Taifa ya Mipango na Matumizi ya Ardhi Bi.
Suzana Mapunda (kulia) wakihakiki hati ya kimila ya mmoja ya wananchi wa Kijiji
cha Mpambala wilayani Mkalama mkoani Singida wakati wa hafla ya utoaji wa hati za kimila
kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi
iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF)
unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.
Sehemu ya wananchi wa Kijiji cha Mpambala wilayani Mkalama mkoani Singida wakiwa wameshika hati za kimila wakati wa picha ya pamoja mara baada ya kukabidhiwa hati hizo kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.
(PICHA NA OFISI YA MAKAMU WA RAIS)
Imeelezwa kuwa Tanzania ni mojawapo ya nchi mbili kati ya 12 za Afrika zilizofanya vizuri zaidi katika utoaji wa hati za kimila za matumizi bora ya ardhi.
Hayo
yamebainishwa na Mratibu wa Mradi wa kitaifa Bw. Joseph Kihaule wakati wa hafla
ya kukabidhi hati za kimila 550 kupitia Mradi wa Kurejesha Ardhi iliyoharibika na Kuongeza
Usalama wa Chakula katika Maeneo kame nchini (LDSF) katika Kijiji cha Mpambala
wilayani Mkalama mkoani Singida.
Aliwahimiza wananchi waendelee kupata hati hizo kwani mafanikio makubwa
yameonekana katika eneo na kusababisha baadhi ya nchi kuiga utaratibu huo ambao
umeonesha mafanikio makubwa.
Aidha, Kihaule alisema pamoja na
utoaji wa hati hizo za kimila, msitu wa Munguli uliopo katika Kata ya Mwangeza umelengwa
kupatiwa hati miliki ya kimila ili uingizwe kwenye biashara ya hewa ya ukaa
ambayo itakuwa chanzo cha mapato.
“Msitu huo utasaidia
kunyonya hewa ya ukaa na biashara hiyo kama mnavyofahamu wawekezaji wamekuwa
wakifika nchini mwetu kuonesha nia ya kufanya baishara hiyo,” alisema Kihaule.
Aliongeza kuwa yapo
mafanikio makubwa katika zoezi la ugawaji wa hati za kimila ambapo tayari
zimetolewa hati za kimila za mfano 750 katika wilaya ya Magu mkoani Mwanza, 600
wilayani Nzega mkoani Tabora.
Hata hivyo, hati za
kimila 351 zilizobakia kati ya 901 zinatarajiwa kutolewa kwa wananchi wa Kijiji
cha Mwangeza kupitia mradi huo na hivyo kupunguza changamoto ya migogoro ya
matumizi ya ardhi.
Mwenyekiti wa
Halmashauri ya Mkalama Mhe. James Mkwega alitoa shukrani kwa Ofisi ya Makamu wa
Rais inayoratibiwa mradi huo na kusema umekuja wakati muafaka kwa wananchi
wilayani humo.
Alisema kuwa kutokana
na changamoto ya ukame inayokabili wilaya hiyo hususana katika kijiji hicho,
mradi huo utakuwa na manufaa ambayo yameanza kuonekana ikiwemo kuimarika kwa kilimo
cha mpunga na ufugaji nyuki.
Mhe.Mkwega
alisema upatikanaji wa hati za kimila utasaidia kupunguza migogoro ya matumizi
ya ardhi katika maeneo ya wanufaika ambao wamekuwa wakitumia muda mrefu
kufuatilia mashauri badala ya kuzalisha.
Aidha,
mwenyekiti huyo alitoa wito kwa wananchi hao kufuata mpango wa matumizi bora ya
ardhi katika maeneo yao ili kuwa na maendeleo endelevu katika matumizi ya
ardhi.
Kwa upande wao wananchi wa
kijiji cha Mpambala walionufaika na hati hizo za kimila, Bi. Regina Edward
alisema zitasaidia kupunguza migogoro ya ardhi na kufaidika na fursa za mikopo
kwa ajili ya maendeleo.
Nae Simon Mluta alishukuru
Mradi wa LDFS ambao pia unawachimbia visima na majosho ambayo yatasaidia
kuondoa changamoto ya uhaba wa maji kutokana na ukame.
Mradi huo unatekelezwa
katika halmashauri tano hapa nchini zikiwemo Magu (Mwanza), Nzega (Tabora), Kondoa
(Dodoma), Mkalama (Singida) na Micheweni (Pemba).
No comments:
Post a Comment