TAARIFA
KWA UMMA
DODOMA, 22
Desemba, 2022 – BENKI ya Dunia imeiidhinishia Tanzania, mkopo wenye
masharti nafuu pamoja na msaada vyote vikiwa na thamani ya dola za Marekani
milioni 775 (Sawa na takriban shilingi za Tanzania trilioni 1.8), kwa ajili ya
kusaidia utekelezaji wa bajeti, kuboresha uchumi na huduma za afya.
Mchanganuo wa fedha hizo unaonesha kuwa Shirika la Kimataifa la Maendeleo
(IDA) litatoa mkopo wa dola za Marekani milioni 500 (sawa na shilingi trilioni 1.1)
kwa ajili ya kufufua uchumi ulioathiriwa na UVIKO-19 na Vita vinavyoendelea
baina ya Ukraine na Urusi, vilivyosababisha kusinyaa kwa shughuli za kiuchumi
na kupanda kwa bei ya bidhaa zinazoagizwa kutoka nje yakiwemo mafuta na bidhaa
nyingine.
Dola milioni 250 (sh. bilioni 581) zitatumika kwa ajili ya program ya
afya ya mama na mtoto kwa njia ya kupima matokeo (PfoR) inayotekelezwa Tanzania
Bara na dola za Marekani milioni 25 (sh. bilioni 58.1) zilizotolewa kama msaada
na Mfuko wa Dunia wa kusaidia wanawake, vijana na watoto zitatumika kwa ajili
ya mradi wa uwekezaji kiuchumi (IPF) kwa upande wa Zanzibar.
“Tumekubaliana na Benki ya Dunia kwamba fedha hizo ambazo zitaanza
kuingia nchini kuanzia kesho (Ijumaa) zitaelekezwa katika kuiwezesha sekta
binafsi kushiriki katika kukuza uchumi, kuziwezesha sekta za fedha kuwa na
uwezo wa kukopesha sekta hiyo, kuimarisha uwazi na uwajibikaji Serikalini,
kuboresha kilimo pamoja na kutatua changamoto za afya ya mama na mtoto” alisema
Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango wa Tanzania.
Benki ya Dunia imetoa fedha za msaada wa kibajeti baada ya kipindi cha
miaka 8 ambapo mara ya mwisho Tanzania ilinufaika na mpango huo mwaka 2014,
baada ya kuridhishwa na utekelezaji na usimamizi mzuri wa sera za kiuchumi na
kifedha, uwazi na uwajibikaji, katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita,
inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tazania.
Katika Taarifa yake Benki ya Dunia, imeipongeza Tanzania kwa usimamizi
makini wa uchumi wake licha ya kuwepo kwa athari hizo za UVIKO 19 na Vita ya
Ukraine na Urusi, ambapo uchumi wake umeimarika na kupigiwa mfano na Taasisi
hizo kubwa za Fedha Duniani, ikiwemo Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la
Kimataifa (IMF).
Imetolewa na:
Benny
Mwaipaja
Mkuu wa
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
No comments:
Post a Comment