Habari za Punde

Maonesho ya Utalii na Uwekezaji Zanzibar Yatatoa Mchango Mkubwa wa Kukuza Sekta ya Utalii Zanzibar.na Kuangalia Mandhari Nzuri na Vivutio vya Utalii

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia na kuyafungua Maonesho ya Utalii na Uwekezaji Zanzibar, yanayofanyika katika viwanja vya Makumbusho Mnazi Mmoja “Baitul Amaan” Wilaya ya Mjini Unguja Jijini Zanzibar leo 9-2-2023

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameihakikishia dunia kwamba Zanzibar ipo salama haina viashiria vyovyote vya kutishia amani kwa wenyeji na wageni wakakaoitembela.

Dk. Mwinyi aliyasema hayo alipofungua maonesho ya Utalii na  Uwekezaji kwenye ukumbi wa Makumbusho ya Beit el Aman, Mnazi Mmoja - Zanzibar.

Alisema maonesho hayo yatatoa mchango mkubwa wa kukuza sekta ya utalii Zanzibar na kuwaomba wageni na watalii kutoa shaka kwa kutembelea visiwa vya Unguja na Pemba kuangalia mandhari nzuri na vivutio vya utalii vilivyomo.

Nachukua nafasi hii kuihakikishia dunia kwamba Zanzibar ni salama hakuna tukio au viashiria vyovyote vya kutishia usalama wa wageni na wenyeji,  kwa wale wote waliopanga kuitembelea nchi yetu tunawakaribisha na wale ambao bado hawajafanya maamuzi ya wapi watembelee, basi nawashauri waichague Zanzibar iwe ni sehemu yao ya mapumziko kwa msimu huu” Alieleza Dk. Mwinyi.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ziko imara kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa salama na yenye amani kwa wenyeji na wageni wanaoitembelea.

Rais Dk. Mwinyi alieleza, mwishoni mwaka jana jumla ya watalii 548,503 waliingia Zanzibar ikilinganishwa na wageni 260,644 waliongia mwaka 2020 kufuatia athari za janga la UVIKO-19 lililoathiri sekta ya utalii nchini na dunia kwa ujumla na kuongeza Zanzibar kama sehemu ya dunia iliathirika kwa shughuli zote za utalii zilisimama kwa takriban miezi saba kuanzia mwezi Machi  mwaka 2019. Alielza hali sasa inaendelea kuimarika kwa watalii wengi kuingia nchini.

Dk. Mwinyi aliitaka Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale kupitia Kamisheni ya Utalii kushirikiana na Jumuiya za wafanyabiashara za utalii kujipanga upya na hatimae kuja na mpango madhubuti wa kuzitumia fursa za biashara ya utalii zilizopo Zanzibar. Aidha, aliipongeza Wizara hiyo kwa kazi nzuri ya kuimarisha Utalii nchini. Sambamba na kuwahimiza kuongeza ubunifu wa kuibua vivutio vipya ikiwemo utalii wa matamasha, mikutano ya kimataifa, makongamano na utalii wa michezo ya baharini.

Pia aliishukuru sekta binafsi kwa kuendelea kutangaza utalii wa Zanzibar pamoja na kutoa huduma nzuri zinazosaidia kuitangaza Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Alisema ushirikiano wa pamoja unahitajika baina ya Serikali na sekta binafsi kwa kufanyakazi pamoja katika kuzitumia vyema fursa za biashara ya utalii zilizopo nchini.

“Natoa pongezi na shukrani kwa Balozi zetu zote zilizo nje ya nchi kwa kufanya juhudi kubwa za kuvutia watalii kuja nchini” Alipongeza Rais Mwinyi.

Akizungumzia utalii endelevu na umuhimu wa kutunza mazingira, Rais Dk. Mwinyi alieleza maonesho hayo pia yanalenga maudhui ya Zanzibar ya kijani yenye kusadifu utalii endelevu wenye urithi tofauti wa kimaumbile, utamaduni na historia hai pamoja na kuonesha uwiano uliopo baina kutunza mazingira hai, uchumi,  jamii na utamaduni ambao ni muhimu kwa maendeleo ya sekta ya utalii na uhifadhi wa mfumo wa ikolojia.

Alisema, dhamira ya Serikali ni kutunza mazingira na kuhakikisha shughuli za utalii na uwekezaji  zinaekewa mikakati mizuri ili kulinda mazingira na utamaduni za wazawa kwa kuongeza mapato yatokanayo na sekta ya utalii na uwekezaji nchini.

Hata hivyo, Dk. Mwinyi aliwataka wageni waliopo nchini kufurahia ukarimu wa watu wa Zanzibar pamoja na kuwataka kuwa mabalozi wazuri watakaporejea kwenye mataifa yao kwa kueleza mambo mazuri waliyoyashuhudia Zanzibar.

Naye, Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale.Mhe. Simai Mohammed Said aliwataka wananchi wa Zanzibar kupenda kununua na kutumia bidhaa zinazozalishwa na kutengenezwa nchini ili kuzifanya pesa kuendelee kuzunguruka na kuongeza uzalishaji.

“Tukifanya hivyo thamani ya pesa itaendelea kubakia ndani itazunguruka kwa watu wetu, tuekeze sana na kutengeneza fedha nyingi ili kuboresha maisha ya watu kwaalili ya maisha mazuri kwao yatokanayo na faida ya utalii, Zanzibar”

Akizungumzia miundombinu ya mawasiliano na barabara, Waziri Simai alieleza barabara nyingi za mji wa Zanzibar hazivutii kwa utalii, hivyo alizishauri mamkala husika kwa sasa waziboreshe na kupanda miti, bustani na maua mengi kwaajili ya kuwavutia wageni wanaofika nchini kwa uzuri na mvuto wa mwonekano wa kijani na maua hivyo aliwashauri Wakuu wa Mikoa na Wilaya pamoja nawadau wa Utalii kuishawishi jamii juu umuhimu wa kuzitunza na kuzienzi barabara na maeneo yote ili Zanzibar iboreke na kuwa na mvuto wa kipekee kwa watalii.

Waziri Simai alielekeza miti mingi ipandwe kwenye barabara kuu za miji, ambako watalii wengi hupita na kuona mandhari halisi ya mji wa Zanzibar.

Alimuahidi Rais Dk. Mwinyi kwamba watashirikiana na taasisi nyengine za serikali zikiwemo Wizara  ya utalii, usafirishaji na mawasiliano, Ardhi, Afya na wadau wengine wa utalii kufanya kazi kama timu moja ili kuungamkono jukudi za serikali kwenye kufikia lengo la utalii endelevu nchini na kufanikisha malengo ya utalii kwa ajili ya kizazi kijacho

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar, Rahim Baloo aliyataka mashirika ya ndege ya kimataifa kuungamkono juhudi za Serikali kwa kuongeza safari za moja kwa moja kutoka mataifa makubwa kutua Zanzibar hali aliyoieleza itaifungua Zanzibar kwenye soko la kimataifa la utalii.

Alisema maonesho hayo yataifungulia milango Zanzibar kwenye soko la kimataifa hadi kwa mataifa ya kusini na kaskazini mwa bara la Amerika.

Maonesho hayo ya siku tatu yanatarajiwa kuhudhuriwa na zaidi ya washiriki 200 kutoka mataifa mbalimbali zikiwemo nchi za Algeria, Argentina, Brazil, Marekani na kwengineko.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.