Habari za Punde

Tanzania Mwenyekiti wa Sekta ya Uvuvi na Uchumi wa Buluu katika Jumuiya ya Nchi za Afrika,Karibiani na Pasifiki

Dodoma, 15 Februari 2023

Tanzania imekabidhiwa rasmi uenyekiti wa Sekta ya Uvuvi na Uchumi wa Buluu katika Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS) kwenye hafla fupi iliyofanyika Makao Makuu ya Jumuiya hiyo yaliyopo jijini Brussels, Ubelgiji tarehe 13 Februari 2023.

Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, kwenye Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya OACPS, Mhe. Jestas Abuok Nyamanga alikabidhiwa rasmi Uenyekiti wa Sekta hiyo kwa ngazi ya mabalozi na Balozi wa Ghana nchini Ubelgiji, Mhe. Harriet Sena Siaw-Boateng ambaye nchi yake imemaliza muda wa uenyekiti.

Uamuzi wa Tanzania kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa sekta hiyo ulifikiwa katika Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Nchi Wanachama wa OACPS uliofanyika Brussels, Ubelgiji, Mwezi Juni 2022. Uenyekiti wa Tanzania utakuwa kwa ngazi mbili ambazo ni za Mabalozi wa Jumuiya waliopo Brussels na Mawaziri wenye dhamana ya sekta ya uvuvi na uchumi wa buluu ndani ya Jumuiya na utadumu kwa miaka miwili hadi Februari 2025.

Tanzania katika kipindi cha uongozi wake imejipanga kikamilifu kusimamia utekelezaji wa masuala mbalimbali katika Jumuiya ikiwa ni pamoja na kuweka mikakati madhubuti na mazingira ya kuwezesha wananchi kupitia nchi zao kunufaika ipasavyo na uchumi wa buluu ikiwemo uvuvi na rasilimali zingine za majini; kuchochea uwekezaji katika sekta ya uchumi wa buluu; kujenga uwezo na matumizi bora ya sayansi na teknolojia; kuongeza wigo wa masoko kwa bidhaa zitokanazo na uvuvi na uchumi wa buluu; kupambana na uvuvi haramu; na kuendeleza juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Aidha, katika kipindi husika, Tanzania itakuwa na jukumu la kuandaa  Mkutano wa Mawaziri wa OACPS wenye dhamana ya masuala ya Uvuvi ambao unatarajiwa kufanyika nchini Tanzania mwaka 2024.

Miongoni mwa sababu zilizopelekea Tanzania kuchaguliwa katika nafasi hiyo ni kutokana na kuongozeka kwa ushawishi wake ndani ya Jumuiya ya OACPS na kuthamini utayari, dhamira na hatua thabiti zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuchochea na kusimamia masuala mbalimbali ya kitaifa na kimataifa ikiwemo yale yanayohusu sekta ya uvuvi na uchumi wa buluu kwa ujumla.

                                                      Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali.     

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.