Habari za Punde

Stop GBV Half Marathon kufanyika Novemba 26 Zanzibar

Mwenyekiti wa TAASISI ya Asma Foundation Asma  Mwinyi akitoa taarifa kwa umma kuhusiana na mbio za marathon (Stop GBV half marathon)  zinazotarajiwa Kufanyika November 26 mwaka huu,kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Vijana, utamaduni na Michezo Fatma Hamad Rajab
Mwenyekiti wa TAASISI ya Asma Mwinyi Foundation akitolea ufafanuzi baadhi ya maswali ya Waandishi wa habari wakati akitoa taarifa kwa umma juu ya mbio za marathon (Stop GBV half marathon)  zinazotarajiwa Kufanyika November 26 mwaka kulia ni Makamo Mwenyekiti chama cha riadha Zanzibar Masoud Tawakkal khayrallah

Katibu kamati ya ufundi chama cha riadha Zanzibar Makame Ali akitolea ufafanuzi baadhi ya maswali ya Waandishi wa habari  wakati wa mkutano na waandishi hao kuhusiana na mbio za marathon (Stop GBV half marathon)  zinazotarajiwa Kufanyika November 26 mwaka huu.

PICHA NA FAUZISA MUSSA- MAELEZO ZANZIBAR

Na Sheha Haji Sheha – Maelezo-06/10/2023

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mgeni rasmi katika mbio za stop GBV Half Marathon zitakazofanyika Novemba 26 mwaka huu hapa Zanzibar.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mwenyekiti wa Taasisi ya Asma Mwinyi Fondesheni Bi Asma Mwinyi huko Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wakati alipokuwa akitoa taarifa kwa wandishi wa habari juu ya ujio wa  mbio hizo.

Amesema mbio hizo ni za kipekee katika ukanda huu wa Afrika ya Mashariki ambazo zitawashirikisha watu tafauti kwa dhamira ya kuwasaidia watu wenye mahitaji maalum.

Bi Asma aliwataka wananchi wa Zanzibar kushiriki katika mbio hizo ikiwa ni fursa kwao kuwaunga mkono watu wenye mahitaji maluum wakiwemo wajane.

“Mbio zetu hizi sio za kawaida kama ilivyozoeleka, mbio hizi zinatambulika ulimwengu mzima, ukienda katika kalenda ya ulimwengu  utaiona stop GBV half marathon Zanzibar”, alieleza Mwenyekiti huyo.

Bi Asma Mwinyi alimshukuru Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suhuhu Hassan kwa mchango wake anaoutoa kwa Taasisi hiyo pamoja na kuwaunga mkono na kukubali kuwa yeye ndio mgeni rasmi wa mbio hizo.

Nae Ndugu Makame Ali kutoka Chama cha Riadha Zanzibar alisema mbio hizo zitajumuisha washiriki kwa kilomita 21, kilomita 10 na kilomita 5 kutoka ndani na nje ya Zanzibar hivyo wamezingatia vigezo vya kimataifa na kanuni za usalama ili kufanikisha vyema mbio hizo

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.