Habari za Punde

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Azungumza na Uongozi wa Bodi ya Uhasibu Zanzibar

Na. Mwandishi na OMKR. 

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, amesema kwamba Zanzibar inazo rasilimali za kutosha kuweza kuzalisha fedha nyingi, lakini zinahitaji kuingizwa kwenye Mfumo rasmi wa kiuchumi utakaosaidia ukuzaji uchumi ili kuleta maendeleo ya haraka.

Mhe. Othman ameyasema hayo ofisini kwake Migombani mjini Zanzibar alipozungunza na Uongozi wa Taasisi ya Wahasibu, Wakaguzi na Washauri Elekezi wa Kodi Zanzibar waliongozwa na  Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Taasisi hiyo ndugu Juma Amour Mohammed walofika ofisini kwa Makamu kujitambulisha baada ya taasisi hiyo kundwa hivi karibuni.

Mhe. Makamu amesema kwamba kuwepo kwa chombo hicho ni muhimu katika kusimamia maendeleo ya ukuzaji uchumi wa kileo hapa Zanzibar na duniani kwa jumla, lakini lazima rasilimali za kifedha zilizopo  kuingizwa katika mfumo nzuri na sahihi ili kuongeza uwezo wa rasilimali fedha zinaopatikana katika biashara  na uwekezaji wa aina mbali mbali.

Amefahamisha kwamba nchi nyingi duniani zimeweza kupiga hatua kubwa ya kiuchumi na kimaendeleo kutokana na kuwepo mifumo na taratibu bora inayowezesha fedha kupatikana kwa wingi kwa vile wawekezaji watajenga imani sahihi na mifumo iliyopo nchini.

Aidha amesema kwamba chombo hicho pia ni muhimu katika kusaidia kuwawezesha wataalamu wa ndani wa kada za fedha, biashara na ukaguzi wanaoweza kusimamia vyema taaluma yao kiushindani katika ngazi za kitaifa na kimataifa na hivyo nchini kunufaika katika suala zima la ajira kwa ndani na nje ya nchi.

Mhe. Othman ametahadharisha Taasisi hiyo kwamba kunahaja ya kuwajengea uwezo wanaaluma wao,  sio tu kwa kuzingatia viwango vya elimu ya darsani, lakini pia kuthamini wenye ujuzi na maarifa mapana ya kuweza kutambua na kumudu vyema majukumu yao kupitia mawanda mapana waliyonayo katika kuifahamu mifumo na taratibu za dunia za kiuchumi unaolenga ushindani kwenye shughuli za kibiashara na uzalishaji ndani nanje ya nchi.

Akizungunzia suala la taaluma ya Kodi ,Mhe. Othman ameutaka uongozi wa Taasisi hiyo kuhakikisha kwamba wanawajenga wanataaluma hiyo katika misingi mipya ya kodi  itakayowezesha kusaidia kuchangia ukuaji wa uchumi wa Zanzibar kwa haraka kama zilivyoweza kufanikiwa nchi nyengine mbali mbali duniani.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Taasisi hiyo ya Wahasibu, Wakaguzi na Washauri Elekezi wa Kodi Zanzibar ndugu Juma Amour Mohammed kwamba Taasisi hiyo inalenga kuijenga kada hiyo katika kufuata na kuzingatia maadili ya kifedha ambayo yameonekana kupotea.

Aidha amesema kwamba watendaji wengi walikosa kujiamini na kutokuwepo uadilifu katika utendaji wa majukumu yao ikiwemo uandishi wa ripoti za kifedha na kwamba kuwepo kwa taasisi hiyo kutawezesha kusimamia vyema maadili na taaluma ya kiuhasibu  Zanzibar.

Amefahamisha kwamba kadri siku siku zinavyokwenda mbele  kunaendelea kutokea mabadiliko makubwa katika kada ya fedha na biashara na ndio maana  tayari hapa Zanzibar kumeanzishwa benki za kiislamu na bima zinazozingatia misingi ya kislamu mambo ambayo yanahitaji kujengewa uwezo ili shunguli za kitaaluma ziweze kufanyika vyema na kufikia lengo la ufanisi.

Naye Mkurugenzi  wa Taasisi hiyo ndugu Ame Burhan Shadhili amesema kwamba ofisi hiyo inakusudia kuongeza ubora wa huduma zinazotolewa na wanachama wa taasisi kwa kuwa awali hakukua na chombo kama hiyo lakini huduma za namna hiyo zilitumiwa kutoka tanzania bara.

Wakati huo huo Mhe. Othman amekabidhi fedha Taslim shilingi milioni mbili na laki tano kwa Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo Mhe. Tabia Maulid Mwita ikiwa ni utekezaji wa ahadi yake ya kuwazawadia Timu ya vijana ya Umri wa Chini ya miaka 15 kufuatia ushindi wao wa hivi karibuni walipoifunga timu ya Uganda mabao Manne kwa matatu kwa mikwaju ya penaliti katika mashindano ya CECAFA baada ya mchezo huo awali kutoka suluhu ya bao moja kwa moja na Zanzibar kuibuka washindi kwa penalty.

Akipokea fedha hizo waziri wa Habari Utamaduni na Michezo Taiba Maulid Mwita amesema kwamba mafanikio yaliyopatikana kwa timu hiyo yametokana na mashirikiano ya viongozi na wananchi mbali mbali jambo ambalo limeleta faraja sana kwa vijana.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.