Habari za Punde

Wanaojiandikisha kuwa wapiga kura zaidi ya mara moja kutumikia kifungo jela

 Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji (Rufaa) Jacobs 

Mwambegele (katikati) akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 25 Julai, 

2024 mkoani Geita. Kulia ni Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume, Bw. Kailima 

Ramadhan na kushoto ni Mjumbe wa Tume, Mhe. Jaji wa Mahakama Kuu, Asina 

Omar.

 Na. Mwandishi Wetu, Geita.

Wananchi watakaofanya udandanyifu ili wajiandikishe zaidi 

ya mara moja wanatenda kosa na wakibainika wanaweza 

kufungwa jela kifungo kisichopungua miezi sita na kulipa faini.


Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya 

Uchaguzi, Mhe. Jaji (Rufaa) Jacobs Mwambegele leo tarehe 

25 Julai, 2024 wakati akizungumza na waandishi wa habari 

mkoani Geita.  


“Ningependa kusisitiza kuhusu suala la kujiandikisha kuwa 

mpiga kura zaidi ya mara moja, jambo hili ni kosa la kisheria 

kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 114(1) cha Sheria ya 

Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na.1 ya Mwaka 

2024,” amesema.


Jaji Mwambegele amefafanua kuwa kifungu hicho kinasema 

mtu yeyote atakayeomba kuandikishwa zaidi ya mara moja 

atakuwa ametenda kosa la kisheria na akitiwa hatiani adhabu 

yake ni faini isiyopungua kiasi cha shilingi laki moja 

(100,000/=) na isiyozidi shilingi laki tatu (300,000/=) au 

kutumikia kifungo kwa kipindi kisichopungua miezi sita na 

kisichozidi miaka miwili au vyote kwa pamoja.  


Katika hatua nyingine, Jaji Mwambegele amesisitiza kuwa 

hakuna uwezekano wa mtu kujiandikisha  mara mbili na 

taarifa zake kusalia kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga 

Kura kwa kuwa kabla ya kutoa nakala ya mwisho, Tume 

hulisafisha Daftari kwa kuwaondoa wapiga kura 

waliojiandikisha zaidi ya mara moja.


“Mara baada ya uandikishwaji wa wapiga kura kukamilishwa, 

taarifa zote huingizwa kwenye mfumo wa AFIS (Automated 

Finger Print Identification System) ambao huwaonesha wote 

waliojiandikisha kwenye Daftari zaidi ya mara moja. Wapiga 

kura wa aina hii hufutwa moja kwa moja kwenye vituo vyote 

na kuwabakisha kwenye kituo alichojiandisha mara ya 

mwisho,” amesema.


Ameongeza kuwa orodha ya waliojiandikisha zaidi ya mara 

moja hupelekwa Jeshi la Polisi kwa ajili ya hatua za kisheria 

na kwamba Tume imefanya hivyo katika chaguzi za nyuma 

ambapo katika uandikishaji uliofanyika mwaka 2015, Tume 

ilibaini jumla ya wapiga kura 52,078 waliojiandikisha zaidi ya 

mara moja ambapo orodha yao ilikabidhiwa kwa Jeshi la 

Polisi tarehe 27 Agosti, 2015 kwa ajili ya hatua za kisheria.


“Katika uboreshaji wa Daftari wa mwaka 2020, Tume ilibaini 

majina ya watu 42,301 ambao walijiandikisha zaidi ya mara 

moja na orodha hiyo ilikabidhiwa kwa vyombo vinavyohusika 

na makosa ya kijinai,” amesema Jaji Mwambegele.


Ameeleza kuwa baada ya kukamilika kwa uchakataji wa 

Daftari, Tume huchapisha na kuweka wazi Daftari hilo chini 

ya kifungu cha 24 cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge 

na Madiwani, Na. 1 ya mwaka 2024 ambapo wananchi 

hulikagua.


“Baada ya kukamilika kwa uchapishaji wa mwisho wa Daftari 

la Kudumu la Wapiga Kura, vyama vya siasa hupewa nakala 

tepe (soft copy), haijawahi kutokea jina likajitokeza zaidi ya 

mara moja. Hivyo, hakuna uwezekano wa mtu kuandikishwa 

zaidi ya mara moja na kuweza kutumia nafasi hiyo kuwa 

kwenye vituo zaidi ya kimoja siku ya kupiga kura,” amesema 

Jaji Mwambegele.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.