Habari za Punde

Uwasilishaji Mradi wa Vijana Plus ambao utawafikia makundi mbali mbali ya vijana wa Zanzibar.

Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Vijana Zanzibar, Shaib Ibrahim Mohamed, Mratibu kutoka Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani,  (Save the Childen) Barnabas Kaniki   na Mratibu kutoka Tanzania  Bora Initiative, , Alfred Kiwuyo pamoja na Maafisa wa Wizara hiyo  katika hafla fupi ya kuutambulisha  Mradi wa Vijana Plus huko Migombani, Wilaya ya Mjini.

Imetolewa na Kitengo cha Habari,Mawasiliano na Uhusiano.

Na.Khadija Khamis , WHVUM.

Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Vijana Zanzibar, Shaib Ibrahim Mohamed amelishukuru Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani, Save the Childen na Tanzania  Bora Initiative,  kwa uwasilishaji  wa mradi wa Vijana Plus  ambao utawafikia  makundi mbali mbali ya vijana wa Zanzibar.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana,Utamaduni na  Michezo Ndugu Fatma Hamad Rajab katika hafla fupi ya utambulisho wa mradi wa ‘ Vijana Plus’ katika  ukumbi wa Wizara hiyo Migombani Wilaya ya Mjini.

Amesema  mradi huo utasaidia kuwajengea uwezo vijana katika usimamizi na utekelezaji wa mashirika yao ili kuepukana na changamoto zinazowakwamisha  katika  uimarishaji wa maendeleo yao.

Aidha amewaomba mashirika hayo kuendeleza mashirikiano yao na Wizara ya Habari, Vijana Utamaduni na michezo  ili kuhakikisha mradi huo unatekelezwa ipasavyo  na kuleta tija jambo ambalo litasaidia  kuimarisha ustawi na maendeleo ya vijana  Wazanzibar.

Amesema Wizara ya Habari Vijana Utamaduni na Michezo  inaratibu na kusimamia maendeleo ya vijana, utekelezaji wa maendeleo hayo  hutekelezwa na wadau mbali mbali wa sekta za  Serikali, Sekta Binafsi pamoja na wadau mbali mbali  kutoka ndani na  nje ya nchi,  Wizara inatambua uwepo wao  kwa mujibu wa Sera ya Maendeleo ya Vijana ya Mwaka 2023.

Nae Mtaalamu wa Ulinzi na Utawala wa Haki za Watoto kutoka  Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani,  (Save the Childen) Barnabas Kaniki  amesema lengo la mradi wa Vijana Plus ni kuyawezesha mashirika ya Vijana na viongozi wake kuwa wadau wakuu kwenye masuala ya utawala bora na maendeleo.

Amefahamisha kuwa vijana watakaolengwa kupatiwa fursa hiyo katika mradi huo ni kati ya umri wa miaka 15 hadi 29  katika kanda  mbali mbali iliyopangiwa ikiwemo Dodoma , Mwanza , Tanga,  Zanzibar, Mtwara, Mbeya, Kigoma pamoja na  Morogoro.

Ameeleza kuwa mradi huo utawajengea uwezo vijana wa mashirika 40 kwa kuzitatua changamoto zilizopo na kuwapa elimu viongozi  wao 100 kutoka katika mashirika hayo ili kuwajengea uwezo kiufanisi.

Kwa upande wa Mratibu wa Mradi kutoka Tanzania Bora Initiative, Alfred Kiwuyo amesema anatarajia mradi huo utawafikia vijana wengi ambao bado hawajawahi kufikiwa ili kufikia lengo lililokusudiwa kwa kuwafungulia njia za kimaendeleo.

Amesema makongamano mbali mbali yatafanyika ili kuwapa fursa vijana wa sekta tofauti mashirika na makundi mbali mbali ikiwemo wajasiriamali,wasanii pamoja na  waandishi wa habari ili kuwaengezea ujuzi katika maeneo wanayofanyia kazi.

Mradi wa Vijana Plus ni wa miaka mitatu ulianza mwaka 2025 hadi 2028 unaotarajiwa kuwafikia vijana wa kitanzania 711,880 ikifadhiliwa na  Save the Childen wakishirikiana  na Tanzania bora Initiative, mradi huo umewekwa Bajeti ya  Auro Milioni 2.2 .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.