Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad akizungumza na wanachama wa chama hicho baada ya kuweka jiwe la msingi katika ofisi ya CUF Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad akizungumza na wanachama wa chama hicho baada ya kuweka jiwe la msingi katika ofisi ya CUF Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam. (Picha, Salmin Said, OMKR).
Na Hassan Hamad OMKR
Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad ameupongeza uongozi wa Chama hicho Wilaya ya Kinondoni mjini Dar es Salaam kutokana na juhudi unazozichukua katika kukiendeleza Chama hicho.
Amesema uongozi wa CUF katika Wilaya hiyo ni mfano wa kuigwa na Wilaya nyengine, na kuwasisitiza wanachama kuendeleza ushirikiano na viongozi wao ili kukiimarisha zaidi Chama hicho katika ngazi ya wilaya hadi Taifa.
Maalim Seif ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ametoa pongezi hizo baada ya kuweka jiwe la msingi katika jengo la ofisi ya CUF Wilaya ya Kinondoni.
Amesema ujenzi huo wa ofisi za kisasa katika ngazi ya Wilaya ni hatua muhimu ya kukiimarisha chama hicho na kutaka Wilaya nyengine ziige mfano huo katika kuimarisha majengo ya ofisi zao.
Katika hatua nyengine Maalim Seif amewaomba wananchi wa Wilaya hiyo kuendelea kukiunga mkono chama hicho, ili kiweze kuendeleza jitihada zake za kuibua na kukabiliana na ufisadi unaohujumu uchumi wa nchi.
“Nakuombeni sana wananchi wa Wilaya hii muendelee kukiunga mkono Chama Cha Wananchi CUF kwani ndio Chama pekee kinachoweza kuondosha ufisadi”, alisema Katibu Mkuu huyo wa CUF.
Mapema kaimu Mwenyekiti wa CUF Wilaya ya Kinondoni bwana Juma Shaaban Nkumbi amesema jengo hilo linalotarajiwa kugharimu shilingi milioni 13 litakuwa na huduma zote muhimu na litatumiwa na wanachama kwa shughuli mbali mbali.
Bwana Nkumbi amekemea tabia ya baadhi ya wanachama na viongozi kushutumiana na kupikiana majungu, na kuwataka kuachana na tabia hiyo ambayo amesema ni hatari kwa maendeleo ya Chama.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CUF Tanzania bara bwana Julius Mtatiro, amesifu usimamizi mzuri na matumizi ya fedha za umma unaofanywa na viongozi wa CUF katika Wilaya hiyo, na kuwataka viongozi hao kuendeleza moyo huyo, ili kuleta matumaini zaidi kwa wanachama na wananchi kwa jumla.
Katika hafla hiyo Maalim Seif alikabidhi vyeti maalum kwa viongozi wa matawi na kata mbali mbali kutokana na mwamko wao wa kukichangia chama hicho na kukiendeleza.
No comments:
Post a Comment