Habari za Punde

Zanzibar ina Haki Kusajili Meli

Waziri akanusha meli za Iran kusajiliwa. 
Ataka isichonganishwe na mataifa ya nje .


Na Ramadhan Makame


WAZIRI wa Miundombinu na Mawasiliano, Hamad Massoud Hamad amesema kuwa Zanzibar haifungiki na inayo mamlaka kwa mujibu wa sheria za ndani za kimataifa kusajili meli za kigeni kutoka nchi yeyote duniani.

Waziri huyo alieleza hayo jana katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi alipokuwa akitoa taarifa ya serikali kwa wajumbe wa Baraza hilo, kuelezea kuwa hakuna meli zilizosajiliwa Zanzibar zenye kufanya biashara ya mfuta nchini Iran.

Serikali imelazimika kupeleka taarifa katika Baraza la Wawakilishi kufuatia katika kikao cha juzi Mwakilishi wa jimbo la Mji Mkongwe (CUF), Ismail Jussa Ladhu, kutaka kujadiliwa kwa hoja hiyo kwa dharura.


“Kulingana na “United Nations Convention Law of the Sea”, Article 91, na za “Geneva convection of Registration” articles 6, 7 na 8, na kulingana na Zanzibar Maritime Transport Act of 2006, section 8, Zanzibar ikiwa ni nchi moja kati ya nchi mbili zinazounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inayo haki ya kusajili meli yoyote kulingana na taratibu na sheria za Zanzibar, na sheria za kimataifa zinazoongoza usajili huo”, ilieleza taarifa hiyo.
         
Alisema pamoja na Zanzibar kuwa na uwezo kisheria wa kusajili meli, imekuwa ikifanya kazi hiyo kwa umakini na hakuna meli za Iran zilizosajili zenye kupeperusha bendera za Tanzania kwa kukwepa vikwazo.

Alifahamisha kuwa vyombo vya habari vilivyoandika taarifa hizo vilikuwa na malengo ya uchonganishi na kwamba hakuna meli hata moja ya Iran iliyosajiliwa katika Mamlaka ya Usafiri wa Bahari.

Waziri Hamad alisema katika suala lisilo la Muungano kama la usafiri wa bahari, Zanzibar isiingiliwe katika utendaji wake kama vile ilivyokuwa haiingilii SUMATRA, ila inaweza kupokea ushauri.

Waziri huyo alifafanua kuwa katika muda wa wiki mbili kampuni zilizosajiliwa Zanzibar hakuna hata moja inayotoka nchini Iran ambapo zote zinatoka katika nchi za Cyprus na Malta.

          “Hii ni biashara yenye kuipatia mapato makubwa serikali, kusajili meli 11 zaenye jumla ya GRT 1,388,368 tons, hivyo suala lisiwe sababu ya kuleta uchonganishi na kuharibu mahusiano ya Zanzibar na nchi za nje, Zanzibar isishirikishe na mambo hayo”,alisema waziri huyo.

Alieleza kuwa Zanzibar ina uhusiano mkubwa na wa muda mrefu na nchi nyingi ikiwemo Iran na hivi karibuni ilipata ugeni wa Makamo wa Rais wa Iran na viongozi wa nchi hiyo walifanya mazungumzo  namna Iran itakavyoendelea kuisaidia Zanzibar katika miradi ya Maendeleo.

“Zanzibar haingependa kuingizwa kwa visingizio vyovyote na kwa njama zozote katika migogoro isiyowahusu”,alisema waziri huyo.
         
Akizungumzia juu ya meli nyingi za kimataifa zinazosajiliwa Zanzibar kuwa zimechakaa, alisema kabla ya meli hizo kusajiliwa hukaguliwa na wangalizi kimataifa na kijiridhisha kuwa zinaubora wa kufanya kazi.

         

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.