Na
Salum Vuai, Maelezo
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Said Ali Mbarouk, ametaka Chama
cha Soka Zanzibar (ZFA), kisiingiliwe katika utendaji wake wala kubughudhiwa.
Akifungua mkutano wa uchaguzi mdogo wa Rais wa chama hicho kwenye hoteli ya
Bwawani jana, Mbarouk alisema ni vyema ZFA iachiwe ifanye kazi zake za
kuendesha soka kwa kufuata katiba na kanuni zake na kujipangia mikakati ya
maendeleo kwa maslahi ya nchi.
"Natoa wito kwa taasisi zangu zote zilizomo ndani ya wizara yangu,
kuiachia ZFA kufanya kazi zake kwa mujibu wa katiba na kanuni zake bila
kuingiliwa", alisisitiza Waziri huyo.
Mbarouk alifahamisha kuwa, hata mashirikisho ya kimataifa ya mpira wa miguu
kama vile FIFA, CAF na CECAFA, yanakataza vyama vyote vya soka kuingiliwa
shughuli zao na serikali za nchi husika, isipokuwa katika masuala ya timu za
taifa.
Alisema kwa hatua ambazo ZFA imezifikia katika siku za karibuni, ni dalili kuwa
sasa inajiweza, na kuongeza kuwa wizara yake inakipongeza kwa dhati chama
hicho.
Alizitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na kupata mdhamini wa ligi kuu kwa
kushirikiana na wizara, kampuni ya TBL kupitia kinywaji chake kisicho na kilevi
cha Grand Malt, kumudu kuiandaa timu ya taifa Zanzibar Heroes na kuipeleka
Kurdistan kwenye mashindano ya dunia kwa nchi ambazo si wanachama wa FIFA.
Aidha alisema kuandaa mashindano ya Kombe la Urafiki Tanzania yanayotarajiwa
kuanza leo, ni ishara njema kwamba chama hicho kimeanza kukua na kuendesha mambo
yake chenyewe.
Waziri huyo alielezea matumaini yake kuwa uchaguzi huo wa jana, utaleta faraja
kwa Wazanzibari kwa kutoa mwanga na dira nzuri na njema kwa maendeleo ya
mpira wa miguu hapa Zanzibar.
No comments:
Post a Comment