Na
Hassan Hamad, OMKR
BALOZI
wa Tanzania nchini Marekani, Mwanaidi Maajar amesema Zanzibar inaweza kupiga
hatua katika kukuza sekta ya utalii iwapo itaimarisha miundombinu ya uwekezaji
katika sekta hiyo.
Balozi
Maajar, alieleza hayo jana alipokuwa na mazungumzo na Makamu wa Kwanza wa Rais
wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad huko
nyumbani kwake Mbweni, nje kidogo ya mji wa Zanzibar.
Alisema
katika kukuza sekta hiyo ni lazima serikali itenge fungu maalum litakalokidhi
haja ya kuimarisha miundombinu ya utalii, ikiwa ni pamoja na kuitangaza sekta
hiyo katika nchi za nje.
“Ni
lazima serikali ikubali kutenga fedha nyingi kwa ajili ya kuutangaza utalii,
sambamba na kuwekeza katika maeneo ambayo yanaweza kuwavutia watalii”,
alifafanua Balozi Maajar.
Alisema
kuwa Zanzibar ina vivutio vingi vya utalii
vikiwemo mashamba ya viungo, na kwamba iwapo vitatumiwa vizuri vinaweza
kuwavutia watalii wengi zaidi na kuinyanyua Zanzibar kiuchumi.
Kuhusu
kilimo, Balozi Maajar aliishauri serikali kuandaa programu zinazolenga
kuendeleza kilimo na kuzituma kwa taasisi zinazojihusisha na kilimo nchini
Marekani, ili ziweze kutoa msukumo katika kilimo hasa cha umwagiliaji.
Kwa
upande wake Makamu wa Kwanza wa Rais Maalim
Seif Sharif Hamad, alisema kwa sasa serikali imeweka mkazo katika kuiendeleza
sekta ya utalii ambayo inatoa mchango mkubwa katika upatikanaji wa fedha za
kigeni.
Alisema
malengo ya serikali ni kufikia watalii milioni moja katika kipindi cha miaka 10
ijayo, na kuelezea haja ya kuimarisha miundombinu na soko la utalii nchini.
Kwa
upande mwengine Maalim Seif amesema serikali inaangalia uwezekano wa kuweza
kushirikiana na jumuiya za kimataifa katika kukabiliana na wimbi la uingizaji
wa dawa za kulevya nchini.
Alifahamisha
kuna uwezekano kwamba baadhi ya dawa zinaingizwa Zanzibar
kama njia ya kupitishia dawa hizo kwenda nchi
nyengine, lakini baadhi ya wafanyabiashara wakorofi wamekuwa wakitumia ujanja
kuziingiza dawa hizo na kuwaathiri vijana ambao ndio nguvu kazi ya taifa.
Makamu
huyo alisema Zanzibar na Marekani zimekuwa na ushirikiano
mzuri na kuipongeza misaada mbali mbali inayolewa na nchi hiyo kwa Zanzibar ambayo inasaidia
kutatua kero za wananchi na kusaidia mipango ya maendeleo.
Alisema
Marekani imekuwa ikitoa misaada mbali mbali hasa katika sekta ya elimu, na
kuiomba nchi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar
katika mipango yake ya maendeleo na kukuza uchumi.
No comments:
Post a Comment