Habari za Punde

Mwanafunzi Mjamzito anywa Dawa ya Panya


Na Masanja Mabula, PEMBA
MWANAFUNZI wa darasa la saba skuli ya msingi Uwondwe shehia ya Mtambwe kaskazini wilaya ya Wete, Ruwaida Khamis Muhusini (17) amelazwa katika hospitali ya Wete akidaiwa kunywa sumu kutaka kujiua baada ya kubainika kuwa na ujauzito.

Akizungumza na Zanzibar Leo, akiwa katika wodi alikolazwa, mwanafunzi huyo, alisema kuwa uwamuzi wa yeye kutaka kujiuwa ni baada ya kuhojiwa na wazazi wake juu ya ujauzito huo ambapo aliona aibu kutokana na kitendo hicho.


Alisema wazazi wake walitaka kujua kuhusiana na mimba hiyo ambapo alihojiwa na kumtaja aliyempa ujauzito, lakini wazazi wake hawakuonesha kama wana hasira kutokana na hali hiyo.

“Nimekunywa sumu ya panya nikiwa na lengo la kutaka kujiuwa baada ya wazazi kunibaini kuwa nina ujauzito, niliona aibu na uwamauzi huu niliuchukua baada ya baba kwenda msikitini kusali sala la alfajiri”, alifahamisha.

Naye mama mzazi wa mwanafunzi huyo, Mariam Haji Shehe alisema kuwa mwanawe alihojiwa na baba yake juu ya ujauzito huo, lakini hakukuwa na hali yoyote ya kutaka kumpa adhabu.

“Baba yake alimhoji na hakuchukua hatua nyingine kwani alikuwa anaandaa utaratibu wa kumpa aliyehusika na kitendo cha kumpa mimba mwanawe, lakini cha kushangaza mtoto alichukua uamuzi wa kutaka kujiuwa na bahati nzuri walimuwahi na kumpa maziwa ili kuuwa sumu”, alisema.

Daktari aliyempokea mgonjwa huyo, Hamad Mohammed Nassor wa hospitali ya Wete alisema uchunguzi wa kitaalamu umebaini kuwa mwanafunzi huyo ana ujauzito wa zaidi ya miezi mitatu.

Alisema kuwa tofauti na wakati wanampokea hali yake kiafya inaendelea vyema ambapo ameshapatiwa huduma zinazostahili lengo ni kuokoa maisha yake.

Kwa upande wake ofisa Ustawi wa Jamii wilaya ya Wete, Horuob Suleiman Hemed alikiri kupokea taarifa za mtoto huyo na kuahidi kufuatilia ili kuhakikisha kuwa muhusika aliyempa mamba hiyo anatiwa mikononi mwa vyombo vya sheria.

Hata hivyo alielezea wasiwasi wake kwa vyombo hivyo kutokana na mapungufu ya ufuatiliaji wa kesi za udhalilishaji wa watoto sambamba na jamii nayo kuwa rushwa muhali jambo ambalo linakwamisha juhudi za kutokomeza vitendo hivyo.

Taatifa zilizopatikana zinaeleza kuwa kijana aliyehusika na kumpa ujauzito mwanafunzi huyo anaishi kisiwani Unguja katika maeneo ya Kibweni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.