04/07/2012
Kwa Uongozi wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu( JUMIKI)
S.L.P 1266
Mkunazini-Zanzibar
Assalama Aleikum,
Kuhusu: MUWAZA inapongeza Msimamo wa JUMIKI kushiriki katika
Mkakati wa zoezi la kutunga Katiba Mpya
Kwa niaba ya Wanachama wa Jumuiya ya Mustakbal wa Zanzibar (MUWAZA),
Muungano wa Wazanzibari ng'ambo, tunaipongeza Jumuiya ya JUMIKI kwa uamuzi wa
kijasiri na kishujaa wa Viongozi wake kushiriki pamoja na Wazanzibari wenziwao
wote katika mchakato wa kutafuta katiba mpya ya Tanzania na kukataa katakata
suala zima la kususia zoezi hilo. MUWAZA inakubaliana kwamba ususiaji wa namna
yeyote wa zoezi hilo utatoa mwanya unaotakiwa na Watu wasioitakia mema
Zanzibar, na ambao wanaweza kuutumia mwanya huo kujifanya wao ndio
wasemaji pekee halali wa Wazanzibari. Ni kushiriki kwa wingi na kikamilifu
katika kutoa maoni mbele ya tume hiyo ya Jaji Warioba ndipo wananchi wa Zanzibar
wataweza kudhihirisha hadharani chaguo gani wanalitaka kuhusu mustakbali wa
maisha yao ya baadae ndani ya Zanzibar. Hii ni fursa nzuri na ya nadra ambapo
Wazanzibari wataweza kurejesha heshima ya nchi yao na ya Viongozi wao.
Hata hivyo, MUWAZA inawashauri Viongozi wa JUMIKI, kama inavowashauri ndugu
zetu Wazanzibari, kwamba fursa hii ya mchakato wa katiba mpya itumike kwa
amani na ustaarabu wa kizanzibari unaothaminiwa duniani kote wa kustahamilia
kila mmoja wetu maoni ya mwenzake, hata kama hakubaliani nayo, kikubwa
kabisa ni kuweka maslahi ya juu kabisa ya visiwa vya Zanzibar na wengi wa
watu wake.
MUWAZA, kama ilivyo JUMIKI, pamoja na Wazanzibari wote wanaopenda amani na
maendeleo ya visiwa vyao, kwa nguvu zote unapinga kabisa matumizi ya nguvu na
mabavu dhidi ya wananchi, bila ya kujali kama vitendo hivyo vinafanywa na
taasisi za dola, vyama vya kisiasa, jumuiya yeyote au mtu mmoja mmoja
binafsi. Tunasisitiza haja ya vyombo vya dola, Vyama vya kisiasa, Jumuiya za
kiraia na Wananchi kwa jumla kutetea na kuheshimu amani ya nchi, uhuru wa watu
wote kuweza kutoa maoni yao na kukusanyika kwa njia huru, bila ya vizuwizi na
vikwazo, mradi wanaambatana na sheria na kulinda amani.
MUWAZA inaamini zoezi la kuwaelimisha Wananchi juu ya haki zao za kikatiba
na kuwazindua juu ya sheria ambazo hazitekelezwi vilivyo kama
ilivokusudiwa, hivyo kupelekea wananchi kukandamizwa na kupoteza haki zao za
kimsingi, ni harakati endelevu isiokuwa na kiwango cha wakati na kipindi.
Hivyo, tunakubali kwamba ni juu ya dola kuweka mazingira mazuri kwa jambo
hilo kufanyika. Ni imani ya MUWAZA kwamba wananchi wanapozidi kuwa na mwamko
zaidi wa kutambua haki zao na kuelewa namna ya kuzipigania kwa njia ya amani,
pamoja na kuelewa namna nchi yao inavotawaliwa na inavofaa kutawaliwa siku za
mbele ni faida kwa nchi yetu na maendeleo yake.
MUWAZA inakubaliana nanyi kwamba kuna mambo kadha ya dhuluma ndani ya
Muungano, kama ulivo sasa, kwamba Muungano huo umekuwa zaidi wa kiserikali.
Hivyo iko haja ya kuuimarisha zaidi Muungano wa Kijamii na kuondosha dhuluma
zilizokuweko mnamo miaka 48 iliopita.
Kama ilivyo JUMIKI, MUWAZA imelikaribisha kwa tamko la Mheshimiwa Jaji Warioba alilolitoa
mbele ya Waandishi wa habari alipoizindua Tume ya kukusanya maoni juu ya
katiba mpya mjini Dar es Salaam tarehe 18/06/2012 kwamba maoni yote
yataheshimiwa na kuzingatiwa, likiwemo suala la Muungano ambalo kwa Wazanzibari
ndilo suala muhimu.
Pia MUWAZA inatarajia, kutokana na watu waliomo ndani ya Tume ya Jaji
Warioba, kwamba uadilifu, haki na uwazi utaoneshwa katika zoezi la
kukusanya maoni ya Wananchi, maoni ya wananchi walio wengi yataheshimiwa na
tume na baadae na Serikali ya Muungano wa Tanzania na ya Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar.Tunaitarajia Tume ya Warioba na Serikali zote mbili zitahakikisha
watu wanatoa maoni yao bila ya kutishwa waseme nini mbele ya Tume, kwamba
hawataadhibiwa kwa namna yeyote juu ya usalama na ajira zao baada ya kutoa
maoni yao mbele ya tume. Tunawahimiza Wazanzibari waseme wazi, tena kwa midomo
mipana, pindi wanatiwa hofu ya aina yeyote wakati wa zoezi hilo.
Kama ilivyo JUMIKA, MUWAZA inatoa mwito kwa Wazanzibari wote waungane
kwa kauli moja ya kurejesha heshima ya rais wa Zanzibar na nchi yao, na kwamba
chimbuko la mamlaka maisha libakie ndani ya mikono ya wananchi.
MUWAZA inapinga vikali vitendo vyovyote vya kuwabeza Wazanzibari wanaopinga
mfumo ulioibakisha nchi yao nyuma kwa miaka na kuwabakisha
wananchi wake wengi katika ufukara na maendeleo duni katika nyanja za
elimu, afya na huduma nyingine za kijamii.
Tunawatakia Wazanzibari kila la kheri, amani na maendeleo, na hayo
yatafikiwa tu ikiwa wenyewe Wazanzibari, katika mazingira yalio huru na ya
amani, watafanya maamuzi sahihi kwa pamoja katika kipindi hiki muhimu cha
historia ya nchi yao.
Iiishi Zanzibar.
Mwenyekiti
Jumuiya ya MUWAZA
UK
No comments:
Post a Comment