Habari za Punde

Makamu wa Rais Maalim Seif akutana na Balozi wa Tanzania Marekani.


.     Balozi wa Tanzania nchini Marekani bibi Mwanaidi Maajar akitoa ufafanuzi juu ya maendeleo mbali mbali ambayo Zanzibar na Marekani zinaweza kushirikiana wakati wa mazungumzo yake na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad huko nyumbani kwake Mbweni Zanzibar. (Picha, Salmin Said OMKR).

Hassan Hamad, OMKR.
Balozi wa Tanzania nchini Marekani bibi Mwanaidi Maajar amesema Zanzibar inaweza kupiga hatua kubwa katika kukuza sekta ya utalii iwapo itaimarisha miundombinu ya uwekezaji katika sekta hiyo.

Balozi Maajar ameeleza hayo leo alipokuwa na mazungumzo na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad huko nyumbani kwake Mbweni, nje kidogo ya mji wa Zanzibar.


Amesema katika kukuza sekta hiyo ni lazima serikali itenge fungu maalum litakalokidhi haja ya kuimarisha miundombinu ya utalii, ikiwa ni pamoja na kuitangaza sekta hiyo katika nchi za nje.

“Ni lazima serikali ikubali kutenga fedha nyingi kwa ajili ya kuutangaza utalii, sambamba na kuwekeza katika maeneo ambayo yanaweza kuwavutia watalii”, alifafanua balozi Maajar.

Amesema Zanzibar ina vivutio vingi vya utalii vikiwemo mashamba ya viungo, na kwamba iwapo vitatumiwa vizuri vinaweza kuwavutia watalii wengi zaidi na kuinyanyua Zanzibar kiuchumi.

Kuhusu kilimo, balozi Maajar ameishauri serikali kuandaa program zinazolenga kuendeleza kilimo na kuzituma kwa taasisi zinazojihusisha na kilimo nchini Marekani, ili ziweze kutoa msukumo katika kilimo hasa cha umwagiliaji.

Kwa upande wake Makamu wa Kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad amesema kwa sasa serikali imeweka mkazo katika kuiendeleza sekta ya utalii ambayo inatoa mchango mkubwa katika upatikanaji wa fedha za kigeni na uchumi wa Zanzibar kwa ujumla.

Amesema malengo ya serikali ni kufikia watalii milioni moja katika kipindi cha miaka kumi ijayo, na kuelezea haja ya kuimarisha miundombinu na soko la utalii nchini.

Kwa upande mwengine  Maalim Seif amesema serikali inaangalia uwezekano wa kuweza kushirikiana na jumuiya za kimataifa katika kukabiliana na wimbi la uingizaji wa dawa za kulevya nchini.

Amesema kuna uwezekano kwamba baadhi ya dawa zinaingizwa Zanzibar kama njia ya kupitishia dawa hizo kwenda nchi nyengine, lakini baadhi ya wafanyabiashara wakorofi wamekuwa wakitumia ujanja kuziingiza dawa hizo na kuwaathiri vijana ambao ndio nguvu kazi ya taifa.

Amesifu ushirikiano uliopo mzuri kati ya Zanzibar na Marekani, na kuishukuru nchi hiyo kutokana na misaada mbali mbali inayoito kwa Zanzibar  ambayo inasaidia kutatua kero za wananchi na mipango ya maendeleo.

Amesema Marekani imekuwa ikitoa misaada mbali mbali hasa katika sekta ya elimu, na kuiomba nchi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika mipango yake ya maendeleo na kukuza uchumi.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.