Habari za Punde

Dijitali yachukua nafasi mswada ZBC



Na  Mwantanga Ame
KAIMU Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Abdilah Jihadi Hassan, amesema mswada wa sheria ya uanzishwaji shirika la utangazaji Zanzibar (ZBC), utaifanya Zanzibar kufuata mfumo wa kimataifa katika kutoa matangazo yake.
Hayo aliyasema jana wakati akiwasilisha mswada huo mbele ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi katika kikao kinachoendelea Chukwani nje kidogo ya mji wa Zanzibar.

Waziri  huyo ambaye pia ni Waziri wa Uvuvi, alisema mengi ya mashirika ya kimataifa yanafanya kazi zake kwa ufanisi  kwa lengo la kuyaweka katika mfumo ya kimataifa inayotumika sasa katika baadhi ya nchi.


Alisema mswada huo utawezesha kupunguza gharama za uendeshaji katika vyombo vya habari vya serikali na italeta ufanisi kwa wasikilizaji wa  redio na televisheni.

Alisema mfumo wa sasa wa dunia umekuwa ukiendesha vyombo vya habari kwa mtindo wa mashirika kama lilivyo la BBC, Xinhua, Reuters na CNN ambayo yameonekana kujiendesha kwa faida na ufanisi katika mfumo wa utangazaji.
Alisema kuja kwa sheria hiyo, kutaweza kulifanya ZBC, kuwa na mfumo wa kisasa unaokubalika kimataifa.
Alisema pia mswada huo utasaidia kuweka mazingira mazuri ya kazi kwa watumishi wa shirika hilo ikiwa ni  pamoja na kuwawezesha kuwa na vifaa vya kisasa na kuimarisha uongozi wa shirika hilo.
Kamati ya Mifugo, Utalii, Uwezeshaji na Habari ya Baraza la Wawakilishi, imesema kwamba mswada huo  utalifanya shirika hilo kuwa bora zaidi katika matangazo yake ikiwa ni pamoja na kujiendesha kibiashara na kiushindani na utoaji huduma bora kwa kuangalia rika.

Mjumbe wa kamati hiyo, Salim Abdalla Hamad, akisoma maelezo ya kamati, alisema kwa vile mswada huo umezingatia mambo mengi yatakayoliwezesha shirika hilo kuwa na mabadiliko ni vyema kwa viongozi na watendaji wakafanya kazi kwa ufanisi.

Alisema kazi kubwa ambayo itahitajika kufanywa na shirika hilo ni kuzingatia suala la utafiti wa habari zake na uwakilishi wa wananchi wa mjini na vijijini.
Nae Mwakilishi wa Mtambile, Mohammed Haji Khalid, akitoa maoni yake juu ya mswada huo aliomba shirika hilo kuwa makini katika kufanya kazi zake hasa taarifa na vipindi ili visivunje maadili ya Mzanzibari.

Nae Mwakilishi wa Matemwe, Abdi Mosi, alisema ni vyema wakati shirika hilo likiimarishwa suala kubwa la kuangaliwa ni namna ya kuwa na vipindi bora vitakavyoweza kutoa elimu ya kilimo, ustawi wa jamii na uimarishaji utamaduni.

Mwakilishi wa viti vya wanawake ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati hiyo, Asha Bakari Makame, alisema ipo haja kwa shirika hilo likapewa vitendea kazi zaidi kwa sababu vilivyopo sasa haviendani na hadhi ya shirika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.