Habari za Punde

Dk. Bilal ahudhuria mazishi ya Makamu wa Rais Zimbabwe



Na Mwandishi wetu
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal ameiwakilisha Tanzania katika mazishi ya mpigania uhuru na mwanaukombozi wa Afrika, Komredi Landa John Nkomo yaliyofanyika katika makaburi ya mashujaa wa Zimbabwe, mjini Harare.
Komredi Nkomo hadi anafikwa na mauti alikuwa Makamu wa Rais wa Zimbabwe na Makamu Mwenyekiti wa chama cha ZANU-PF kinachoongozwa na Rais Robert Mugabe.
Nkomo alifariki Januari 17, 2013 nchini Afrika Kusini alikopelekwa kwa matibabu baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa kansa kwa miaka kadhaa na alifariki akiwa na umri wa miaka 79.
Mazishi hayo yaliongozwa na Rais Mugabe na  yalihudhuriwa na Makamu wa Rais wa Afrika Kusini, Zambia, Botswana na Namibia.

Maelfu ya wananchi wa Zimbabwe walihudhuria mazishi hayo huku wakionekana kuguswa na msiba huo mkubwa, hali iliyowafanya kutokuondoka katika eneo la mazishi hata pale mvua ilipokuwa ikinyesha.
Rais Mugabe wakati akilihutubia taifa alisema, hayati Nkomo alikuwa mfano thabiti wa amani katika Afrika na hata wakati anapelekwa Afrika Kusini kutibiwa alikuwa kinara katika mazungumzo ya kufikia mkataba wa makubaliano ya vyama vya siasa juu ya katiba itakayotumika kwa jili ya uchaguzi mkuu ujao nchini Zimbabwe, makubaliano yaliyopitishwa mapema juma lililopita.
Akizungumza na Dk. Bilal Ikulu jijini Harare, Rais Mugabe aliishukuru Tanzania kwa kuwa mshirika na ndugu wa karibu katika hali zote za maisha ya wananchi wa Zimbabwe na akafafanua kuwa udugu katika nchi hizo ni wa kutukuka na unatakiwa kulindwa na kuenziwa kwa vizazi vingi vijavyo.
Katika ziara hiyo fupi, Dk. Bilal licha ya kuhudhuria mazishi ya Nkomo, pia alipata fursa ya kumtembelea Rais Mugabe ofisini kwake ikulu jijini Harare na kisha kukutana na baadhi ya Watanzania waishio Zimbabwe katika makazi ya balozi wa Tanzania.
Katika maelezo mafupi aliyoyatoa kwa wananchi wa Tanzania waishio Zimbabwe, Dk. Bilal aliwataka kujiuliza kuhusu mambo yapi wanaona ni muhimu na bora kwa kuutangaza Utanzania na Mtanzania na kuwataka kuyatumia hayo hasa sasa wakati nchi inapoendelea na mchakato wa mabadiliko ya katiba ili yawe chachu ya uzalendo na taswira kwa kila Mtanzania kama yalivyo mataifa mengine.
Watanzania hao pia waliitaka serikali ya awamu ya nne kuwaelimisha wananchi wa Mtwara kuhusu umuhimu wa gesi kutumika kwa maendeleo ya taifa na wakamuomba Dk. Bilal kuwaelimisha wananchi hao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.