Habari za Punde

Umeme wakatisha kikao Barazani


Na Mwantaga Ame
TATIZO la kukatika mara kwa mara kwa umeme limesababisha kikao cha Baraza la Wawakilishi kushindwa kufanyika jana asubuhi.

Hali hiyo ilijitokeza wakati kikao hicho kikiendelea katika kipindi chake cha masuala na majibu.

Kabla ya Spika wa Baraza hilo Pandu Ameir Kificho, kuamua kuahirisha kikao hicho umeme huo ulikatika ghafla baada ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Baraza la Mapinduzi, Mwinyihaji Makame kumaliza kujibu suala la Mwakilishi wa jimbo la Chaani, Ussi Jecha Simai.

Kutokana na hali hiyo Spika Kificho, alitoa tangazo la kuahirisha kwa muda kikao hicho na kuwataka wajumbe wa Baraza hilo kusubiri hadi umeme huo urudi.

Hata hivyo, wakati Spika akijitayarisha kutoka katika ukumbi huo huduma ya umeme ilirudi na kuwataka wajumbe hao kuendelea na kikao hicho.   


Wajumbe hao walianza kikao hicho lakini pia walijikuta wakiifanya kazi hiyo kwa muda mfupi baada ya umeme  kukatika tena jambo ambalo lilimfanya Spika kutoa tangazo la moja kwa moja kuwataka wajumbe kutoka katika kikao hicho.

Akiahirisha kikao hicho Spika huyo, alisema asingeweza kuendelea na kikao hicho kwa sababu umeme uliokuwa ukiwaka usingeweza kumudu kuendesha na vipoza hewa kutokana na kiwango chake kuwa kidogo.

Alisema hali hiyo ingeliweza kusababisha hali ya afya za baadhi ya wajumbe kuathirika.

Spika alisema kutokana na hali hiyo imemlazimu kuahirisha kikao hicho kwa vile tayari Shirika la Umeme lilishalitaarifu baraza hilo kuwa limo katika matengenezo baada ya kutokea hitilafu katika baadhi ya mitaa ya eneo hilo.

Alisema kwa vile hakuna uhakika wa muda gani wa mafundi wa shirika hilo wataweza kufanikiwa kukamilisha urejeshaji wa huduma hiyo,kikao hicho hakitaweza kuendelea hadi wakati wa jioni.

Kuahirishwa kikao hicho kulisababisha masuala yapatayo tisa kutoulizwa yakiwemo yanayohusu umeme, chumba cha wagonjwa mahatuti ,ICU, elimu ya juu, shirika la bandari, ushajiishaji wananchi katika kilimo cha umwagiliaji maji, uvunjaji wa shirika  la magari na utengzaji wa barabara.

Tatizo la kukatika umeme lilikuwa kubwa juzi usiku katika maeneo mengi ya Zanzibar.

Wakaazi wa eneo la Kisimamajongoo, Kikwajuni, Michenzani, Mazizini na Chukwani walikosa huduma hiyo  kwa siku ya pili jana baada ya kukatika nyakati za saa 2:15 usiku ambapo hadi jana mchana huduma hiyo ilikuwa haijarudi.

Hata hivyo wananchi wa Kikwajuni na Kisimamajongoo wameilalamikia hali hiyo kwa kujitokeza mara kwa mara ya kukatika umeme kunakosababishwa na kuunguwa kwa Trasfoma iliopo eneo la Kisimamajongoo.

Wananchi hao walieleza huenda ikawa tatizo hilo linatokana na trasfoma iliyowekwa ikawa ni ndogo kulingana na uwezo wa watumiaji kwani imekuwa ikiripuka mara kwa mara.

Ni siku chache tu wakati yakitokea ahayo Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Iddi alikaa na viongozi wa Shirika la Umeme na kuwataka kuona awanatekeleza majukumu yao vyema kutokana ana kuongezeka kwa vitendo vya ukatikaji wa huduma ya umeme mara kwa mara.

Hata hivyo sababu kubwa ambayo Shirika la Umeme imekuwa ikiitoa juu ya kuwepo kwa suala hilo ni kutokana na kuwepo kwa mabadiliko ya utandazaji wa waya mpya wa huduma ya umeme chini ya mradi wa MCC.

Hapo awali Shirika hilo lilitangaza kuwa litakamilisha kazi hiyo mwezi Disemba mwaka jana lakini tayari wametoa tarehe nyengine ya kukamilisha kazi hiyo kufikia mwezi Februari hadi Machi mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.