Habari za Punde

Mchina mbaroni akijaribu kumuhonga DC



Na Pascal Michael,Bunda
RAIA wa kigeni kutoka China, Mark Wang Wei amekamatwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wilayani Bunda wakati akijaribu kumuhonga Mkuu wa Wilaya hiyo rushwa ya shilingi 500,000 ili kampuni yake ipewe zabuni ya kusambaza pembejeo za kilimo wilayani humo.

Wang ni Mkurugenzi wa kampuni ya Panda International Co. Ltd.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa wilaya ya Bunda, Joshua Mirumbe alisema baada ya kushtukia jaribio hilo aliweka mtego uliofanikisha kukamatwa.

Alisema Mkurugenzi huyo alimtumia ujumbe mfupi kwa njia ya simu (sms) akimwambia  kuwa anamletea zawadi ya ahsante  ofisi kwake jambo lililomshangaza Mkuu huyo wa wilaya kwa kuwa alikuwa hajui kazi aliyofanya kiasi cha kupewa ahsante.

Mirumbe alisema Wang ni mmoja ya mawakala wanaotumiwa kusambaza pembejeo za kilimo na alitakiwa kuwasilisha kibali  cha kuishi nchini  na cha  kufanya kazi ili aingie mkataba na Halmashauri ya wilaya hiyo   kwa ajili ya kusambaza pembejeo za kilimo lakini baada ya kuoneka muda wake wa kuishi nchini unamalizika alinyimwa kibali hicho.


Lakini alisema raia huyo alifika ofisini kwake akiwa na barua kutoka Idara ya Uhamiaji ikimtambulisha kuwa kibali chake cha kuishi nchini kimeongezwa hadi Machi.

"Nilishangaa,  kwa kawaida  barua zote zinapaswa  kupelekwa masjala  lakini raia huyu aliniletea  moja kwa moja ofisini kwangu  barua iliyotoka Idara ya Uhamiaji ikimtambulisha  kuwa anacho kibali cha kuishi nchini  hadi mwezi Machi na baadae akanikabidhi bahasha ya fedha. 

Nikamuuliza fedha hizo ni za nini akaniambia ni ahsante, nikamuuliza ahsante  ya nini  au kazi gani niliyofanya, akaanza kubabaika  ndipo nilipowaita TAKUKURU ambao wapo karibu na kumkamata,” alisema.
Fedha hizo zilihesabiwa mbele ya mashahidi na kuonekana ni shilingi 500,000.
Raia huyo atafikishwa mahakamani baada ya uchunguzi kukamilika.

Akihojiwa na waandishi wa habari, Mchina huyo alikiri kutoa fedha hizo huku akisitiza kuwa  alimpa Mkuu huyo wa Wilaya kama ‘zawadi’ na kwamba hiyo siyo rushwa.

Kaimu Afisa kilimo wa wilaya ya Bunda, Masuke Ogwa, aliwaambia waandishi wa habari kuwa kampuni  ilikuwa bado haijaruhusiwa kusambaza pembejeo wilayani humo, kutokana na kutokuwa na vielelezo vinavyotakiwa vya kumruhusu kuishi nchini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.